Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Inafaa Kuwachukia Watu wa Jamii Nyingine?

Je, Inafaa Kuwachukia Watu wa Jamii Nyingine?

Maoni ya Biblia

Je, Inafaa Kuwachukia Watu wa Jamii Nyingine?

UNGEHISIJE kama ungeonwa kuwa mdanganyifu, mjeuri, mjinga, au mwovu kwa sababu tu wewe ni wa jamii fulani? * Bila shaka ungeudhika. Kwa kusikitisha, mamilioni ya watu wanaonwa hivyo. Isitoshe, tangu zamani watu wengi sana wasio na hatia wametendewa vibaya na hata kuuawa kwa sababu tu ya rangi yao au kwa sababu wao ni wa taifa tofauti. Ama kweli, vita vingi leo vimesababishwa na chuki ya kijamii. Hata hivyo, watu wengi wanaounga mkono vita hivyo hudai kwamba wanamwamini Mungu na Biblia. Baadhi yao hudai kwamba ubaguzi wa rangi utadumu milele na kwamba hiyo ndiyo asili ya wanadamu.

Je, Biblia inaunga mkono chuki ya kijamii? Je, inafaa kuwachukia watu wa utamaduni au rangi tofauti katika hali fulani? Je, kuna matumaini ya kuishi katika ulimwengu usio na chuki ya kijamii wakati ujao? Biblia inasema nini?

Walihukumiwa kwa Matendo Yao

Ukitazama kijuujuu jinsi Mungu alivyoshughulika na wanadamu zamani, unaweza kukata kauli kimakosa kwamba Mungu aliunga mkono chuki ya kijamii. Si Biblia ina masimulizi kadhaa yanayoonyesha jinsi Mungu alivyoangamiza makabila na mataifa mazima-mazima? Hiyo ni kweli, lakini ukiangalia vizuri, utaona kwamba Mungu aliwahukumu watu hao kwa sababu ya kupuuza sheria zake za uadilifu, bali si kwa sababu walikuwa wa jamii fulani.

Kwa mfano, Yehova Mungu aliwahukumu Wakanaani kwa sababu ya desturi zao zilizopotoka za ngono na ushirikina. Hata waliwateketeza watoto wao ili wawatoe kama dhabihu kwa miungu ya uwongo! (Kumbukumbu la Torati 7:5; 18:9-12) Hata hivyo, Wakanaani fulani walimwamini Mungu na wakatubu. Hivyo, Mungu hakuwaangamiza bali aliwabariki. (Yoshua 9:3, 25-27; Waebrania 11:31) Baadaye, hata mwanamke Mkanaani, Rahabu, akawa nyanya wa kale wa Mesiya aliyeahidiwa, Yesu Kristo.—Mathayo 1:5.

Sheria ambayo Mungu aliwapatia Waisraeli inaonyesha kwamba hana ubaguzi. Badala yake, yeye huwajali kikweli watu wote. Katika andiko la Mambo ya Walawi 19:33, 34, tunasoma amri hii ya Mungu yenye huruma kwa Waisraeli: “Na mgeni akikaa pamoja nawe katika nchi yako, usimdhulumu. Mgeni akaaye pamoja nawe atakuwa kama mzalia kwenu; mpende kama nafsi yako; kwa maana ninyi mlikuwa wageni katika nchi ya Misri; Mimi ndimi BWANA, Mungu wenu.” Amri kama hizo zinapatikana pia katika kitabu cha Kutoka na Kumbukumbu la Torati. Ni wazi kwamba Yehova hakuunga mkono chuki ya kijamii. Alitaka watu wa jamii zote waishi kwa amani.

Yesu Aliwahimiza Watu wa Jamii Zote Wapendane

Wakati Yesu alipokuwa duniani, kulikuwa na chuki fulani kati ya Wayahudi na Wasamaria. Katika pindi moja, Wasamaria walimfukuza Yesu kutoka katika kijiji chao kwa sababu tu alikuwa Myahudi aliyekuwa akielekea Yerusalemu. Ungehisije kama ungetendewa hivyo? Huenda wanafunzi wa Yesu walichochewa na chuki hiyo kati ya Wasamaria na Wayahudi walipomuuliza hivi: “Bwana, je, wataka tuambie moto uteremke kutoka mbinguni na kuwaangamiza?” (Luka 9:51-56) Je, Yesu aliruhusu maoni yao mabaya yamwathiri? Hata kidogo, badala yake aliwakemea na kwenda kwenye kijiji kingine kwa amani. Muda mfupi baadaye, Yesu alitoa kielezi cha Msamaria mwema. Kielezi hicho kilionyesha kwa mkazo sana kwamba jamii ya mtu haimfanyi kuwa adui. Ama kweli, aweza kuwa jirani mwema sana!

Jamii Mbalimbali Katika Kutaniko la Kikristo

Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alifanya wanafunzi hasa kutoka kwa watu wa taifa lake. Lakini baadaye alisema kwamba wengine pia wangekuwa wanafunzi wake. (Mathayo 28:19) Je, watu wa jamii zote wangekubaliwa? Ndiyo! Mtume Petro alisema hivi: “Kwa hakika nahisi kwamba Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Baadaye mtume Paulo alikazia jambo hilo kwa kusema waziwazi kwamba katika kutaniko la Kikristo watu wote ni sawa hata wawe wa jamii gani.—Wakolosai 3:11.

Jambo jingine linaloonyesha kwamba Mungu huwakubali watu kutoka kwa jamii zote lapatikana kwenye kitabu cha Biblia cha Ufunuo. Katika njozi iliyoongozwa na Mungu, mtume Yohana aliona “umati mkubwa . . . kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha” uliokolewa na Mungu. (Ufunuo 7:9, 10) ‘Umati huo mkubwa’ utakuwa msingi wa jamii mpya ya wanadamu itakayokuwa na watu wa jamii zote ambao wataishi kwa amani, wakiunganishwa na upendo wao kwa Mungu.

Kwa sasa, Wakristo hawapaswi kuwahukumu wengine kwa sababu wao ni wa jamii fulani. Badala ya kumwona mtu kuwa wa jamii fulani, ni jambo la haki na la upendo kuzingatia sifa zake kama Mungu anavyofanya. Bila shaka wewe pia unataka kuonwa hivyo. Yesu alihimiza hivi: “Kwa hiyo, mambo yote mtakayo watu wawafanyie nyinyi, lazima mwafanyie wao pia hivyohivyo.” (Mathayo 7:12) Kuishi bila chuki ya kijamii ni jambo lenye kufurahisha. Hilo huleta amani nyingi ya akili na amani pamoja na wengine. La muhimu hata zaidi, hiyo hutufanya tuwe kama Muumba wetu Yehova Mungu asiye na ubaguzi. Hiyo ni sababu kuu inayopaswa kutufanya tukatae katakata kuwachukia watu wa jamii nyingine!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Katika makala hii, neno “jamii” linamaanisha watu wa rangi, taifa, kabila, au utamaduni mmoja.