Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Utatuzi wa Kudumu?

Je, Kuna Utatuzi wa Kudumu?

Je, Kuna Utatuzi wa Kudumu?

UHALIFU huonwa kuwa jambo lisiloepukika katika ulimwengu wa leo. Licha ya jitihada nzuri za wafanyakazi wa jamii, polisi, na watu wanaorekebisha tabia za wahalifu, ulimwengu unazidi kuwa hatari. Je, kuna utatuzi?

Biblia inaonyesha kwamba kutakuwa na badiliko kubwa wakati ujao. Badiliko hilo halitaletwa na serikali za wanadamu. Wanadamu wote wanaotawala hawana uwezo kamili, hata iwe wana miradi mizuri jinsi gani. Hawana uwezo na namna ya kuondoa chanzo cha uhalifu wala kuleta usalama wa kudumu.

Badiliko hilo linaloelezwa katika Biblia litaletwa na Muumba wetu. Kwa kuwa yeye ndiye Mfanyi wa ulimwengu wote, ana uwezo na haki ya kufanya yale ambayo wanadamu hawawezi. Biblia inasema kwamba yeye “ndiye awatanguaye wakuu, na kuwabatilisha waamuzi wa dunia . . . yeye ni hodari kwa nguvu zake.” (Isaya 40:23-26) Mungu anaahidi kuleta mabadiliko gani, na je, kweli yanatupa tumaini hakika kwamba hali zitaboreka ulimwenguni?

Zaburi 37:10 inasema hivi kuhusu ahadi ya Mungu: “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala [asiye haki] hatakuwapo.” Mungu anakusudia kuwakatilia mbali watu waovu kabisa ambao hawataki kubadilika. Hata hivyo, hatawaharibu watu wote. Mtunga-zaburi anawaahidi hivi wote wale wanaotaka kuwa wapole, wanyenyekevu, na wanaopenda amani: “Wewe umngoje BWANA, uishike njia yake, naye atakutukuza uirithi nchi, wasio haki watakapoharibiwa utawaona.” Waovu wakiisha kuondolewa, watakaobaki watafurahia “wingi wa amani”—ulimwengu usio na uhalifu wa aina yoyote.—Zaburi 37:11, 34.

Watu Wanahitaji Kubadili Maoni na Mioyo

Ili kuondoa uhalifu usiwepo daima dawamu, haitoshi tu kuwaharibu watu waovu na kuwaacha watu wazuri. Mengi zaidi yahitajiwa. Mara nyingi uhalifu hutokea kwa sababu akili na mioyo ya watu haijazoezwa vizuri. Hata hivyo, hapo ndipo serikali ya Mungu ni bora kuliko zote. Maagizo na elimu zitatolewa ili kuwazoeza watu kupenda uadilifu. Isaya 54:13 inasema: “Watoto wako wote watafundishwa na BWANA; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.”

Matokeo yataridhisha wee! Biblia inaonyesha vizuri mabadiliko yatakayofanywa na watu ambao zamani walikuwa kama wanyama. Inasema: “Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja.” Kwa nini? “Maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Isaya 11:6, 9) Hata hivyo, wewe na familia yako hamhitaji kungojea hadi wakati ujao ili mfanye mabadiliko hayo. Kwa nini?

Unaweza Kufaidika Sasa

Kuna watu ambao wanafanya mabadiliko sasa ili waishi katika ulimwengu usio na uhalifu. Tayari wanavaa utu mpya, utu ambao Mungu anataka watu watakaoishi katika ulimwengu wake mpya wawe nao. (2 Petro 3:13) Wanafanya hivyo kwa kutumia kanuni za Biblia maishani mwao. Ona maelezo haya yenye kupendeza katika Biblia: “Mfanywe upya katika kani inayotendesha akili yenu, na mvae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.”—Waefeso 4:23, 24.

Wakolosai 3:12-14 inaelezea zaidi sifa nzuri ambazo watu wengi wenye mioyo minyofu wanasitawisha sasa. Inasema hivi: “Kama wachaguliwa wa Mungu, watakatifu na wapendwa, jivikeni wenyewe shauku nyororo za huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, na ustahimilivu. Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe nyinyi kwa hiari, fanyeni hivyo nyinyi pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni wenyewe upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”

Je, ungependa kusaidiwa kuvaa utu mpya wa Kikristo? Tayari mamilioni ya watu ulimwenguni kote wanasaidiwa na Mashahidi wa Yehova kufanya hivyo. Kwenye mikutano inayofanywa kwa ukawaida kwenye Majumba ya Ufalme, na kwenye makusanyiko makubwa, hata watu ambao hapo zamani walikuwa wahalifu wajeuri wamejifunza jinsi ya kuwa wenye amani. * Ikiwa ungependa kufaidika kutokana na elimu hiyo nzuri ya Biblia, waandikie wachapishaji wa gazeti hili. Watafurahi kukusaidia uwe miongoni mwa watu wanaojitayarisha sasa kuishi katika ulimwengu wa Mungu usio na uhalifu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Ili upate mifano, ona toleo la Amkeni! la Mei 8, 2001, ukurasa wa 8-10.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mamilioni wanapata elimu itakayowawezesha kuishi katika ulimwengu usio na uhalifu