Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unawezaje Kukabiliana na Magumu ya Kuwa na Wazazi Walezi?

Unawezaje Kukabiliana na Magumu ya Kuwa na Wazazi Walezi?

Vijana Huuliza . . .

Unawezaje Kukabiliana na Magumu ya Kuwa na Wazazi Walezi?

“Sijui lolote kuhusu wazazi wangu, na hilo hunihangaisha sana.”—Barbara, mwenye umri wa miaka 16.

“Sijui nilikozaliwa au wazazi wangu ni akina nani. Wakati mwingine mimi huwaza kuhusu jambo hilo wakati ninapolala.”—Matt, mwenye umri wa miaka 9.

“Ninapobishana na wazazi wangu, mimi huwazia kuwa wazazi wangu ‘halisi’ wangenielewa zaidi. Ninajua kwamba sipaswi kuwa na maoni hayo, na sijawaambia wazazi wangu kuhusu hilo.”—Quintana, mwenye umri wa miaka 16.

HAPANA shaka kwamba watoto wenye wazazi walezi wana matatizo mbalimbali. Vijana wengi huwa na maoni kama yale ambayo yametajwa hapa juu. Wengi hujiuliza ikiwa inafaa wawatafute wazazi wao waliowazaa, au huwazia kwamba maisha yao yangekuwa bora iwapo wangeishi nao. Na hayo si magumu pekee wanayopata.

Makala iliyotangulia katika mfululizo huu ilizungumzia mtazamo usiofaa wa vijana wenye wazazi walezi. * Ni muhimu vijana hao washinde maoni hayo yasiyofaa ili wapate furaha. Ni yapi baadhi ya magumu mengine ambayo huenda yakawapata vijana hao, nao wanaweza kufanya nini ili wakabiliane nayo?

Je, Mzazi Wako Ni Yule Aliyekuzaa Tu?

Jake mwenye umri wa miaka 13 asema kwamba sikuzote alimfikiria mama yake mzazi. Jambo hilo lilimfanya akosane na wazazi wake walezi. Anakumbuka hivi: “Nilipokasirika ningemwambia, ‘La, huwezi kuniadhibu hivyo, wewe si mama yangu halisi!’”

Ni wazi kwamba Jake alihitaji kujiuliza swali hili muhimu: Mama yake “halisi” ni nani? Iwapo una wazazi walezi, huenda unajiuliza swali hilo pia, hasa ikiwa unawazia kwamba wazazi wako wangekutendea vizuri kuliko walezi wako. Lakini je, kuzaa tu ndiko kunamfanya mtu awe mzazi “halisi”?

Mama mlezi wa Jake hakukubaliana na jambo hilo. Jake asema: “Mama yangu alisema, ‘Naam, mimi ni mama yako halisi. Hata ingawa una mama aliyekuzaa, mimi ndiye mama yako halisi sasa.’” Watu wanapomchukua mtoto nyumbani mwao na kukubali kumwandalia makao, chakula, malezi, na kumtimizia mahitaji yake, kwa hakika wanakuwa wazazi wake “halisi.” (1 Timotheo 5:8) Huenda hata sheria ya nchi yenu inasema hivyo. Vipi machoni pa Mungu?

Fikiria kisa maarufu zaidi cha mtoto mwenye wazazi walezi, yaani Yesu Kristo. Ingawa Yusufu yule seremala hakuwa baba mzazi wa Yesu, alimkubali awe mtoto wake. (Mathayo 1:24, 25) Je, Yesu aliasi mamlaka ya Yusufu alipokuwa mkubwa? La. Badala yake Yesu alitambua kwamba yalikuwa mapenzi ya Mungu amtii baba yake mlezi. Yesu alijua sheria ambayo Yehova alikuwa amewapatia watoto Waisraeli. Ilikuwa sheria gani?

Waheshimu Baba na Mama Yako

Maandiko huwaambia hivi vijana: “Waheshimu mama yako na baba yako.” (Kumbukumbu la Torati 5:16) Neno ‘kuheshimu’ hutumiwa katika Biblia mara nyingi kuonyesha staha, kuthamini, na kujali. Unaweza kuwaheshimu walezi wako kwa kuwaonyesha fadhili, kustahi hadhi yao, kuwasikiliza, na kuwa tayari kufanya mambo yanayofaa ambayo wanakuomba ufanye.

Namna gani ikiwa wanataka ufanye mambo yasiyofaa? Huenda wakafanya hivyo. Wazazi wote hawajakamilika, wawe walezi au la. Hilo laweza kufanya iwe vigumu sana kwako kutii. Wakati mwingine, unaweza kuwazia kwamba hupaswi kutii kwa sababu wao ni walezi tu. Lakini ndivyo ilivyo kweli?

Huenda ikasaidia kumfikiria Yesu. Kumbuka kwamba yeye alikuwa mtu mkamilifu. (Waebrania 4:15; 1 Petro 2:22) Lakini baba yake mlezi wala mama yake mzazi hakuwa mkamilifu. Basi, huenda kuna nyakati ambapo alijua wazazi wake wamekosea. Je, aliasi ukichwa wa Yusufu asiyekamilika au mwongozo wa Maria wenye kosa? La. Biblia husema kwamba Yesu aliendelea kukua, “naye akaendelea kujitiisha” kwa wazazi wake.—Luka 2:51.

Huenda ukahisi kwamba wazazi wako wamekosea wakati kutoelewana kunapotokea. Hata hivyo, ni lazima ukubali kwamba hata wewe hujakamilika. Kwa hiyo, inawezekana kwamba ni wewe umekosea. Vyovyote vile, je, si ni vema kufuata mfano wa Yesu? (1 Petro 2:21) Hiyo itakusaidia kutii. Lakini kuna sababu nyingine inayopaswa kukusukuma uwatii wazazi wako.

Biblia inasema: “Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika kila jambo, kwa maana hilo linapendeza vema katika Bwana.” (Wakolosai 3:20) Naam, Baba yako wa mbinguni hufurahi unapotii. (Mithali 27:11) Pia yeye anataka ujifunze kutii kwa kuwa anataka uwe mwenye furaha pia. Neno lake huwatia moyo vijana watii, ‘ili ipate kuwa vema kwao na wapate kudumu muda mrefu juu ya dunia.’—Waefeso 6:3.

Imarisha Uhusiano Wako na Walezi Wako

Kuwa na uhusiano mzuri pamoja na walezi wako kunatia ndani mengi zaidi ya kuwaheshimu na kuwatii. Yaelekea unataka familia yenu iwe na uchangamfu na upendo. Walezi wako wana daraka la kudumisha hali hiyo. Lakini unaweza kufanya jambo fulani pia. Jambo lipi?

Kwanza, tafuta njia za kuimarisha uhusiano wako pamoja na wazazi wako. Waombe wakueleze kuhusu maisha yao ya zamani, ya sasa, na kuhusu mapendezi yao. Waombe ushauri kuhusu baadhi ya matatizo unayokabili, wakati ambapo wametulia na wanaweza kukusikiliza. (Mithali 20:5) Pili, fikiria jinsi unavyoweza kuwasaidia, labda kwa kufanya kazi za nyumbani hata kabla hujaombwa ufanye hivyo.

Vipi kuhusu wazazi wako waliokuzaa? Ukiamua kuwatafuta au wakiamua kukutafuta, je, hilo litaathiri uhusiano wako na walezi wako? Zamani, mashirika yaliyoshughulikia utunzaji wa watoto yalikataa kutoa habari ambazo zingewasaidia wazazi kuwapata watoto wao au kutoa habari hizo kwa watoto waliotafuta wazazi wao. Leo, sheria za nchi fulani zinaruhusu habari hizo zitolewe, na watoto wengi wameonana na wazazi wao ambao hawawakumbuki hata kidogo. Bila shaka, sheria za kwenu huenda zikawa tofauti.

Vyovyote vile, ni daraka lako kuamua kutafuta wazazi wako au kutowatafuta. Huenda isiwe rahisi kufanya hivyo. Vijana wenye wazazi walezi wana maoni tofauti-tofauti kuhusu jambo hilo. Wengine hutamani kuwatafuta wazazi wao na wengine wameazimia kutowatafuta. Hata hivyo, vijana wengi wameonana na wazazi wao bila kuharibu uhusiano wao mzuri na walezi wao.

Tafuta ushauri kutoka kwa walezi wako na marafiki wengine wakomavu katika kutaniko la Kikristo. (Mithali 15:22) Fikiria jambo hilo vizuri kabla ya kufanya uamuzi. Kama andiko la Mithali 14:15 linavyosema, “Mwenye busara huangalia sana aendavyo.”

Ukiamua kuanzisha uhusiano na wazazi wako, jitahidi kuwahakikishia walezi wako kwamba bado unawapenda na kuwastahi. Hivyo, pole kwa pole unapokuja kuwafahamu wale waliokuzaa, utaendelea kudumisha uhusiano mzuri na wale ambao walikulea na kukuzoeza.

Imarisha Uhusiano Wako na Baba Yako wa Mbinguni

Vijana wengi wenye wazazi walezi huogopa kuachwa. Wao huwa na wasiwasi kwamba huenda wakapoteza familia iliyowalea jinsi walivyopoteza wazazi wao. Woga huo unaeleweka. Lakini, kumbuka maneno haya yenye hekima: “Hakuna hofu katika upendo, lakini upendo mkamilifu hutupa hofu nje.” (1 Yohana 4:18) Usiruhusu hofu ya kuwapoteza wapendwa wako ikutawale. Badala yake, imarisha upendo wako kwa wengine, kutia ndani washiriki wa familia yenu. La muhimu zaidi, imarisha upendo wako kwa Baba yako wa mbinguni, Yehova Mungu. Yeye anategemeka kabisa na hawezi kuwaacha watoto wake waaminifu. Atamaliza hofu yako.—Wafilipi 4:6, 7.

Catrina, aliyeanza kutunzwa na wazazi walezi tangu utoto, anasema kwamba kusoma Biblia kumemsaidia sana aimarishe uhusiano wake na Mungu na kuishi maisha yenye furaha na yenye kusudi. Asema kwamba kuwa na uhusiano mzuri na Yehova “ni muhimu sana kwa sababu Baba yetu wa mbinguni anajua hisia zetu.” Catrina anapenda sana maneno ya Zaburi 27:10 yanayosema: “Baba yangu na mama yangu wameniacha, bali BWANA atanikaribisha kwake.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona makala “Kwa Nini Nina Wazazi Walezi?” katika toleo la Aprili 22, 2003 la Amkeni!

[Picha katika ukurasa wa 20]

Tafuta njia za kuboresha uhusiano wako na walezi wako