Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Maadili Yanabadilika?

Kwa Nini Maadili Yanabadilika?

Kwa Nini Maadili Yanabadilika?

“Ni jambo gani lililo muhimu zaidi maishani?”

Watu 50,000 katika nchi 60 waliulizwa swali hilo. Matokeo ya kura ya maoni ya Gallup yalionyesha kwamba jibu lililotolewa na watu wengi zaidi kutoka kila sehemu ya ulimwengu lilikuwa “kuwa na maisha ya familia yenye furaha” na “kuwa na afya bora.”

UKIANGALIA kijuu-juu tu, utadhani kwamba watu ulimwenguni pote wana maadili mema. Hata hivyo, mambo ni tofauti kabisa. Zamani watu walikuwa na maadili yaliyotegemea kanuni za dini na adabu za kale. Lakini hali inabadilika haraka sana. Mtafiti Marisa Ferrari Occhionero anasema hivi kuhusu nchi ya Italia: “Vijana wana tabia ambazo zinaonyesha kwamba wamesahau maadili ya kale ya wazazi wao, ya kidini na kitamaduni.” Hali iko hivyo pia kwa watu ulimwenguni pote, vijana kwa wazee.

Profesa Ronald Inglehart, msimamizi wa utafiti unaoitwa Uchunguzi wa Maadili Ulimwenguni anasema hivi: “Kuna uthibitisho mkubwa kwamba maoni ya watu yamebadilika sana.” Ni nini kinacholeta mabadiliko hayo? Inglehart asema: “Mabadiliko hayo yanaletwa na maendeleo ya kiuchumi na kitekinolojia.”

Kwa mfano, kura ya maoni ya Gallup, ilifichua kwamba katika nchi tajiri kuajiriwa kazi kulichukua “nafasi ya chini sana” katika mambo yanayoonwa kuwa muhimu maishani. Lakini kupata kazi kulionwa kuwa jambo muhimu zaidi katika nchi zinazoendelea. Hii yaonyesha kwamba watu maskini wanaona kupata mahitaji ya kila siku kuwa jambo muhimu zaidi. Nchi zinapoendelea kiuchumi, watu huanza kutilia maanani mambo kama vile afya, furaha ya familia, na uhuru wa kusema.

Kwa sababu ya maendeleo ya kitekinolojia, watu katika nchi zinazoendelea wataathiriwa na maadili mapya. Gazeti The Futurist linasema hivi: “Imani na maadili yetu huathiriwa na yale tunayoona na kusikia.” Hivyo, vyombo vya habari vinaathiri sana maadili ya nchi za Magharibi. Gazeti The Futurist linasema: “Vyombo vya habari vinaathiri watu ulimwenguni pote.”

Ni mabadiliko gani ambayo yametokea katika mitazamo na tabia za watu? Mabadiliko hayo yamekuwa na athari gani kwako na kwa familia yako?