Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanyeje Msiba Ukitokea?

Nifanyeje Msiba Ukitokea?

Vijana Huuliza . . .

Nifanyeje Msiba Ukitokea?

“Kwa nini magaidi walimwua mama yangu?” —Kevin. *

“[Kabla ya Septemba 11], nilipenda njia za chini ya ardhi. Lakini siku hizi mimi huwazia nikifa katika mlipuko wa njia ya chini ya ardhi.” —Peter.

MAMA ya Kevin alikufa mnamo Septemba 11, 2001, wakati majengo ya World Trade Center katika New York City yaliposhambuliwa. Peter hakupatwa na maafa makubwa hivyo, lakini aliathiriwa sana na tukio hilo.

Ripoti moja ya habari inasema hivi: “Maelfu ya watoto wanaoishi jijini New York wana matatizo ya akili yanayohusiana na [mashambulizi ya] Septemba 11, na mengi yataendelea hata watakapokuwa watu wazima.” Kwa kusikitisha, “watoto waliokuwa mbali na majengo hayo waliathiriwa kihisia kama tu wale walioona msiba wenyewe ukitokea.” *

Hali huwa hivyo pia kuhusiana na misiba mingine, kama vile mabomu ya kujilipua huko Israeli na mashambulizi ya kiholela kwa kutumia risasi kwingineko. Kuhusu mashambulizi kama hayo ya risasi, mtaalamu mmoja wa mfadhaiko alisema hivi: “Hata ikiwa watoto wanaishi umbali wa kilometa 3,200 hivi kutoka mahali pa mashambulizi, matukio hayo yanaweza kuongeza mfadhaiko [wao].”

Kwa nini? Misiba inapotokea, vyombo vya habari huonyesha picha nyingi sana kuhusiana na matukio hayo na vijana huzitazama. Picha zenye kuogopesha za mashambulizi ya kigaidi, kushambuliwa kwa bunduki shuleni, na misiba ya kiasili huonyeshwa tena na tena, hivyo huwa vigumu kwa vijana wengi kusahau matukio hayo. Basi si ajabu kwamba ripoti ya uchunguzi wa Kamati ya Elimu ya New York City ilionyesha kwamba: “miezi sita baada ya majengo ya World Trade Center kushambuliwa, asilimia 76 ya wanafunzi 8,266 katika shule za umma waliendelea kukumbuka mashambulizi hayo ya kigaidi.”

Tunaishi katika kipindi ambacho Biblia inaita “nyakati zenye kuogofya.” (2 Timotheo 3:1-5, New International Version) Unawezaje kukabiliana na misiba? *

Kwa Nini Misiba Hutokea?

Njia moja ya kukabiliana na maafa ni kutumia “uwezo wetu mwangavu wa kufikiri.” (2 Petro 3:1) Jaribu kuona mambo kwa njia nzuri, kama Mungu anavyoyaona. Kwa mfano, unapaswa kukumbuka kwamba misiba mingi hutokea kwa sababu ya “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11, NW) Yesu Kristo alitoa mfano wa jambo hilo alipoelezea kuanguka kwa mnara wa Siloamu. Watu 18 walikufa katika msiba huo. Hata hivyo, Yesu alisema kwamba Mungu hakuwa anawaadhibu watu hao. Walikufa tu kwa sababu walikuwa mahali pasipofaa kwa wakati usiofaa. (Luka 13:1-5) Kutafakari kuhusu jambo hilo kunaweza kukusaidia uwe na maoni yanayofaa kuhusu misiba.

Maoni yanayofaa yanaweza kukusaidia ‘usielekeze hasira yako dhidi ya Mwenyezi Mungu.’ (Mithali 19:3, Biblia Habari Njema) Yehova ni “Mungu wa faraja yote,” hivyo hatuletei mateso. (2 Wakorintho 1:3) Misiba inapotokea tunapaswa kumkaribia, badala ya kujitenga mbali naye kwa hasira. Tafakari kuhusu maneno ya Biblia katika Yakobo 1:13: “Wakati yuko chini ya jaribu, acheni yeyote asiseme: ‘Mimi ninajaribiwa na Mungu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” *

Msiba uliotokea karne nyingi zilizopita huko Mashariki ya Kati unaweza kututhibitishia jambo hilo. Biblia inasema kwamba mtu pekee aliyeokoka msiba huo aliripoti hivi: “Moto wa Mungu ulianguka kutoka mbinguni na kuwateketeza kondoo, na wale watumishi, na kuwaangamiza.” (Ayubu 1:16) Huo ulikuwa msiba ulioje! Isitoshe, mtu huyo aliyekuwa na woga alifikiri kwamba Mungu ndiye aliyekuwa ameusababisha. Lakini, haikuwa hivyo. Kitabu cha Ayubu 1:7-12 kinasema kwamba moto huo haukuletwa na Mungu, bali na Mpinzani wake, Shetani Ibilisi!

Hilo lilikuwa tukio la pekee: Yehova alimruhusu Shetani ajaribu uaminifu wa Ayubu. Kwa hiyo usikate maneno kwamba Shetani anahusika moja kwa moja katika misiba ya kiasili kama vile dhoruba na mafuriko. * Hata hivyo, Biblia inasema kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19) Hivyo, anaweza kutumia wanadamu kuleta maafa na uharibifu.

Hata hivyo, hatuhitaji kuhisi tumeshindwa kabisa. Fikiria kisa kingine kwenye Biblia katika kitabu cha 1 Samweli 22:12-23. Andiko hilo linasema kuhusu mauaji mabaya sana ya kikundi cha makuhani waaminifu na familia zao. Bila shaka, Shetani alichochea Mfalme Sauli mwovu afanye ukatili huo mbaya. Hata hivyo, Daudi mwaminifu, ambaye hatimaye alikuwa mfalme, aliandika Zaburi ya 52 ambapo alionyesha uhakika kwamba Mungu angewaangamiza watu waovu waliosababisha msiba huo.—Zaburi 52:5.

Vivyo hivyo leo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu hataendelea kuvumilia milele mauaji na jeuri inayochochewa na Ibilisi. Ndiyo sababu Biblia inaahidi kwamba hivi karibuni Mungu atamtumia Mwana wake, Yesu, ‘kuvunja-vunja kazi za Ibilisi’! (1 Yohana 3:8) Hatimaye, hakutakuwa na masalio yoyote ya uharibifu ambao umesababishwa na Shetani. Mungu anaweza hata kuwafufua watu ambao wamekufa katika misiba inayosababishwa na jeuri au ugaidi.—Matendo 24:15.

Njia za Kukabiliana na Misiba

Ahadi hiyo ya Biblia inaweza kukusaidia ukabiliane na woga wa kupita kiasi. Lakini pia kuna hatua unazoweza kuchukua. Kwa mfano, unaweza kutumia kanuni inayopatikana katika Mithali 12:25. Ni kwa kuwaambia wengine jinsi unavyohisi ndipo unaweza kupokea “neno jema” la kukutia moyo. Kufanya hivyo kunaweza kukusaidia utambue kwamba huko peke yako katika msiba huo. Kwa hiyo, ikiwa umevunjika moyo, jaribu kuzungumza na wazazi wako au Mkristo mwingine mkomavu kutanikoni. *

Dokezo jingine: Usitazame picha nyingi za misiba katika habari. Kufanya hivyo kunaweza kukufanya usisahau matukio hayo.—Zaburi 119:37.

Je, wewe ni Mkristo? Basi shikamana na ratiba yako ya mambo ya kiroho. (Wafilipi 3:16) Mambo hayo ni kama vile kuhudhuria mikutano pamoja na Wakristo wenzako na kushiriki imani yako pamoja na watu wengine. (Waebrania 10:23-25) Hilo litakusaidia usikazie fikira mambo mabaya siku zote. Kujitenga kunaweza kukuathiri vibaya kihisia na kiroho.—Mithali 18:1.

Kuendelea kusoma Biblia kila siku kunaweza kukusaidia ukabiliane na mikazo. Mama ya msichana mmoja aitwaye Loraine alikuwa anaugua kansa. Ona jinsi Loraine alivyoweza kukabiliana na hali hiyo ngumu: “Nakumbuka nikisoma kitabu cha Ayubu mara kadhaa wakati huo. Kitabu cha Zaburi kilinifariji sana pia. Nilipokuwa nikisoma maneno hayo yenye kufariji kutoka kwa Maandiko, nilihisi kana kwamba Yehova alikuwa ananikumbatia.” Mishael, dada yake, akumbuka hivi: “Nilijua siku ambazo sikusoma Biblia. Akili zangu zilianza kufikiria mambo mabaya. Kusoma Biblia kulinipa nguvu za kiroho nilizohitaji kila siku.”

Iwapo umepatwa na msiba, hasa kufiwa na mpendwa, unaweza kupata faraja kwa kusoma broshua Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa. * Soma na utafakari maandiko yote yaliyoonyeshwa. Pia, tafakari kuhusu tumaini la ufufuo. “Ni kana kwamba nilimwona mama yangu akifufuliwa,” asema Loraine. “Nilimsikia akisema hivi: ‘Nimerudi. Mmepika nini jioni hii?’ Jambo hilo lilinifanya nitabasamu.”

Ukimtegemea Yehova kupitia sala, anaweza kukuimarisha ili ukabiliane na msiba mbaya. Loraine akumbuka: “Nilikuwa chumbani mama yangu alipokufa. Wakati huohuo nilisali kwa Yehova, nikimwomba anipe nguvu ya kuvumilia hali hiyo. Wakati huohuo nilipata amani ya Mungu.” Taja mambo waziwazi unaposali kwa Yehova. Mjulishe jinsi unavyohisi. Mtunga-zaburi anatusihi hivi: “Ifunueni mioyo yenu mbele zake.”—Zaburi 62:8.

Kadiri wakati unavyosonga, kuna uwezekano mkubwa kwamba taabu zitaongezeka duniani. (2 Timotheo 3:13) Lakini Biblia inaahidi hivi: “Maana watenda mabaya wataharibiwa . . . Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:9-11, 29) Ukiitumaini ahadi hiyo kabisa, utafaulu kukabiliana na misiba.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 6 Kulingana na wataalamu wa magonjwa ya akili, dalili za magonjwa ya akili ni kukosa hisia, kuota ndoto mbaya, kujitenga, kutoweza kufanya shughuli za kawaida, na kuhisi hatia au hasira.

^ fu. 9 Ingawa makala hii inazungumzia misiba mikubwa, mashauri yanayotolewa yanaweza kutumiwa pia mtu mmoja-mmoja anapopatwa na maafa, kama vile kufiwa na mpendwa.

^ fu. 12 Ukitaka kujua kwa nini Mungu huruhusu kuteseka, ona sura ya 7 ya kitabu Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 14 Ona makala “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Kiingereza la Desemba 1, 1974.

^ fu. 18 Iwapo mtu amefadhaika sana au ameshuka moyo, huenda akahitaji kumwona daktari.

^ fu. 22 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Inafaa udhibiti utazamaji wa picha zenye kuogofya katika vyombo vya habari