Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Nataka Kila Kitu Ninachofanya Kiwe Kikamilifu?

Kwa Nini Nataka Kila Kitu Ninachofanya Kiwe Kikamilifu?

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Nataka Kila Kitu Ninachofanya Kiwe Kikamilifu?

“Kwa kuwa baba yangu alikuwa mwalimu, kila mtu alitarajia nipate ‘A’ katika kila somo. Nyakati nyingine nilikuwa nikilia sana mpaka ninapolala.”—Leah. *

“Mimi hutaka kila kitu kiwe kikamilifu. Lazima nifanye jambo kwa njia bora kabisa au kwa njia tofauti kabisa na watu wengine, la sivyo hakuna haja ya kulifanya.”—Caleb.

JE, WEWE huhisi kwamba nyakati zote lazima ufanye mambo kikamilifu? Je, wewe huona kwamba hata ukijitahidi kadiri gani, bado huridhiki? Je, wewe huvunjika moyo unapokosolewa? Mambo yanapoharibika je, wewe hujilaumu, na kujiona kuwa mjinga, duni, au hustahili? Unapotaka jambo fulani lifanywe vizuri, je, wewe huhisi kwamba ni lazima ulifanye wewe mwenyewe? Je, wakati mwingine wewe huogopa sana kukosea hivi kwamba unakawia-kawia kufanya mambo au hata unayaacha kabisa?

Uhusiano wako pamoja na wengine ukoje? Je, wewe hukosa marafiki kwa sababu hakuna yeyote anayefanya mambo kikamilifu? Je, wewe huhangaishwa sana na makosa na kasoro za wengine? Ikiwa hivyo ndivyo ilivyo, basi huenda ikawa una tatizo la kudai ukamilifu. Hata hivyo, si wewe peke yako uliye na tatizo hilo. Vijana wengi wana tatizo hilo hasa vijana wenye vipawa au wenye mafanikio. *

Ni nini husababisha hali hiyo ya kudai ukamilifu? Watafiti wanakisia tu. Kitabu Perfectionism—What’s Bad About Being Too Good? chadokeza: “Kudai ukamilifu si ugonjwa, si zoea uliloambukizwa. Kudai ukamilifu hakurithiwi; hukuzaliwa ukiwa na hali hiyo. Kwa hiyo ulipataje kuwa mtu anayedai ukamilifu? Wataalamu fulani wanaamini kwamba kudai ukamilifu huanzia utotoni. Familia, mtu mwenyewe, jamii, vyombo vya habari, na watu maarufu, wote pamoja huwafanya watu fulani wawe na wasiwasi maishani, wakisumbuliwa na dhamiri, na kujitahidi kupita kiasi.”

Hata kisababishi kiwe nini, kudai ukamilifu kunaweza kuyadhuru maisha yako. Hebu tuchunguze vizuri zaidi hali hiyo ya kudai ukamilifu na kwa nini inaweza kukudhuru.

Kudai Ukamilifu Ni Nini?

Kudai ukamilifu hakumaanishi kujitahidi tu kufanikiwa au kuonea fahari kazi iliyofanywa vizuri. Katika Mithali 22:29, Biblia humsifu mtu “mwenye bidii katika kazi zake.” Pia Biblia huwataja watu waliositawisha stadi mbalimbali. (1 Samweli 16:18; 1 Wafalme 7:13, 14) Basi, ni vizuri kujitahidi kupata mafanikio, kuweka miradi ya juu lakini inayoweza kufikiwa. Kwa hiyo, mtu anaweza “kuiburudisha roho yake kwa mema katika kazi yake.”—Mhubiri 2:24.

Hata hivyo, mtu anayedai ukamilifu hatosheki. Ana maoni mabaya kuhusu mafanikio. Kulingana na wataalamu fulani, kudai ukamilifu hutia ndani kuweka “miradi isiyoweza kufikiwa (yaani, ukamilifu), na kukosa kuridhika daima, licha ya mambo ambayo mtu anatimiza.” Kwa hiyo, kudai ukamilifu husababisha “mkazo daima, na mara nyingi humfanya mtu ahisi kwamba hawezi kufaulu.” Kichapo kimoja hufafanua kudai ukamilifu kuwa “imani isiyo na msingi ya kwamba wewe na/au mazingira yako lazima yawe makamilifu.” Ni “mtazamo ulioenea sana wa kwamba kila jambo unalojaribu kufanya maishani lazima liwe kamilifu kabisa, bila kasoro yoyote, kosa lolote, ubaya wowote, wala upungufu wowote.”

Lakini je, Yesu hakusema: “Lazima nyinyi basi mwe wakamilifu, kama Baba yenu wa kimbingu alivyo mkamilifu”? (Mathayo 5:48) Ndiyo, lakini Yesu hakuwa akisema kwamba mtu anaweza kuwa mkamilifu kabisa. Biblia hufundisha kwamba “wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Basi, Yesu alimaanisha nini? Katika Biblia, neno “kamilifu” humaanisha kuwa kamili. (Mathayo 19:21) Yesu aliposema lazima tuwe wakamilifu, alikuwa akizungumza kuhusu upendo naye alikuwa akiwatia moyo wafuasi wake wawe na upendo kikamili zaidi. Jinsi gani? Kwa kuwapenda hata adui zao. Mwandishi wa Biblia Luka aandika maneno haya ya Yesu: “Endeleeni kuwa wenye rehema, sawa na vile Baba yenu ni mwenye rehema.”—Luka 6:36.

Hata hivyo, watu ambao hudai ukamilifu, hujitahidi wakidhani kwamba inawezekana kuwa wakamilifu kabisa. Kwa hiyo huenda wakadai mambo mengi mno kutoka kwa watu wengine. Kulingana na kitabu Never Good Enough—Freeing Yourself From the Chains of Perfectionism, wenye kudai ukamilifu ni “watu ambao hutamaushwa na jinsi ambavyo wengine hufanya kazi zao . . . Wao huona kwamba watu wengine hawajihangaishi kufanya kazi nzuri, wala hawaonei fahari mambo wanayotimiza.”

Kwa mfano, Carly anafanya vema shuleni, naye ameandikishwa katika programu ya wanafunzi wenye vipawa. Hata hivyo, uhusiano kati yake na wengine si mzuri. Amepoteza marafiki wengi kwa sababu anataka kila kitu kiwe kikamilifu. Aeleza, “Nafikiri kwamba walikuwa na kasoro nyingi.”

Huenda wengine wakadai ukamilifu kutoka kwao wenyewe badala ya kutoka kwa wengine. Kitabu Never Good Enough chaeleza kwamba watu kama hao “huhisi kwamba wao wenyewe au matendo yao hayaridhishi . . . , nao huhangaikia sana jinsi wengine wanavyowaona.”

Madhara ya Kujaribu Kuwa Mkamilifu

Kutafuta ukamilifu mara nyingi hakufai na kunadhuru, badala ya kufaidi. Na badala ya kuchangia mafanikio, mtazamo huo mara nyingi huchangia kushindwa. Mwanamume Mkristo anayeitwa Daniel akumbuka jinsi alivyotayarisha kwa muda mrefu na kwa bidii hotuba ambayo aligawiwa kutoa katika shule kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Wasikilizaji wengi walimpongeza kwa kutoa hotuba yake vizuri. Kisha mwalimu wa shule akamshauri Daniel kwa busara. Biblia hututia moyo ‘tusikilize mashauri, na kupokea mafundisho.’ (Mithali 19:20) Lakini badala ya kukubali mashauri hayo yenye kujenga, Daniel akavunjika moyo. “Nilitaka kujificha,” akumbuka. Kwa majuma kadhaa hakupata usingizi.

Kwa hiyo, kudai ukamilifu kwaweza kumzuia mtu asijifunze. Katika makala iliyokuwa katika kituo cha vijana kwenye Internet, msichana anayeitwa Rachel aliandika hivi: “Nilipoanza shule ya sekondari niliazimia kufanya vema. Sikuzote nilikuwa nikipata alama za “A” nami sikuona kwa nini hali iwe tofauti.” Lakini muda si muda Rachel akagundua kwamba somo la aljebra lilikuwa gumu naye akapata “tu” alama ya “B+” katika somo hilo. Rachel akumbuka kwamba “kila mtu aliiona kuwa alama nzuri lakini kwangu, . . . ilikuwa aibu. Nilianza kuhangaika na kuingiwa na wasiwasi . . . Niliogopa kumwomba mwalimu wangu anisaidie kwa sababu nilidhani kwamba ikiwa ningekubali kuwa nahitaji kusaidiwa, hilo lingemaanisha kwamba sikuelewa somo hilo. . . . Nyakati nyingine niliona ni afadhali kufa kuliko kushindwa.”

Kwa sababu ya kuogopa kushindwa, vijana fulani hata wamefikiria kujiua. Jambo la kupendeza ni kwamba, vijana wengi hawafikirii kuchukua hatua nzito kama hiyo. Lakini kama vile mtaalamu wa afya ya akili Sylvia Rimm anavyoona, huenda wakajaribu kuepuka kushindwa kwa kutofanya chochote. Kulingana na Rimm, baadhi ya wale ambao hudai ukamilifu “hawataki kazi yao isahihishwe na mwalimu, hawajivunii kazi yao, wanasahau kufanya migawo yao, nao hutoa udhuru.”

Kwa upande mwingine, huenda vijana wengine wakajitahidi kupita kiasi ili kufaulu. “Nilikuwa nikifanya kazi za shuleni mpaka usiku sana ili nihakikishe kwamba kila kitu kiko sawa kabisa,” akiri Daniel. Tatizo ni kwamba, kwa kawaida jitihada kama hizo zinazopita kiasi huathiri mafanikio. Mwanafunzi ambaye husinzia hawezi kufanya vema shuleni.

Basi, si ajabu kwamba kudai ukamilifu kunahusianishwa na kukasirika daima, kujidharau, kusumbuliwa na dhamiri, kutazamia mabaya, kuwa na matatizo ya kula na kushuka moyo. Hata hivyo, zaidi ya yote, kudai ukamilifu kunaweza kumdhuru mtu kiroho. Kwa mfano, Biblia huwaagiza Wakristo wawajulishe wengine imani yao. (Waroma 10:10; Waebrania 10:24, 25) Hata hivyo, kijana anayeitwa Vivian hakutaka kujibu katika mikutano ya Kikristo ili asikosee anapojibu. Mwanamke mchanga anayeitwa Leah alikuwa na hofu hiyohiyo. Anasema: “Nikisema jambo lisilofaa, wengine watanifikiria vibaya. Kwa hiyo mimi hunyamaza tu.”

Basi ni wazi kwamba, kutaka kuwa mkamilifu hakufai na kwaweza kudhuru. Na ikiwa una yoyote kati ya tabia zinazotajwa katika makala hii, huenda ukahitaji kubadili maoni yako. Makala ya wakati ujao itazungumzia jinsi unavyoweza kufanya hivyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 6 Uchunguzi mmoja uliofanywa katika shule moja ulionyesha kwamba asilimia 87.5 ya wanafunzi wenye vipawa walikuwa na mwelekeo wa kudai ukamilifu.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kuogopa kushindwa huwazuia vijana fulani wasimalize migawo yao

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kudai ukamilifu kunaweza kumfanya mtu ashuke moyo na kujidharau