Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Matumaini Yoyote?

Je, Kuna Matumaini Yoyote?

Je, Kuna Matumaini Yoyote?

SHIRIKA la Afya Ulimwenguni na mashirika mengine yanafanya utafiti na kujaribu kuzuia magonjwa leo. Mashirika kadhaa yanasambaza habari na kufanya utafiti kuhusu dawa mpya na njia mpya za kuzuia magonjwa. Jitihada hizo zinafanywa ili kukabiliana na tatizo hilo linalozidi kuwa sugu. Watu mmoja-mmoja na jamii zinaweza kujifunza kuhusu magonjwa hayo na kujikinga. Lakini, kuna tofauti kati ya kuwalinda watu mmoja-mmoja na kuyakomesha ulimwenguni kote.

Wataalamu wengi wanaamini kwamba watu wote wanapaswa kushirikiana na kutumainiana ili jitihada za kuzuia magonjwa ziweze kufaulu. Laurie Garrett, mwandishi wa habari na mshindi wa Tuzo ya Pulitzer, aliandika hivi katika kitabu chake The Coming Plague—Newly Emerging Diseases in a World out of Balance: “Utandawazi unawataka wanadamu kila mahali duniani waone kwamba wana mazingira mengine zaidi ya ujirani wao, mikoa yao, nchi zao, au maeneo yao. Viini na wadudu wanaovieneza hawatambui mipaka iliyowekwa na wanadamu.” Mlipuko wa ugonjwa huhangaisha watu duniani pote, bali si watu wa nchi moja tu.

Serikali na jamii fulani hushuku msaada wa aina yoyote ile unaotoka nje, hata kama unasaidia kuzuia magonjwa. Isitoshe, mara nyingi pupa ya kibiashara na kutopangia vizuri kwa ajili ya wakati ujao huharibu jitihada za kimataifa. Je, mwanadamu atashindwa kuzuia viini vya magonjwa? Mwandishi Eugene Linden, anayefikiri kuwa mwanadamu atashindwa, anasema hivi: “Tuna muda mfupi tu wa kubadili hali hiyo.”

Sababu ya Kuwa na Tumaini

Sayansi na tekinolojia hazijaweza kukomesha magonjwa yanayoenezwa na wadudu. Na, bila shaka, kuna magonjwa mengine mengi yanayohatarisha afya. Hata hivyo, kuna sababu ya kuwa na tumaini. Ingawa wanasayansi wameanza kuelewa ushirikiano tata ulioko kati ya viumbe hivi majuzi tu, wanatambua uwezo wa dunia wa kujifanya upya. Sayari yetu inaweza kujifanya upya na kurudia hali yake ya kawaida. Kwa mfano, misitu hukua tena inapokatwa na ushirikiano kati ya viini, wadudu, na wanyama huanza baada ya muda fulani.

La muhimu zaidi, ubuni tata wa viumbe huonyesha kuna Muumba, Mungu aliyeanzisha mifumo ya dunia. Wanasayansi wengi wanakubali kwamba kuna mtu fulani mwenye akili aliyeiumba dunia. Naam, watu wenye kufikiri hawawezi kukataa kwamba Mungu yuko. Biblia inasema kwamba Muumba, Yehova Mungu, ni Mweza-Yote na mwenye upendo. Anataka sana tuwe na furaha.

Biblia pia inasema kwamba mwanadamu wa kwanza alifanya dhambi kwa kukusudia, hivyo wanadamu wamerithi kutokamilika, ugonjwa, na kifo. Je, hiyo inamaanisha kwamba tutaendelea kuteseka daima? La! Kusudi la Mungu ni kufanya dunia hii iwe paradiso, ambapo wanadamu wataishi kwa amani na viumbe wengine wakubwa kwa wadogo. Biblia inatabiri kuhusu ulimwengu ambao hautakuwa na kiumbe yeyote atakayemdhuru mwanadamu, awe mnyama mkubwa au mdudu mdogo sana.—Isaya 11:6-9.

Hapana shaka kwamba wanadamu watakuwa na wajibu fulani katika kuleta mabadiliko hayo ya kijamii na ya kimazingira. Mungu alimpa mwanadamu wajibu wa “kuitunza” dunia. (Mwanzo 2:15) Katika paradiso ijayo, wanadamu watatekeleza wajibu huo kwa ukamili wakifuata maagizo kutoka kwa Muumba mwenyewe. Hivyo, tunaweza kutazamia wakati ambapo “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24.