Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Familia za Mzazi Mmoja Nimekosa maneno ya kueleza jinsi nilivyofurahia kusoma mfululizo wa makala wenye kichwa “Familia za Mzazi Mmoja Zinaweza Kufaulu.” (Oktoba 8, 2002) Mimi husoma gazeti hilo tena na tena! Nina watoto wawili lakini sina mwenzi wa ndoa. Kila mara ninaposoma makala hizo, mimi hujitia moyo kwamba ninaweza kufaulu na kwamba siko peke yangu. Asanteni sana!

C. B., Marekani

Mume wangu alinitaliki. Maisha yalikuwa magumu sana nilipoachwa na watoto wawili. Ninamshukuru Yehova kwa kutusikia tunapomwomba msaada na kutujibu kwa makala zenye kufariji kama hizo. Hivyo, yeye hutuhakikishia kwamba anatujali na anatupenda.

L. T., Jamhuri ya Cheki

Asanteni sana kwa makala hizo. Nilikuwa nimeanza kulemewa na hali ninayokabili sasa ya kutokuwa na mwenzi wa ndoa na kulazimika kurudi kufanya kazi baada ya kuwa mke nyumbani kwa miaka mingi. Hata hivyo, makala hizo zilinipa tumaini na zilinitia moyo kuendelea kuvumilia. Ninapanga kutumia madokezo hayo, kama yale yaliyosema kuhusu kuwa mwenye utaratibu na kujifunza Biblia kwa ukawaida pamoja na familia yangu. Nitaweka gazeti hilo karibu na nitalisoma kila wakati ninapoanza kuhisi kwamba nimelemewa.

B. A., Marekani

Nina mwana mmoja na binti mmoja na nilianza kuwalea nikiwa peke yangu miaka 14 iliyopita. Ninawashukuru kwa jitihada mnazofanya kutayarisha vitabu na magazeti yenu, lakini sehemu fulani za makala hizo zilinivunja moyo. Kwa mfano, neno “kufaulu” lilitumiwa mara nyingi. Ninaona kwamba nimetumia yale madokezo yaliyo kwenye ukurasa wa 11, lakini sijafaulu sana kama yule mzazi anayeonyeshwa kwenye ukurasa huo. Jamani, mzazi aliyefanikiwa si yule tu ambaye amemsaidia mtoto wake kuwa mhubiri wa wakati wote au mishonari.

M. S., Japan

“Amkeni!” linajibu: Tunatambua kwamba mafanikio yanapimwa kwa njia nyingi. Tulikusudia kutoa madokezo yatakayowasaidia wazazi wasio na wenzi kukabiliana na magumu maishani na kuwatia moyo kwamba jitihada zao si za bure. Tulitumia mifano ya vijana walio katika utumishi wa wakati wote ili kuonyesha kwamba wazazi wasio na wenzi wamefanikiwa kulea watoto wanaomwogopa Mungu. Ni matumaini yetu kwamba wazazi wote—iwe wana wenzi au hawana wenzi—wataendelea kuwapa watoto wao mahitaji yao ya kiroho, ya kihisia, na ya kimwili.

Njaa Huko Ireland Asanteni kwa makala yenye kuelimisha yenye kichwa “Njaa Kuu ya Ireland Iliyosababisha Vifo na Uhamaji Usio na Kifani.” (Oktoba 8, 2002) Wakati wa njaa hiyo, watu wengi walihama Ireland na kuja Kanada kwa meli. Wengi walikufa kutokana na kipindupindu, ugonjwa unaosababishwa na chawa, na magonjwa mengine. Watoto wengi waliachwa mayatima, na wengine walichukuliwa na familia zilizozungumza Kifaransa na wakapewa majina ya Kifaransa. Hivyo, baada ya muda, watu wengi wakapoteza utamaduni wao wa Ireland.

K. S., Kanada

Vijana Huuliza Ninataka kutoa maelezo kuhusu makala “Vijana Huuliza . . . Mbona Mzazi Wangu Hanipendi?” (Septemba 22, 2002) Nilishuka moyo sana wakati wazazi wangu walipotalikiana. Nyakati nyingine, nilidhani kwamba hakuna mtu ambaye angenisaidia. Ninampenda mama yangu na ndugu yangu sana, lakini nyakati nyingine mimi huona kuna pengo maishani mwangu—pengo ambalo baba yangu aliacha. Nilimwomba Yehova anipe kitu cha kunifariji. Na makala hiyo ilinifariji sana. Ilinisaidia niwe na maoni mazuri, na nikajifunza jinsi ya kukabiliana na hali hiyo. Andiko la Zaburi 27:10 ndilo lililonitia moyo sana. Lilinisaidia kutambua kwamba Yehova ananipenda hata wakati ambapo inaonekana kwamba hakuna mtu anayejali.

D. B., Marekani