Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuutazama Ulimwengu

Kuutazama Ulimwengu

Kuutazama Ulimwengu

Je, Wamepata Matokeo Bora Kazini?

Gazeti Vancouver Sun linaripoti hivi: “Miaka kumi iliyopita ni asilimia 10 tu ya Wakanada waliokuwa wakifanya kazi kwa zaidi ya saa 50 kila juma, lakini siku hizi asilimia 25 ndio wanaofanya kazi kwa zaidi ya saa 50 kila juma.” Katika uchunguzi mmoja wa kiserikali uliochunguza Wakanada 31,500 wanaofanya kazi, “nusu ya wale waliohojiwa walisema kwamba wao huenda kazini mwishoni mwa juma au wanafanyia kazi nyumbani. Hivyo wanafanya kazi ya ziada kwa saa 27 kila mwezi.” Jambo moja linalochangia hali hiyo ni tekinolojia. Gazeti hilo lilisema hivi: “Uchunguzi huo ulionyesha kwamba watu wote wanaofanya kazi ya ziada nyumbani bila kulipwa . . . ‘hutumia kompyuta.’” Kwa hiyo, badala ya kuwawezesha watu kufanya kazi kwa siku nne kwa juma na kupata wakati mwingi wa kupumzika, “tekinolojia hasa ndiyo imeongeza mfadhaiko, magonjwa, uchovu, visa vya kukosa kwenda kazi, na mambo mengine yanayozuia watu wasiwe na matokeo mazuri kazini.” Gazeti hilo linaongeza hivi: “Watu wengi waliohojiwa walisema kwamba tekinolojia imewasaidia wapende kazi yao zaidi na kuboresha matokeo yao kazini. Hata hivyo, hakuna mtu aliyesema kwamba tekinolojia imempunguzia kazi wala kupunguza mfadhaiko kazini.”

Uchafuzi Katika Majiji Makubwa

Gazeti El Universal la Mexico City linaripoti kwamba “Mexico City, Caracas, Bogotá, na Havana ni baadhi ya majiji machafu zaidi ulimwenguni.” Huo ndio mkataa uliofikiwa baada ya uchunguzi kufanywa na Shirika la Mercer Human Resource Consulting Society na kuchapishwa huko London. Uchunguzi huo, ambao ulichunguza jinsi majiji ulimwenguni pote yanavyoathiriwa na uchafuzi, ulikazia hasa usafi wa hewa, uzoaji wa takataka, usalama, makao, elimu, usafiri, na huduma za umma. Zurich na Vienna ndiyo majiji ya hali ya juu zaidi huko Ulaya. Calgary na Honolulu ndiyo majiji safi zaidi ulimwenguni. Kulingana na ripoti hiyo, jiji la San Juan, Puerto Rico ndilo safi zaidi kati ya majiji yote ya Amerika Kusini.

Madhara ya Kuvunjika kwa Ndoa

Baada ya kuchanganua matokeo ya miradi 100 ya uchunguzi iliyofanywa kwa zaidi ya miaka 20, Rebecca O’Neill, mkurugenzi wa mradi wa Shirika la Civitas la Uchunguzi wa Familia, aliripoti kwamba “akina mama, akina baba, na watoto wengi kutoka ‘familia zisizo na baba’ hukabili umaskini, maumivu ya kihisia, magonjwa, na kwamba wanakosa fursa za kujiendeleza maishani, na familia hizo haziwi imara.” Kulingana na O’Neill, “watoto ambao wazazi wao wametengana wanaelekea kupata matatizo ya afya kwa kiwango cha asilimia 50 zaidi, na uwezekano wao wa kutoroka nyumbani ni mara mbili zaidi, hali uwezekano wao wa kuumizwa au kutendewa vibaya kingono ni mara tano zaidi,” laripoti gazeti The Sunday Telegraph la London. Gazeti hilo linaongeza hivi: “Watoto wasio na baba wanaelekea kutopatana na watu vizuri na kupata matatizo shuleni mara tatu zaidi ya watoto wengine. Kuna uwezekano maradufu kwamba watoto hao wanapobalehe watakuwa walevi, watavuta sigara, watatumia dawa za kulevya, . . . watakuwa wahalifu, na watafanya ngono wakiwa na umri mdogo na kupata watoto.” Kulingana na ripoti hiyo, ijapokuwa familia zenye wazazi wote wawili zinaweza kuwa maskini, watoto wao hawatakabili sana matatizo hayo.

Kujiua Ndicho Kisababishi Kikuu cha Vifo vya Kijeuri

Gazeti la London The Independent linasema kwamba “kujiua ndicho kisababishi kikuu cha vifo vya kijeuri ulimwenguni pote.” Makala hiyo, ambayo ilitegemea ripoti moja ya Shirika la Afya Ulimwenguni, pia inasema kwamba mnamo mwaka wa 2000 watu milioni 1.6 walikufa kutokana na jeuri. Watu 815,000 walijiua mwaka huo, watu 520,000 waliuawa, na watu 310,000 walikufa kwa sababu ya vita. Gazeti hilo linasema kwamba wengi wa watu hao waliokufa katika mwaka wa 2000 “walitoka katika nchi zinazoendelea na chini ya asilimia 10 ya watu waliokufa ni wa nchi zilizoendelea.” Idadi ya watu waliojiua katika nchi za Belarus, Estonia, na Lithuania ni mara nne zaidi ya idadi ya waliojiua huko Uingereza. Idadi ya watu wanaouawa Afrika, Amerika Kaskazini na Kusini inazidi kwa mara mbili idadi ya watu wanaojiua. Lakini huko Australia, Ulaya, na Mashariki ya Mbali, idadi ya wanaojiua ni mara mbili zaidi ya watu wanaouawa.

Watoto Wasiolala vya Kutosha

Gazeti U.S.News & World Report linasema kwamba watoto wanaathiriwa sana kwa sababu ya kutolala vya kutosha. Watoto wasiolala vya kutosha hawafanikiwi shuleni na hushindwa kupata marafiki. Gazeti hilo linaripoti hivi: “Mara nyingi watoto wasiolala vya kutosha hushindwa kukaza fikira kwa muda mrefu, hukasirika haraka, hawatulii, na hawana subira.” Madaktari wanasema kwamba mara nyingi wazazi huchangia matatizo hayo. Barbara Braun-McDonald, ambaye ni daktari wa magonjwa ya akili na ya kihisia ya watoto, anasema hivi: “Ikiwa unawakawiza watoto wako hadi saa 5:00 usiku, unahitaji kurekebisha jambo hilo.” Wazazi wanatiwa moyo kuwawekea watoto wao wakati hususa wa kulala na wa kuamka kila siku, hata mwishoni mwa juma, ili kuwasaidia kulala vya kutosha. Madokezo mengine yanatia ndani kufanya mambo kwa ukawaida kabla ya kulala kama vile kuoga, kumpakata mtoto mdogo au kumsomea hadithi, na kutowaruhusu watazame televisheni au watumie kompyuta saa moja kabla hawajalala.

“Michezo, Vitafuno, na Damu”

Gazeti IHT Asahi Shimbun linaripoti kwamba vijana Wajapani wamekuwa wakienda kupata huduma za bure kwenye “majumba yanayoonyesha video, yenye michezo ya kompyuta, vitafuno, na watu wanaokanda miguu. Vijana hao hutakikana wafanye jambo moja tu. Wao hupaswa kuchanga damu yao.” Majumba hayo ni vituo vya kuchangisha damu vinavyoendeshwa na Shirika la Msalaba Mwekundu la Japan. “Watu huchanga damu wakiwa wamestarehe,” lasema gazeti hilo. “Baadaye vijana wengi hubaki katika majumba hayo wakifurahia maandazi, maji ya matunda na michezo ya kompyuta. Jambo jingine linalowavutia kwenye majumba hayo ni ubashiri unaotolewa bure ambao hufanywa mara kadhaa kila juma.” Pia wanajifunza jinsi ya kujipamba, wanakandwa mwili, wanatazama sarakasi, na wanapata fursa ya kununua vitu. Kwa kuwa idadi ya watu wanaochanga damu imepungua sana, Shirika la Msalaba Mwekundu limebadili sura ya vituo vyake kotekote nchini. Gazeti hilo linasema kwamba ijapokuwa hapo awali vituo hivyo “havikupendwa na viliogopesha,” sasa “vinapendwa sana na vijana wa umri mbalimbali.”

Meli za Starehe na Uchafuzi

Gazeti The Sunday Times la London linaripoti kwamba “meli za starehe zinazowapeleka mamilioni ya abiria kila mwaka kwenye sehemu zenye kupendeza zaidi ulimwenguni zinahatarisha viumbe wa baharini kutokana na uchafuzi.” Kila siku, meli moja kubwa inayobeba watu 4,000 hivi, kutia ndani abiria na mabaharia, humwaga makumi ya maelfu ya lita za maji machafu, takataka, na maji ambayo watu wametumia kuogea na kufulia nguo. Isitoshe, meli hiyo humwaga lita 56 hivi za kemikali zenye sumu na tani saba za takataka. Watalii wanaotembelea sehemu mbalimbali kwa meli husababisha uchafuzi mwingi sana kuliko wale wasiotumia meli. Mnamo mwaka wa 2000, meli za starehe 240 hivi ziliwapeleka watu milioni kumi kwenye maeneo yanayohitaji kutunzwa sana, kama vile Ghuba ya Barafu ya Alaska, matumbawe na visiwa vya Karibea, pwani za Mediterania, na hata kwenye Ncha ya Kusini. Inasemekana kwamba meli 50 zitaongezwa kufikia mwaka wa 2005. Roger Rufe, wa Shirika la Kuhifadhi Mazingira Baharini, anasema: “Watu wengi zaidi wanapenda kusafiri kwa meli hizo za starehe, lakini meli hizo ni kama majiji yasiyokuwa na sheria za kudhibiti utupaji wa takataka.”

Sanamu za Papa Hazinunuliwi Sana

Kwa miaka mingi, “watu walipata pesa nyingi kwa kuuza bidhaa za kidini [huko Poland],” laripoti gazeti Newsweek la Poland. Hata hivyo, wauzaji wa sanamu hizo takatifu wamekabili “tatizo kubwa.” Ijapokuwa ziara ya papa nchini Poland mwaka wa 2002 ilitangazwa sana, watu wengi hawakununua bidhaa za kidini kama vile mikufu na michoro. Gazeti hilo linasema kwamba “wauzaji walikuwa na mamilioni ya bidhaa kama vile sanamu mbalimbali, mikeka, na michoro” ya papa lakini “wanunuzi hawakuvipenda.” Hata hivyo, kuna bidhaa moja ya kidini inayozidi kupendwa. Ni kadi ya plastiki ambayo kwenye upande mmoja ina “sanamu takatifu” na kwenye upande ule mwingine ina “shanga za rangi ya dhahabu zilizoyeyushwa katika plastiki yenyewe.” Gazeti Wprost la Poland linasema kwamba “kadi hizo za rosari” ndizo bidhaa za kidini “zinazopendwa zaidi na za karibuni zaidi.”