Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Serikali Itakayoleta Maadili ya Kimungu

Serikali Itakayoleta Maadili ya Kimungu

Serikali Itakayoleta Maadili ya Kimungu

HEBU wazia kukiwa na serikali moja ulimwenguni ambayo inatawala watu wa jamii zote na lugha. Hebu wazia serikali ambayo inalinda maadili, serikali inayokomesha vita, chuki, uhalifu, umaskini, uchafuzi, ugonjwa, na hata kifo!

Huenda ukasema kwamba hilo ni jambo zuri sana, lakini haliwezekani. La, linawezekana. Hapana shaka litatukia. Yesu Kristo aliahidi serikali ya aina hiyo. Aliwafundisha wanafunzi wake kusali kwa ajili yake: “Basi, nyinyi lazima msali kwa njia hii: ‘Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe. Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.’”—Mathayo 6:9, 10.

Huenda unaijua sala hiyo kwani mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanaijua, ama wamewahi kuisikia. Lakini je, umewahi kufikiria maana ya sala hiyo? Ona kwamba Ufalme unahusiana na kutendeka kwa mapenzi ya Mungu duniani. Basi, Ufalme wa Mungu ni nini? Na mapenzi ya Mungu ni nini kwa ajili ya dunia?

Maana ya Ufalme wa Mungu

Ufalme unaweza kufafanuliwa kuwa serikali inayoongozwa na mfalme. Ufalme wa Mungu ni njia ya Yehova Mungu ya kuonyesha enzi yake kuu ya ulimwengu wote mzima. Ni serikali inayoongozwa na Mwana wake, Yesu Kristo. Kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia limeelezwa waziwazi kabisa kwenye Zaburi 37:10, 11: “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo. Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”

Kwa hiyo usivunjike moyo kwa sababu ya maadili yanayoendelea kuzorota ulimwenguni. Biblia inaahidi kwamba hivi punde maadili na hali za ulimwengu zitabadilika kabisa. Tunaweza kutumaini kabisa ile ahadi ya kwamba Ufalme wa Mungu utatawala dunia hivi punde na kuleta maadili ya Mungu.

Tunaweza kupata usalama mwingi tunapoamini ahadi za Ufalme wa Mungu. Hebu ona maadili yatakayoletwa na Ufalme huo: “Njoni myatazame matendo ya BWANA, jinsi alivyofanya ukiwa katika nchi. Avikomesha vita hata mwisho wa dunia.” (Zaburi 46:8, 9) Ni ahadi nzuri kama nini ya amani na usalama!

Zaburi 72:12-14 inasema hivi inapozungumzia unabii fulani unaomhusu Mfalme wa Ufalme wa Mungu, Yesu Kristo: “Atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa. Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu, na damu yao ina thamani machoni pake.”

Maadili Yaliyomo Katika Biblia

Hebu ona baadhi ya maadili ambayo Biblia inafundisha: “Wenye furaha ni wale wenye kuona uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Pia inasema hivi: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.”—Mithali 3:5, 6.

Biblia pia inafundisha kwamba sote tunawajibika kuhusiana na maadili tunayochagua. Hebu ona jinsi Mhubiri 11:9 inavyosema: “Wewe kijana, uufurahie ujana wako, na moyo wako ukuchangamshe siku za ujana wako, ukaziendee njia za moyo wako, na katika maono ya macho yako, lakini ujue wewe ya kwamba kwa ajili ya hayo yote Mungu atakuleta hukumuni.” Andiko la Mithali 2:21, 22, linaonyesha wazi kwamba tunawajibika kwa yale tunayotenda: “Wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”

Kwa kuwa tumaini hilo kuhusu serikali yenye uadilifu linatia moyo sana, ni muhimu sana kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Tukishirikiana na wengine wanaotaka kuwa raia za Ufalme wa Mungu, hilo litatusaidia kujitayarisha kufurahia utawala wa Ufalme huo mtukufu na baraka zitakazotokana na maadili yake bora.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wapole “watairithi nchi” na “watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—ZABURI 37:11.