Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mamilioni Watahudhuria Je, Wewe Utakuwapo?

Mamilioni Watahudhuria Je, Wewe Utakuwapo?

Mamilioni Watahudhuria Je, Wewe Utakuwapo?

▪ WAPI? Kwenye mojawapo ya Makusanyiko ya Wilaya ya “Mtukuzeni Mungu” yatakayofanywa katika sehemu nyingi ulimwenguni pote. Programu hiyo ya siku tatu iliyopangwa na Mashahidi wa Yehova imetayarishwa kuwasaidia wote wanaompenda Mungu kumpa Muumba wao utukufu anaostahili maishani mwao.

Siku ya kwanza ya kusanyiko hilo itakazia kichwa hiki, “Wewe Wastahili, Yehova, . . . Kupokea Utukufu.” (Ufunuo 4:11) Hotuba yenye kichwa “Uumbaji Unatangaza Utukufu wa Mungu” itatusaidia kuona jinsi sifa za Yehova “zaonwa waziwazi,” au “zafahamiwa kwa vitu vilivyofanywa.” (Waroma 1:20) Hotuba ya msingi yenye kutia moyo, “Tunachochewa na Maono ya Utukufu ya Kiunabii,” itatuhimiza sote kukumbuka matukio muhimu yaliyotabiriwa katika Neno la Mungu kuhusu siku zetu. “Unabii wa Amosi—Ujumbe Wake kwa Ajili ya Siku Zetu” ndicho kichwa cha mfululizo wenye sehemu tatu ambao utakazia jinsi maonyo ya nabii huyo wa kale yanavyotuhusu leo. Hotuba “‘Nchi Nzuri’—Kuona Paradiso Kimbele” itatusaidia tuthamini zaidi nchi ambayo Yehova aliwapa watu wake wa kale.

Siku ya pili ya kusanyiko itakuwa na kichwa “Wahubirini Mataifa Habari za Utukufu Wake,” kinachotegemea Zaburi 96:3. Mambo makuu yatatia ndani mfululizo wenye kichwa “Tutoe Kama Vioo Mrudisho wa Utukufu wa Yehova.” Mfululizo huo wenye sehemu tatu utaonyesha jinsi tunavyoweza kutimiza huduma yetu kwa matokeo zaidi. Hotuba yenye kichwa “Wanaochukiwa Bila Sababu” itafuatwa na hotuba ya wakfu na baadaye ubatizo, ambalo ni jambo la kawaida katika kila kusanyiko la Mashahidi wa Yehova. Alasiri kutakuwa na hotuba yenye kichwa, “Jihadhari na ‘Sauti ya Wageni’” ambayo itatoa mashauri mazuri kuhusu “walimu wasio wa kweli” ambao hujaribu kuwadanganya watu wa Mungu kwa “maneno bandia.” (2 Petro 2:1, 3) Programu ya siku hiyo itamalizika kwa hotuba yenye kichwa, “Watoto Wetu—Urithi Wenye Thamani.” Wazazi na watoto watafurahia hotuba hiyo.

Siku ya mwisho ya kusanyiko hilo itakuwa na kichwa “Fanyeni Mambo Yote kwa Utukufu wa Mungu.” (1 Wakorintho 10:31) Hotuba yenye kichwa, “Jinsi Vijana Wanavyomsifu Yehova” itakuwa pia na mahojiano. Kipindi cha asubuhi kitakuwa pia na drama ya dakika 45 yenye kichwa “Kuhubiri kwa Ujasiri Licha ya Upinzani.” Kwa kuwa dini hutajwa sana katika vyombo vya habari, hotuba ya watu wote itazungumzia swali, “Ni Nani Wanaomtukuza Mungu Leo?” Hotuba yenye kichwa “‘Fulizeni Kuzaa Matunda Mengi’ kwa Utukufu wa Mungu,” itatamatisha vyema kusanyiko hilo.

Hizo tu ni baadhi ya hotuba zenye kuchochea zitakazotolewa kwenye Kusanyiko la Wilaya la Mashahidi wa Yehova la “Mtukuzeni Mungu.” Jitahidi kuhudhuria siku zote tatu. Ili ujue mahali ambapo kusanyiko litafanywa katika eneo lenu, nenda kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la kwenu au uwaandikie wachapishaji wa gazeti hili.