Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Alifanikiwa Kuliko Alivyotarajia

Alifanikiwa Kuliko Alivyotarajia

Alifanikiwa Kuliko Alivyotarajia

“NILIJUA kwamba mwalimu wangu wa historia hakuwapenda Mashahidi wa Yehova lakini sikujua sababu,” asema Rebekka mwenye umri wa miaka 17 kutoka Ujerumani. Hivyo, wakati mwalimu alipowaomba wanafunzi wajitolee kutoa hotuba mbele ya darasa, Rebekka alisitasita. Hata hivyo, alijipa ujasiri na kumwomba mwalimu ruhusa ya kutoa hotuba kuhusu mnyanyaso wa Mashahidi wa Yehova chini ya utawala wa Wanazi wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu. Mwalimu alifurahia ombi hilo.

Wanafunzi walifurahia hotuba ya Rebekka na wakakubali kuchukua magazeti na vijitabu 44 vyenye habari hiyo. Baadaye, Rebekka alimpa mwalimu matokeo ya utafiti wake pamoja na vitabu kadhaa na video kutoka kwa watu wasio Mashahidi. Video moja ilionyesha jinsi Mashahidi wa Yehova walivyonyanyaswa huko Ujerumani Mashariki wakati wa Vita Baridi. Mwalimu aliifurahia sana kwa sababu hakujua habari hiyo.

Ndipo Rebekka alipogundua kwa nini mwalimu hakuwapenda Mashahidi wa Yehova. Mwalimu alisema kwamba kulikuwa na Shahidi wa Yehova katika shule aliyosomea. Mvulana huyo hakusema lolote kuhusu imani yake akiwa Shahidi. Kwa hiyo, mwalimu huyo akakata kauli kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu wasioeleweka na akaazimia kutoshirikiana nao. Lakini hotuba ya Rebekka ilibadili maoni yake. “Sasa ninaelewana na mwalimu huyo vizuri zaidi,” asema. “Pia nilijifunza kwamba tukiwa vijana tunapaswa kuongea na watu waziwazi kuhusu imani yetu.”

Lakini mambo hayakuishia hapo. Mwalimu huyo aliwaeleza walimu wenzake kuhusu hotuba nzuri sana ya Rebekka. Siku kadhaa baadaye, mwalimu wa somo la maadili alimwomba Rebekka atoe hotuba nyingine, lakini si mbele ya darasa moja tu bali wakati wa siku ya pekee sana, yaani, ukumbusho wa kila mwaka shuleni wa kukombolewa kwa wafungwa wa kambi ya mateso ya Auschwitz mwishoni mwa Vita ya Pili ya Ulimwengu. Wanafunzi wapatao 360 na walimu 10 walihudhuria. Baada ya hotuba hiyo, wahudhuriaji walipokea vijitabu 50, na shule ikaagiza vijitabu 150 zaidi vya kugawanya baadaye.

Rebekka alifanikiwa kuliko alivyotarajia. Alitoa ushahidi mzuri kuhusu imani yake darasani na vilevile mbele ya shule nzima. Pia mwalimu wake alianza kuwa na maoni yanayofaa kuhusu Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Heinrich Fundis alikatwa kichwa na Wanazi. Mamia ya Mashahidi wengine waliuawa pia

[Picha katika ukurasa wa 14]

Mashahidi wengi wa Yehova wangeachiliwa iwapo wangetia sahihi hati hii ya kukana imani yao

[Hisani]

Courtesy of United States Holocaust Memorial Museum

[Picha katika ukurasa wa 15]

Watoto kama vile Berthold Mewes walinyakuliwa kutoka kwa wazazi wao

[Picha katika ukurasa wa 15]

Video hii husimulia jinsi Mashahidi wa Yehova walivyoonyesha ujasiri katika Ujerumani ya Nazi

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kitambaa cha zambarau chenye pembe tatu kilishonwa kwenye mavazi ya wafungwa ili kuwatambulisha Mashahidi wa Yehova