Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wakristo Wanapaswa Kupumbazwa Akili?

Je, Wakristo Wanapaswa Kupumbazwa Akili?

Maoni ya Biblia

Je, Wakristo Wanapaswa Kupumbazwa Akili?

“Asionekane kwako mtu . . . alogaye kwa kupiga mafundo.” —KUMBUKUMBU LA TORATI 18:10, 11.

KUPUMBAZWA akili (uhiponozi) kumekuwa mjadala mkuu na wenye kubishaniwa. * Hata wataalamu wa kupumbaza akili hushindwa kueleza jinsi kunavyofanya kazi. Kwa kawaida inaeleweka kwamba kupumbaza akili ni hali iliyopinduliwa ya fahamu, au kuduwaa. Hata hivyo, watu wengi hupendezwa na faida inayoletwa na kupumbazwa akili badala ya kutaka kujua jinsi kunavyofanya kazi.

Katika miaka ya hivi karibuni, limekuwa jambo la kawaida kwa wanatiba katika nchi kadhaa kupendekeza tiba ya kupumbazwa akili. Kwa mfano, gazeti Psychology Today linasema hivi: “Matibabu ya kupumbazwa akili yanaweza kutibu maumivu ya kichwa, kupunguza maumivu ya kuzaa, kumsaidia mtu aache kuvuta sigara, kutumiwa badala ya nusukaputi, na kuboresha tabia za kujifunza. Matibabu hayo hayana madhara yoyote.” Kwa upande mwingine, kupumbazwa akili huhusianishwa mara nyingi na kuwasiliana na roho na uchawi.

Maoni ya Biblia ni nini? Bila shaka Biblia si kitabu cha tiba, na haitaji moja kwa moja habari ya kupumbaza akili. Lakini kanuni zinazopatikana katika Neno la Mungu zinaweza kutusaidia tuone maoni ya Mungu.

Je, Kuna Uhusiano Kati ya Kupumbazwa Akili na Uchawi?

Je, madai ya kwamba kuna uhusiano kati ya kupumbazwa akili na uchawi ni mawazo yaliyobuniwa na mtu fulani tu? Hadithi zisizo za kweli katika sinema na vitabu vya riwaya zimeendelea kuchochea wazo hilo, hata hivyo, kuna uhusiano kati ya kupumbazwa akili na kuwasiliana na roho. Kuhusu kupumbazwa akili, kitabu Encyclopedia of Occultism and Parapsychology kinasema hivi: “Tangu zamani kulihusisha sana uchawi.” Kuduwazwa kidini, ambako kumekuwa sehemu ya uchawi na mazingaombwe kwa muda mrefu, kunaonwa kwa kawaida kuwa aina fulani ya kupumbazwa akili. Pia, makuhani katika Misri na Ugiriki ya kale walimweka mtu katika hali kama ya kupumbazwa akili walipojaribu kutibu ugonjwa kwa uwezo wa miungu yao ya uwongo.

Ensaiklopedia iliyotajwa hapo juu yasema: “Hata leo maajabu mengi ya kupumbazwa akili yanaonwa kuwa ‘Mawasiliano na Roho.’” Ingawa ni vigumu kuelewa ni kwa kadiri gani ambavyo aina mbalimbali za kupumbaza akili huenda zikahusiana na uchawi, ukweli ni kwamba Mungu hukataza mawasiliano yoyote na roho. (Kumbukumbu la Torati 18:9-12; Ufunuo 21:8) Kwa hiyo, Wakristo hawapaswi kupuuza kwamba kupumbazwa akili hakupatani na maandiko.

Jinsi Kunavyoathiri Tabia

Vipi athari zinazompata mtu kiakili na kitabia anapopumbazwa akili? Je, kuna hatari zozote? Wasiwasi mmoja mkubwa ni kwamba mtu aliyepumbazwa akili anaweza kukosa kudhibiti tabia yake. Watu wanaopumbaza wengine akili katika maonyesho hutumia mbinu hii, wakiwachochea wenye kujitolea wafanye mambo ambayo kwa kawaida hawangefanya, hata kuwafanya waonekane kama walevi.

Kitabu The Encyclopedia Americana chasema hivi kuhusu maonyesho hayo ya kupumbaza watu akili: “Mtu ambaye anapumbazwa akili anaweza kuongozwa kwa urahisi na yule anayempumbaza, anaweza kuongozwa kwa urahisi na tamaa zake ambazo hazionekani wazi kwa ukawaida, na anapopumbazwa huenda akahisi kwamba hahitaji kufuata mwenendo wa kawaida tena.” Kitabu Collier’s Encyclopedia nacho chasema hivi: “Mtu ambaye amepumbazwa akili anaweza kukaza fikira zake kabisa, na hilo linamfanya akubali uongozi wa yule ambaye amempumbaza na kuyafuata madokezo yake.”

Je, hilo halina madhara? Je, ingefaa Mkristo wa kweli ajiruhusu kuongozwa na madokezo ya mtu ambaye anampumbaza akili? Hilo litapingana na shauri hili la mtume Paulo: ‘Toeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri kuzuri. Na komeni kufanyizwa kulingana na mtindo wa mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe umbo kwa kufanya upya akili yenu, ili mpate kujithibitishia wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.’—Waroma 12:1, 2.

Je, Mkristo anaweza kuwa na “dhamiri njema,” akijiruhusu kuwekwa katika hali ambayo hataweza kudhibiti akili zake kikamili au tamaa zake, au hata matendo yake? (1 Petro 3:16) Biblia hushauri hivi: “Kila mmoja wenu [apaswa] kujua jinsi ya kupata umiliki wa chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima.” (1 Wathesalonike 4:4) Ni dhahiri kwamba, kupumbazwa akili kutamzuia mtu asifuate shauri hilo.

Tumaini la Kupata Afya Kamilifu

Kulingana na kanuni za Biblia zilizotajwa hapo juu, Mashahidi wa Yehova huepuka njia zinazohusiana na kupumbazwa akili au kujipumbaza akili. Wanatii amri iliyo kwenye Kumbukumbu la Torati 18:10, 11: “Asionekane kwako mtu . . . alogaye kwa kupiga mafundo.” Kwa wale wanaopatwa na matatizo ya afya, kuna tiba nyingine za aina nyingi ambazo hazimwingizi mtu katika hatari za uchawi au kuruhusu akili yake kuongozwa vibaya na wengine.

Kwa kuepuka mazoea yasiyopatana na kanuni za Biblia, Wakristo wanaweza kuwa na tumaini la kuishi milele katika ulimwengu wenye uadilifu wa Mungu. Wakati huo wanadamu watafurahia afya kamilifu kimwili na kiakili bila kupumbazwa akili.—Ufunuo 21:3, 4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kupumbazwa akili ni hali ya kumtia mtu mwingine katika usingizi na kumfanya akumbuke mambo ambayo alikuwa amesahau, kumfanya aone njozi, au kumfanya aongozwe kwa urahisi na yule ambaye anampumbaza.