Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Mauaji ya Kijeuri Yameongezeka Sana?

Kwa Nini Mauaji ya Kijeuri Yameongezeka Sana?

Kwa Nini Mauaji ya Kijeuri Yameongezeka Sana?

AINA zote za uhalifu ni mbaya. Hata hivyo, uhalifu unaofanywa bila sababu hususa haueleweki. Majasusi hushangazwa sana na visa hivyo vya uhalifu kwani mara nyingi vinafanywa bila kusudi hususa. Kutokana na maendeleo ya vyombo vya habari katika miaka ya hivi karibuni, habari za visa hivyo vya uhalifu vyenye kushtua husambazwa haraka kwa mamilioni, au hata mabilioni ya watu. Ripoti iliyochapishwa na Shirika la Afya Ulimwenguni inasema kwamba “jeuri huathiri mabara yote, nchi zote, na jamii nyingi.”

Matendo ya kijeuri yanayofanywa bila sababu hususa yametokea hivi karibuni hata katika maeneo ambayo zamani yalikuwa salama kwa kadiri fulani. Kwa mfano, kwa muda mrefu hakujawa na visa vingi vya mauaji ya kijeuri huko Japan. Hata hivyo, mnamo Juni 2001, mwanamume mmoja aliingia katika shule moja huko Ikeda akiwa amebeba kisu, akaanza kuwadunga-dunga na kuwakata-kata watoto. Aliwaua watoto 8 na kuwajeruhi wengine 15 kwa dakika 15 tu. Kisa hicho na visa vingine huko Japan, kama vile vinavyohusu vijana wanaowaua watu wasiowajua hata kidogo ili kujifurahisha, vinaonyesha wazi kwamba mambo yamebadilika.

Hata katika nchi zenye uhalifu mwingi, matendo fulani ya kichaa yamewafanya watu walalamike. Hilo lilionekana wazi baada ya majengo ya World Trade Center huko New York kushambuliwa mnamo Septemba 11, 2001. Mwanasaikolojia Gerard Bailes alisema hivi: “Tukio hilo limefanya ulimwengu ubadilike kabisa na kuwa hatari sana hivi kwamba huwezi kujua jambo litakalotendeka baadaye.”

Kwa Nini Wanaua Watu Kijeuri?

Hakuna sababu hususa inayoeleza kwa nini watu wanafanya matendo ya kichaa ya kijeuri. Visa fulani vya uhalifu havieleweki kwani vinafanywa bila kusudi maalumu. Kwa mfano ni vigumu zaidi kuelewa sababu inayomfanya mtu awadunge kisu watu asiowajua kamwe au aendeshe gari lake hadi kwenye nyumba yoyote ile na kuanza kufyatua risasi ovyoovyo.

Watu wengine wanasema kwamba watu huzaliwa wakiwa wajeuri. Wengine wanasema kwamba wanadamu wanaweza kuepuka kufanya matendo ya kijeuri yasiyo na msingi wowote.—Ona sanduku “Je, Ni Asili ya Wanadamu Kuwa Wajeuri?”

Wataalamu wengi wanaamini kwamba kuna sababu na hali nyingi zinazowachochea watu kufanya matendo ya kijeuri yasiyo ya akili. Ripoti iliyochapishwa na Taasisi ya Shirika la Ujasusi la Marekani inasema hivi: “Mtu mwenye akili timamu hawezi kumuua mwenzake.” Watu fulani wanaweza kupinga kauli hiyo. Hata hivyo, wengi wanakubaliana na wazo lake. Watu wanaofanya mauaji ya kijeuri si timamu. Jambo fulani huwa limeathiri akili zao kiasi cha kwamba wanafanya yasiyowazika. Ni mambo gani yanayowachochea watu kufanya matendo hayo? Hebu tuchunguze mambo kadhaa ambayo wataalamu wamesema kwamba yanaweza kuwachochea watu kufanya hivyo.

Kuvunjika kwa Familia

Mwandishi wa Amkeni! alimwomba Marianito Panganiban, msemaji wa Idara ya Kitaifa ya Ujasusi huko Ufilipino, aeleze kuhusu maisha ya utotoni ya watu wanaofanya uhalifu wa kinyama. Alisema hivi: “Wanatoka katika familia zilizovunjika. Hawakutunzwa wala kuonyeshwa kwamba wanapendwa. Watu hawana maadili thabiti kwani wamekosa mwongozo na hivyo wamepotoka.” Watafiti wengi wanasema kwamba wahalifu wengi wakatili wametoka katika familia zenye matatizo na zenye jeuri.

Kituo cha Kitaifa cha Uchanganuzi wa Mauaji ya Kijeuri cha Marekani kilitoa ripoti iliyotaja mambo ambayo yanawatambulisha vijana wanaoweza kufanya mauaji shuleni. Yafuatayo ni baadhi ya mambo yaliyotajwa ambayo hutukia katika familia: uhusiano mbaya kati ya mzazi na mtoto, wazazi wasiotambua matatizo ya watoto wao, kutokuwa na uhusiano wa karibu, wazazi wasiowawekea watoto wao mipaka, na watoto wanaoficha mambo yao kabisa huku wakiishi maisha maradufu bila wazazi kujua.

Leo watoto wengi wanaathiriwa na kuvunjika kwa familia. Wazazi wa watoto wengine hawatumii wakati mwingi pamoja nao. Vijana wengi sana wamelelewa bila mwongozo wa kutosha wa kifamilia na wa kimaadili. Wataalamu fulani wanasema kwamba hali kama hiyo inaweza kuwafanya watoto wasipatane vizuri na wengine, na hivyo kuwafanya watake kuwaumiza wanadamu wenzao, na mara nyingi hawahisi hatia yoyote.

Makundi Yenye Chuki na Madhehebu

Uthibitisho unaonyesha kwamba madhehebu na makundi fulani yenye chuki yamechangia sana matendo fulani ya uhalifu. Mtu mmoja mweusi mwenye umri wa miaka 19 huko Indiana, Marekani, alikuwa akielekea nyumbani baada ya kutoka dukani. Muda mfupi baadaye, alipatikana akiwa amelala kando ya barabara huku akiwa na risasi ubongoni. Kijana aliyemfyatua alitaka kumuua mtu yeyote tu. Kwa nini? Inasemekana kwamba muuaji huyo alitaka kuwa mwanachama wa kundi fulani linalopendelea watu weupe zaidi ya weusi na alitaka kutiwa alama ya utando wa buibui ngozini kwa sababu ya kumuua mtu mweusi.

Shambulizi lililofanywa mnamo mwaka wa 1995 kwenye njia ya chini kwa chini huko Tokyo kwa gesi yenye sumu; kisa cha watu wengi kujiua pamoja huko Jonestown, Guyana; na vifo vya wafuasi 69 wa Madhehebu ya Solar Temple vilivyotukia huko Uswisi, Kanada, na Ufaransa vilichochewa na madhehebu. Mifano hiyo inaonyesha jinsi makundi fulani yameathiri sana fikira za watu wengine. Viongozi wenye uvutano wamewachochea watu kufanya “unyama” wakiwaahidi kwamba watapata faida fulani.

Uhusiano Kati ya Vyombo vya Habari na Jeuri

Wengine wanasema kwamba vyombo vya kisasa vya mawasiliano vinaweza kuchangia jeuri. Inasemekana kwamba kutazama jeuri kwa ukawaida kwenye televisheni, sinema, michezo ya video, na kwenye Internet kwaweza kufanya dhamiri za watu zisifanye kazi na kuwachochea kuua kijeuri. Dakt. Daniel Borenstein, rais wa Chama cha Wataalamu wa Magonjwa ya Akili wa Marekani, alisema: “Kwa sasa kuna zaidi ya uchunguzi 1,000 unaotegemea utafiti uliofanywa kwa zaidi ya miaka 30 ambao unaonyesha kwamba jeuri kwenye vyombo vya habari husababisha watoto fulani kuwa wajeuri.” Dakt. Borenstein alisema hivi mbele ya kamati ya Bunge la Marekani: “Tunasadiki kwamba kutazama jeuri ya kila aina tena na tena ni hatari sana kwa watu wote.”—Ona sanduku “Maoni ya Daktari Kuhusu Michezo ya Kompyuta Yenye Jeuri.”

Visa mbalimbali hutajwa mara nyingi ili kuonyesha ukweli wa kauli hiyo. Katika kisa kilichotajwa kwenye makala ya kwanza cha yule mtu aliyewaua wenzi wawili wa ndoa walipokuwa ufuoni wakitazama jua likichomoza, waendesha-mashtaka waliwasilisha uthibitisho ulioonyesha kwamba mauaji hayo ya kujifurahisha yalifanywa kwa sababu ya kutazama mara nyingi sinema yenye jeuri. Katika kisa kilichotukia shuleni ambapo watu 15 walipigwa risasi na kuuawa, inasemekana kwamba wale wanafunzi wawili waliofanya mauaji hayo walikuwa wakicheza michezo ya video yenye jeuri kwa saa nyingi kila siku. Isitoshe, walipenda kutazama sinema zenye jeuri nyingi na mauaji.

Dawa za Kulevya

Huko Marekani, visa vya mauaji vilivyofanywa na vijana viliongezeka mara tatu katika kipindi cha miaka minane. Wenye mamlaka wanasema ni nini kinachochangia hali hiyo? Magenge, na hasa magenge yanayotumia kokeini kali. Kati ya zaidi ya mauaji 500 yaliyotukia hivi majuzi huko Los Angeles, California, “polisi walisema kwamba magenge yalihusika katika asilimia 75 ya mauaji hayo.”

Ripoti moja iliyochapishwa na Taasisi ya Shirika la Ujasusi la Marekani inasema hivi: “Dawa za kulevya huchangia visa vingi sana vya mauaji.” Watu fulani waliopotoshwa fikira kwa sababu ya kutumia dawa za kulevya huua wanapozitumia. Wengine huwa wajeuri ili watetee biashara yao ya kuuza dawa za kulevya. Ama kweli, dawa za kulevya huwachochea watu sana kufanya matendo ya kuogopesha.

Silaha Hatari Zinapatikana kwa Urahisi

Kama ilivyotajwa kwenye makala inayotangulia, mtu mmoja huko Tasmania, Australia, aliwaua watu 35 kwa kuwapiga risasi. Aliwajeruhi wengine 19. Mtu huyo alikuwa na silaha hatari za kijeshi. Kisa hicho kiliwafanya wengi waone kwamba mauaji ya kijeuri yameongezeka kwa sababu silaha zinapatikana kwa urahisi.

Ripoti moja inaonyesha kwamba mnamo mwaka wa 1995 kulikuwa na visa 32 tu vya mauaji ya kutumia bunduki huko Japan. Vingi kati ya visa hivyo vilihusisha wezi ambao waliwaua wezi wenzao. Kwa upande mwingine, kulikuwa na zaidi ya visa 15,000 vya mauaji ya kutumia bunduki huko Marekani. Mbona kuna tofauti hiyo? Wengine wanasema kwamba ni kwa sababu ya sheria kali za Japan zilizowekwa ili kuwazuia watu kumiliki bunduki.

Watu Wameshindwa Kukabiliana na Matatizo

Watu fulani wanaposikia kuhusu matendo fulani ya kinyama wanaweza kusema hivi, ‘Mtu huyo ana kichaa!’ Hata hivyo, wengine wanaofanya matendo hayo hawana kichaa. Lakini, wengi hushindwa kukabiliana na matatizo ya maisha. Wataalamu wanasema kwamba kuna kasoro za utu zinazoweza kumwongoza mtu afanye mambo mabaya sana. Baadhi ya kasoro hizo zinatia ndani: kushindwa kujifunza na kuchangamana na wengine; athari za kudhulumiwa kimwili na kingono; kushindwa kupatana na watu; kuchukia watu wa aina fulani, kama vile wanawake; kutojutia makosa; na tamaa ya kuwatumia wengine ili kujifaidi.

Haidhuru tatizo lao, wengine hulemewa sana na tatizo lenyewe hivi kwamba wanakosa kufikiri vizuri na hivyo wanafanya matendo ya kiajabu. Kisa kimoja kinachoonyesha jambo hilo kinamhusu muuguzi aliyependa sana kusifiwa na watu. Aliwadunga watoto wadogo dawa ya kulegeza misuli ambayo iliwafanya washindwe kupumua. Kisha, akafurahia sifa aliyopata eti kwa “kuwaokoa” watoto hao. Kwa kusikitisha, hakufaulu kuwasaidia wote wapumue tena. Hivyo, akapatikana na hatia ya kuua.

Kwa mintarafu ya yale tuliyokwisha kuyataja, ni wazi kwamba kuna mambo mbalimbali yanayowachochea watu kufanya mauaji ya kijeuri. Hata hivyo, ni lazima tukamilishe hoja zetu kwa kuzungumzia sababu moja ya mwisho iliyo muhimu sana.

Maoni ya Biblia

Biblia inatusaidia kuelewa yale yanayotukia sasa na kwa nini watu wanafanya mambo mabaya kupindukia. Pia inaeleza mitazamo ambayo tunaiona wazi. Kwa mfano, andiko la 2 Timotheo 3:3, 4 linataja kwamba watu wangekosa “shauku ya kiasili” na kwamba wangekuwa “wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wasio na upendo wa mema,” na “wenye vichwa vigumu.” Maneno haya ya Yesu yamenukuliwa katika kitabu kingine cha Biblia: “Upendo wa idadi iliyo kubwa zaidi utapoa.”—Mathayo 24:12.

Biblia inasema: “Katika siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa.” (2 Timotheo 3:1) Naam, yale tunayoona yanaonyesha kwamba tunaishi mwishoni mwa mfumo huu wa mambo. Hali za ulimwengu na mitazamo ya watu inazidi kuzorota. Je, twaweza kutazamia kwamba utatuzi utakuja haraka? Biblia inajibu: “Watu waovu na walaghai wataendelea kutoka ubaya hadi ubaya zaidi.”—2 Timotheo 3:13.

Je, hiyo inamaanisha kwamba wanadamu hawawezi kuepuka kuwa wajeuri na kwamba uhalifu utaongezeka daima? Hebu tuchunguze swali hilo katika makala inayofuata.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Je, Ni Asili ya Wanadamu Kuwa Wajeuri?

Watu fulani wanasema kwamba wanadamu huzaliwa wakiwa na nia ya kuwa wajeuri au nia ya kuua. Watu wanaounga mkono nadharia ya mageuzi wanasema kwamba tulitokana na wanyama wa pori na hivyo tumerithi tabia zao za ujeuri. Dhana hizo zinaonyesha kwamba tutakuwa wajeuri sikuzote.

Hata hivyo, kuna sababu nyingi zinazopinga dhana hizo. Dhana zilizotajwa juu hazionyeshi ni kwa nini visa vya kijeuri hutofautiana sana katika jamii mbalimbali na kwamba vinatukia mara nyingi zaidi katika jamii fulani-fulani. Hazionyeshi ni kwa nini katika jamii fulani watu hupenda kulipiza kisasi wanapotendewa kijeuri, huku kukiwa na visa vichache sana vya jeuri na mauaji katika jamii nyingine. Mtaalamu wa akili Erich Fromm alionyesha kuwa dhana ya kwamba sisi hurithi ujeuri kutokana na wanyama haina msingi wowote aliposema kwamba ijapokuwa wanyama fulani huwa wajeuri kwa sababu ya kujitafutia mahitaji ya msingi au ili kujilinda, ni wanadamu tu wanaowaua wengine ili kujifurahisha tu.

Katika kitabu chao The Will to Kill—Making Sense of Senseless Murder, Profesa James Alan Fox na Profesa Jack Levin wanasema hivi: “Watu fulani ni wajeuri kuliko wengine, lakini wote wana uhuru wa kuamua. Ijapokuwa nia ya kuua huchochewa na hali mbalimbali zilizo nje na ndani ya mwili, nia hiyo bado inahusisha uwezo wa kuchagua na wa kufanya uamuzi, na hivyo mtu anawajibika.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

Maoni ya Daktari Kuhusu Michezo ya Kompyuta Yenye Jeuri

Dakt. Richard F. Corlin, aliyekuwa rais wa Chama cha Kitiba cha Marekani, aliwahutubia madaktari waliokuwa wakihitimu huko Philadelphia, Pennsylvania, Marekani. Katika hotuba hiyo, alizungumzia michezo ya kompyuta inayochochea jeuri. Katika baadhi ya michezo hiyo, wachezaji hupata alama kwa kusababisha majeraha, wanapata alama nyingi zaidi kwa kumpiga mtu risasi mwilini, na hata alama nyingi zaidi kwa kumpiga mtu risasi kichwani. Damu humwagika, na ubongo hutapakaa kotekote.

Dakt. Corlin alisema kwamba watoto hawaruhusiwi kuendesha gari, kunywa pombe, wala kuvuta sigara wanapokuwa wachanga. Kisha akasema: “Lakini sisi huwaruhusu watumie bunduki wakiwa na umri mdogo sana hata kabla hawajajifunza kudhibiti tamaa zao, kabla hawajawa wakomavu, na kabla hawajapata nidhamu ya kutumia silaha wanazocheza nazo bila kusababisha hatari. . . . Tunahitaji kuwafundisha watoto wetu tangu wanapokuwa wadogo kwamba nyakati zote ujeuri una matokeo—matokeo hatari.”

Inasikitisha kwamba badala ya kufundishwa kwamba ujeuri una matokeo mabaya, mara nyingi watoto ndio huuawa kijeuri. Takwimu zinaonyesha kwamba watoto kumi huuawa kila siku huko Marekani kwa kupigwa risasi. Dakt. Corlin anasema: “Nchi ya Marekani ndiyo nchi yenye visa vingi vya watoto wanaouawa kwa kupigwa risasi.” Kisha akakata kauli hii: “Watu wanaotumia bunduki kufanya ujeuri wanahatarisha watu wote katika nchi yetu. Huo ndio ukweli wa mambo.”

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Mambo Yanayochangia Mauaji ya Kijeuri

Wataalamu wengi wanaonelea kwamba mambo yafuatayo yanaweza kuchangia mauaji ya kijeuri:

Kuvunjika kwa familia

Makundi yenye chuki, watu wenye siasa kali

Madhehebu hatari

Burudani yenye jeuri

Kuona matendo ya jeuri

Kutumia dawa za kulevya

Kushindwa kukabiliana na matatizo

Kupata silaha hatari kwa urahisi

Magonjwa fulani ya akili

[Picha katika ukurasa wa 8]

Mojawapo ya milipuko mitano ya mabomu ambapo angalau watu 12 walikufa na zaidi ya watu 80 wakajeruhiwa, katika Jiji la Quezon, Ufilipino

[Hisani]

AP Photo/Aaron Favila December 30, 2000

[Picha katika ukurasa wa 8]

Wanafunzi wawili wamuua mwalimu, wanafunzi 12, kisha wajiua katika Shule ya Sekondari ya Columbine, huko Colorado, Marekani

[Hisani]

AP Photo/Jefferson County Sheriff’s Department April 20, 1999

[Picha katika ukurasa wa 9]

Bomu lililotegwa ndani ya gari lawaua angalau watu 182 na kuwajeruhi wengine 132 waliokuwa katika disko huko Bali, Indonesia

[Hisani]

Maldonado Roberto/GAMMA October 12, 2002