Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Biblia Inavyoweza Kuwasaidia Wanaougua Kisukari

Jinsi Biblia Inavyoweza Kuwasaidia Wanaougua Kisukari

Jinsi Biblia Inavyoweza Kuwasaidia Wanaougua Kisukari

NI MUHIMU sana watu wanaougua ugonjwa wa kisukari wajidhibiti na kuwa na mtazamo unaofaa ili wadumishe afya bora. Lakini ili wasitawishe sifa hizo, wanahitaji kutegemezwa daima. Kwa hiyo haifai washiriki wa familia na marafiki kuwashawishi wale vyakula vinavyoweza kuwadhuru, labda wakisema, ‘Kula kidogo tu, hakitakudhuru.’ “Mke wangu hunitegemeza sana,” asema Harry, anayeugua ugonjwa wa moyo na ugonjwa wa kisukari wa Aina ya 2. “Hawezi kununua vyakula vinavyoweza kunidhuru. Lakini watu wengine hawaelewi, wala hawajui jinsi ilivyo vigumu kujizuia kula vyakula ambavyo vinatamanisha.”

Ikiwa wewe hushirikiana kwa ukawaida na mtu anayeugua ugonjwa wa kisukari, zingatia kanuni hizi mbili zinazopatikana katika Biblia: “Acheni kila mmoja afulize kutafuta sana, si faida yake mwenyewe, bali ya mtu yule mwingine,” na “Upendo . . . hautafuti masilahi yao wenyewe.”—1 Wakorintho 10:24; 13:4, 5.

Watu wote wanaojali afya yao wanapaswa kudhibiti ulaji wao, iwe wanaugua kisukari au la. Biblia inatoa msaada kuhusiana na hilo, kwani inaonyesha kwamba tunahitaji kusitawisha sifa ya kujidhibiti. Je, umeazimia kusitawisha sifa hiyo maishani mwako? (Wagalatia 5:22, 23) Pia, mifano ya watu wanaotajwa katika Biblia inaweza kukusaidia, kama vile mfano wa mtume Paulo. Mtu mmoja anayeugua ugonjwa wa kisukari anasema hivi: “Paulo alikuwa na mwiba wa kudumu katika mwili wake, lakini alimtumikia Mungu kwa uaminifu na kwa ukamili. Basi, mimi pia ninaweza!”

Naam, Paulo alizoea hali hiyo ambayo hangeweza kuibadili na akapata mafanikio mengi akiwa mishonari. (2 Wakorintho 12:7-9) Dustin, ambaye ana umri wa miaka 18, alizaliwa akiwa kipofu, naye amekuwa akiugua ugonjwa wa kisukari tangu alipokuwa na umri wa miaka 12. Anaandika hivi: “Ninajua kwamba hakuna mtu duniani aliye na maisha makamilifu. Ninatarajia wakati ambapo nitapona katika ulimwengu mpya wa Mungu. Ninaona ugonjwa huu kuwa wa muda tu. Huenda ugonjwa huu ukadumu kwa muda mrefu kuliko mafua au homa, lakini hatimaye utakwisha.”

Dustin alikuwa akizungumzia tumaini linaloonyeshwa katika Biblia la kuishi maisha makamilifu katika dunia paradiso kupitia Ufalme wa Mungu. (Ufunuo 21:3, 4) Neno la Mungu linaahidi kwamba chini ya utawala wa Mungu, “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” (Isaya 33:24; Mathayo 6:9, 10) Je, ungependa kujua mengi zaidi kuhusu ahadi hiyo inayoelezwa katika Biblia? Wasiliana na Mashahidi wa Yehova wa eneo lako, au uwaandikie wachapishaji wa gazeti hili ukitumia anwani ifaayo iliyoorodheshwa kwenye ukurasa wa 5.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Ni muhimu kujidhibiti na kuwa na mtazamo unaofaa