Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Umoja wa Kikristo Unawataka Watu Wafanane?

Je, Umoja wa Kikristo Unawataka Watu Wafanane?

Maoni ya Biblia

Je, Umoja wa Kikristo Unawataka Watu Wafanane?

DINI imegawanyika sana siku hizi. Hata waumini wa kanisa moja wanaweza kuwa na imani tofauti-tofauti zenye kupingana kuhusiana na mafundisho na maadili. Mwandishi mmoja alisema hivi: “Ni vigumu hata kuwapata watu wawili wanaoamini Mungu yuleyule. Inaonekana kwamba siku hizi kila mtu anaamini mafundisho yake mwenyewe.”

Lakini kinyume kabisa, mtume Paulo aliwahimiza Wakristo wa karne ya kwanza huko Korintho ‘waseme kwa upatano’ na ‘waunganishwe kwa kufaa katika akili ileile na katika mstari uleule wa fikira.’ (1 Wakorintho 1:10) Watu fulani leo husema kwamba himizo hilo halifai. Wao husema kwamba watu hawafanani na hivyo haifai kusisitiza kwamba Wakristo wote wanapaswa kufikiri na kutenda kwa njia ileile. Lakini je, Paulo alikuwa anasema kwamba Wakristo wanapaswa kufanya mambo yanayofanana kabisa? Je, Biblia inaruhusu watu wafanye maamuzi yao wenyewe?

Ni Umoja, Si Kufanana

Kwenye barua yake nyingine, Paulo aliwasihi Wakristo wamtumikie Mungu kwa ‘nguvu zao za kufikiri.’ (Waroma 12:1) Bila shaka hakuwa na nia ya kuwafanya Wakristo Wakorintho wafikiri kwa njia ileile. Lakini kwa nini aliwaambia ‘waunganishwe kwa kufaa katika akili ileile na katika mstari uleule wa fikira’? Paulo alitoa shauri hilo kwa sababu kutaniko la Korintho lilikuwa na tatizo zito. Kulikuwa na migawanyiko. Watu fulani walimwona Apolo kuwa kiongozi wao huku wengine wakimpendelea Paulo ama Petro na wengine wakimpendelea Kristo. Hilo lilikuwa tatizo kubwa kwa sababu lilitishia amani ya kutaniko hilo.

Paulo aliwataka Wakorintho ‘washike umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani,’ kama alivyowahimiza Wakristo Waefeso baadaye. (Waefeso 4:3) Alikuwa akiwatia moyo akina ndugu wamfuate Yesu Kristo kwa umoja, badala ya kugawanyika katika vikundi mbalimbali, au mafarakano. Hilo lingewawezesha kupata amani na umoja wa kusudi. (Yohana 17:22) Kwa hiyo, shauri la Paulo lilikusudiwa kuwasaidia Wakorintho warekebishe kufikiri kwao na kudumisha amani, wala hakuwataka wafanane.—2 Wakorintho 13:9, 11.

Ni muhimu pia kuwa na umoja katika mafundisho. Wafuasi wa Yesu wanatambua kuwa kuna “imani moja” tu, kama kulivyo tu na “Mungu mmoja na Baba.” (Waefeso 4:1-6) Hivyo, Wakristo huhakikisha kwamba mambo wanayoamini yanapatana na kweli ambayo Mungu amefunua kupitia Neno lake kumhusu yeye na makusudi yake. Wanaamini mambo yaleyale kumhusu Mungu na matakwa yake. Pia wanaishi kupatana na viwango vya maadili ambavyo vimeonyeshwa waziwazi katika Neno la Mungu. (1 Wakorintho 6:9-11) Kwa njia hiyo, Wakristo huwa na umoja wa mafundisho na wa maadili.

Maoni Yanapotofautiana

Hiyo haimaanishi kwamba kila Mkristo hupewa maagizo ya jinsi ya kufikiri na kutenda katika mambo yote maishani. Katika mambo mengi kila mtu anapaswa kufanya uamuzi wake mwenyewe. Fikiria mfano mmoja. Wakristo kadhaa katika karne ya kwanza huko Korintho waliepuka kula nyama ambayo ilikuwa imetolewa dhabihu katika hekalu la sanamu. Baadhi yao waliamini kwamba kula nyama hiyo ni sawa na kuabudu sanamu, na wengine waliona kwamba haidhuru nyama ilitoka wapi. Ili kutatua suala hilo nyeti, Paulo hakutoa sheria ambayo ilionyesha jambo ambalo Wakristo walipaswa kufanya. Badala yake, alisema kwamba watu wangefanya maamuzi tofauti-tofauti kuhusu jambo hilo. *1 Wakorintho 8:4-13.

Leo huenda Wakristo wakafanya maamuzi yanayotofautiana na yale ya Wakristo wengine katika masuala ya kazi, afya, burudani, na mambo mengine yanayohusu mapendezi ya kibinafsi. Mapendezi hayo huenda yakawasumbua watu wengine. Huenda wakahofu kwamba tofauti hizo za maoni zinaweza kuleta migogoro na migawanyiko kutanikoni. Hata hivyo, maoni hayo hayawezi kuepukika. Kwa mfano, ingawa watungaji wa muziki wana idadi hususa ya noti za muziki ambazo wanaweza kutumia, wao hutunga muziki mtamu wa aina mbalimbali. Vivyo hivyo, Wakristo wanaweza kufanya maamuzi tofauti-tofauti bila kukiuka kanuni za Mungu. Hata hivyo, wana kiasi fulani cha uhuru wanapofanya maamuzi ya kibinafsi.

Je, inawezekana kudumisha umoja wa Kikristo huku tukiendelea kuheshimu uhuru wa kila mtu wa kufanya maamuzi? Jambo la maana ni kuonyeshana upendo. Upendo kwa Mungu hutusukuma tuzitii amri zake kwa hiari. (1 Yohana 5:3) Upendo kwa wenzetu hutusukuma tuheshimu haki zao za kufanya maamuzi yanayotegemea dhamiri katika mambo ya kibinafsi. (Waroma 14:3, 4; Wagalatia 5:13) Paulo aliweka mfano mzuri katika jambo hilo alipokubali mwongozo wa baraza linaloongoza la karne ya kwanza kuhusiana na suala lililohusu mafundisho. (Mathayo 24:45-47; Matendo 15:1, 2) Pia, aliwatia moyo wote waheshimu dhamiri za Wakristo wenzao katika mambo yanayohusu maamuzi ya kibinafsi.—1 Wakorintho 10:25-33.

Ni wazi kwamba hakuna mtu anayepaswa kulaumiwa kwa kufanya maamuzi yanayohusu dhamiri ikiwa hayapingani na kanuni za Biblia. (Yakobo 4:12) Kwa upande mwingine, Wakristo waaminifu hawapaswi kusisitiza kupata haki zao za kibinafsi huku wakiumiza dhamiri za wengine au kuharibu umoja wa kutaniko. Hawapaswi kamwe kufanya mambo ambayo yamelaumiwa waziwazi na Neno la Mungu. (Waroma 15:1; 2 Petro 2:1, 19) Upendo kwa Mungu unapaswa kutusukuma tupatanishe dhamiri zetu na maoni ya Mungu. Jambo hilo litatusaidia tudumishe umoja kati yetu na waamini wenzetu.—Waebrania 5:14.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Kwa mfano, huenda watu fulani ambao waliabudu sanamu kabla ya kuwa Wakristo hawakuona tofauti yoyote kati ya kula nyama na kuabudu. Sababu nyingine huenda ilikuwa kwamba Wakristo waliokuwa dhaifu wangewaelewa vibaya wale waliokula na wangekwazika.