Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitu Kisichoweza Kuharibiwa na Dhoruba

Kitu Kisichoweza Kuharibiwa na Dhoruba

Kitu Kisichoweza Kuharibiwa na Dhoruba

NA WAANDISHI WA AMKENI! NCHINI UJERUMANI, AUSTRIA, MEXICO, NA KOREA

KATIKA mwaka wa 2002, hali mbaya ya hewa ilisababisha misiba katika nchi nyingi. Bara la Ulaya lilikumbwa na mafuriko makubwa. Kwingineko, Mexico ilikumbwa na tufani kali, na Korea ilipigwa na kimbunga. Ijapokuwa matukio hayo yalikuwa yenye kuhuzunisha, yaliimarisha upendo kati ya Wakristo wa kweli.

Baada ya mafuriko yaliyokumba bara la Ulaya mwaka wa 2002, aliyekuwa waziri mkuu wa Ujerumani Magharibi Helmut Schmidt aliulizwa kuhusu msaada ambao watu walioathiriwa walihitaji. Alijibu hivi: “Watu wanahitaji chakula, makao, pesa, na msaada wa kiroho.” Mashahidi wa Yehova wamewasaidia watu ambao wameathiriwa na dhoruba, kwa njia ya kimwili na ya kiroho. Ebu ona msaada waliotoa katika nchi ya Ujerumani, Austria, Mexico, na Korea.

Watu Walijitolea Kusaidia Nchini Ujerumani

Waliposikia kuhusu furiko lililokuwa likikaribia wengi wa Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani walijiunga na watu wengine kujitahidi kuyazuia maji yasifurike. Kathleen, mwenye umri wa miaka 19 anayeishi Dresden, anasema hivi: “Sikuweza kukaa kitako tu. Niliposikia kwamba watu wangepoteza mali zao zote, nilisukumwa kuwasaidia.”

Mashahidi nchini Ujerumani walianza kujipanga ili kutoa msaada kwa haraka. Kwa kuwa wao ni Wakristo, walihisi kwamba wana daraka hasa kuwasaidia ndugu na dada zao wa kiroho. Lakini walionyesha upendo kwa watu wengine pia. (Marko 12:31) Kwa hiyo, zaidi ya watu 2,000 waliojitolea walipangwa katika vikundi vyenye watu 8 hadi 12, na kila kikundi kilipewa kazi maalumu katika eneo lililokuwa limeathiriwa na furiko. Kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Selters, Ujerumani, namba 13 tofauti-tofauti za simu zilitengwa ili kupokea simu kutoka kwa maelfu ya watu waliouliza kuhusu msiba huo na waliotaka kusaidia.

Ronnie na Dina ni wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, ambao hutumia maisha yao kuwasaidia marafiki na watu wenzao kujifunza kweli za Biblia. Waliposikia kuhusu furiko lililokuwa linakaribia, kwanza walikwenda Dresden ili kusaidia kuokoa majengo ya kale ya jiji hilo. Baada ya furiko, Ronnie na Dina walijiunga na Mashahidi wengine kusafisha Jumba la Ufalme la Freital, ambalo lilikuwa limefurikwa na maji machafu. Kisha walianza kuwasaidia watu walioishi katika ujirani. Mtu mmoja mwenye mkahawa karibu na Jumba la Ufalme alifurahi sana Mashahidi walipoondoa takataka na matope kutoka katika vyumba vyake vya chini ya ardhi na ghorofa ya chini.

Siegfried na Hannelore wanaishi katika kijiji cha Colmnitz, umbali wa kilometa 40 kusini-magharibi ya Dresden. Kijito kinachopita katikati ya kijiji hicho kilifurika sana, na maji yaliingia katika nyumba na bustani yao. Baada ya maji kupungua, majirani walishangaa kuwaona Mashahidi 30 hivi, ambao si wakazi wa eneo hilo, waliokuja kusafisha nyumba ya Siegfried na Hannelore. Kisha Mashahidi hao walianza kusafisha bustani za majirani wa Siegfried na Hannelore. Wanakijiji kadhaa waliwauliza ni nini kilichowasukuma kusafiri kilometa 100 ili kuwasaidia watu ambao hawakuwafahamu. Hivyo, Mashahidi walikuwa na nafasi ya kutumia Biblia ili kuwafariji watu wa Colmnitz walioathiriwa na msiba huo.

Sehemu zilizo karibu na mji wa Wittenberg pia zilifurikwa. Frank na Elfriede, wenzi wa ndoa ambao ni Mashahidi, walifanya kazi pamoja na majirani wao kwa siku kadhaa kabla ya furiko. Walijaza magunia kwa mchanga na kuyapanga kwenye kingo za mto ili kuziimarisha. Baada ya maji kupungua Frank na Elfriede waliwatembelea watu walioathiriwa na furiko hilo ili kuwapelekea chakula na kuwafariji. Frank anasema hivi: “Bibi mmoja hakuweza kuamini kwamba wageni walimletea chakula bila kutoza malipo. Alituambia kwamba hakuna yeyote wa kanisa lake aliyekuwa amemtembelea. Na lile shirika lililokuwa limemletea chakula lilikuwa limetoza malipo kwa kila mlo. Watu walishangaa kuwaona Mashahidi wa Yehova wakija na chakula motomoto badala ya vitabu vya Biblia.”

Msaada Watolewa Haraka Nchini Austria

Furiko lilisababisha uharibifu mkubwa pia katika nchi jirani, Austria. Halmashauri tatu za kutoa msaada zilianzishwa ili kusimamia jitihada za kutoa msaada. Majumba ya Ufalme matatu yaliyokuwa yameharibika vibaya yalirekebishwa kwanza. Vilevile, familia 100 hivi za Mashahidi ziliathiriwa na mafuriko hayo, na nyumba 50 za Mashahidi ziligharikishwa. Baadhi yao walipoteza mali zao zote isipokuwa nguo walizokuwa wamevalia. Ndugu kwenye ofisi ya tawi nchini Austria walijulisha makutaniko ya karibu na hazina ya msaada ilianzishwa. Dola 34,000 za Marekani zilikuwa zimechangwa kufikia mwezi wa Septemba.

Mama mmoja aliandika hivi: “Mwana wangu mwenye umri wa miaka minane alikuwa amehifadhi dola 14 hivi. Hata hivyo, aliposikia kwamba ndugu wengine walikuwa wamepoteza mali zao zote, alikuwa tayari kuchanga pesa hizo zote kwa ajili ya hazina ya msiba.”

Halmashauri za Ujenzi za Mkoa, ambazo kwa kawaida husimamia ujenzi wa Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova, zilipanga vikundi vya watu wasaidie kurekebisha nyumba zilizokuwa zimeharibiwa na mafuriko. Mtu mmoja alisema hivi: “Magazeti yanapaswa kusambaza habari kuhusu kazi yenu.” Hata wengine walibadili maoni yao kuwahusu Mashahidi wa Yehova. Shahidi mmoja mzazi anasema hivi: “Hadi leo hii, watoto wangu ambao si Mashahidi, walikataa kunisikiliza nilipojaribu kuwaelezea kuhusu imani yangu. Lakini sasa wananisikiliza kwa mara ya kwanza!”

Pia wengi ambao si Mashahidi walisaidiwa. Kwa mfano, mwanamke mmoja alivutiwa sana Shahidi mmoja alipokuja nyumbani kwake saa moja na nusu asubuhi na kumwuliza ikiwa anahitaji msaada. Ilimbidi mwanamke huyo ahame kwa sababu tayari maji yalikuwa yakiingia katika nyumba yake. Hata hivyo, aliporudi, alipata barua ndogo kutoka kwa Mashahidi hao kwenye lango la bustani yake. Barua hiyo ilisema hivi: “Ukihitaji msaada, tuite mara moja.” Mashahidi walisaidia kuondoa takataka na matope kutoka katika nyumba na bustani yake.

Mashahidi 100 walikwenda hadi mji wa Au ili kuwasaidia Mashahidi wa huko na majirani wao. Wale walioongoza kazi hiyo walitembelea wakazi wa eneo hilo na kuwauliza ikiwa wangehitaji msaada. Watu walishangaa kuwaona Mashahidi wakija na vyombo vya kuondoa maji na vya usafi, kama vile pampu za kusukuma maji, fagio, na vyombo vya kuchimbia. Kazi ambayo ingaliwachukua wenye nyumba juma zima kumaliza, ilimalizika kwa saa chache tu. Watu walitazama wakitokwa na machozi.

Wapata Mashahidi 400 walihusika katika kazi ya kutoa msaada, wengine wakifanya kazi usiku kucha. Watu walivutiwa sana kujionea jinsi Ukristo wa kweli ulivyo na nguvu.

Tufani ya Isidore Yakumba Mexico

Chanzo cha tufani inayoitwa Isidore kilikuwa dhoruba kaskazini ya Venezuela. Dhoruba hiyo ikawa tufani yenye nguvu ya wastani, ikapiga Rasi ya Yucatán, nchini Mexico, Septemba 22, 2002. Tufani hiyo yenye mwendo wa kilometa 190 kwa saa, pamoja na mvua kubwa, ilisababisha uharibifu mkubwa uliowahi kukumba majimbo ya Yucatán na Campeche, na iliathiri vilevile jimbo la Quintana Roo kwa kadiri fulani. Katika jimbo la Yucatán nyumba 95,000 ziliharibiwa vibaya na watu 500,000 waliathiriwa.

Mashahidi wa Yehova walikuwa na matokeo mazuri sana katika jitihada zao za kutoa msaada huko Yucatán hivi kwamba gazeti moja la Mexico kaskazini lilikuwa na kichwa hiki kwenye ukurasa wa mbele: “Mashahidi wa Yehova Wajitolea Kusaidia.” Halmashauri ya kutoa msaada ilipangwa mapema kabla ya dhoruba kufika. Mipango ya dharura ilifanywa ili kuandaa makao ya muda kwa mamia ya Mashahidi wa eneo hilo. Makutaniko ya karibu yalichanga pesa. Nguo, dawa, na zaidi ya kilogramu 22,000 za chakula ziligawiwa watu walionusurika katika dhoruba hiyo, kutia ndani watu wengi ambao si Mashahidi. Wazee wa huko waliombwa kuwatembelea na kuwafariji watu walioathiriwa na tufani ya Isidore.

Baada ya dhoruba, halmashauri za kutoa msaada za eneo hilo zilipangwa ili kutafuta Mashahidi waliokuwa wamepotea. Wengi walipatikana kichakani na mahali penginepo na walikuwa wamekosa chakula na maji ya kunywa kwa siku tatu. Katika maeneo fulani maji yalikuwa mengi hivi kwamba yalifunika taa za barabarani! Kwa hiyo, mashua zenye injini zilitumiwa kutafuta watu, kuwaletea chakula, na kuwapeleka hadi maeneo yenye usalama.

Watu wenye mamlaka wa eneo hilo waliwapa Mashahidi mashua na vifaa vingine ili waweze kufikia maeneo ambayo watu wengine waliogopa kwenda. Mwanzoni, afisa mmoja wa jeshi aliwakataza Mashahidi wasiende sehemu hizo hatari ili kuwatafuta watu. Hata hivyo, alipoona ujasiri wao, alisema hivi: “Nina hakika kwamba nyinyi mngetumia hata helikopta ili kuwaokoa watu wenu kama ingehitajika. Mnaweza kutumia magari yetu kwenda mahali popote mnapotaka.”

Mwenye duka mmoja alitaka kujua ni kwa nini Mashahidi fulani walinunua chupa nyingi sana za maji. Walieleza kwamba maji hayo yalikuwa kwa ajili ya ndugu zao wa kiroho na wengine wenye uhitaji. Mtu huyo aliamua kuwapa bila malipo chupa zote za maji alizokuwa nazo dukani. Kesho yake pia alichanga kiasi kikubwa cha maji. Mnunuzi katika duka lingine alitaka kujua ni kwa nini Mashahidi walinunua chakula kingi sana. Alipoelezwa kwamba chakula hicho kilinunuliwa kwa ajili ya watu walioathiriwa na mafuriko aliwapa mchango ili wanunue chakula zaidi.

Ijapokuwa karibu familia 3,500 za Mashahidi zilipoteza mali kwa sababu ya kimbunga cha Isidore, hakuna Shahidi wa Yehova aliyepotea au kufa. Hata hivyo, kwa sababu nyumba 331 za Mashahidi zilikuwa zimeharibika kabisa au kwa kadiri fulani, nyumba mpya zilihitaji kujengwa na nyingine kurekebishwa. Mashahidi wanaojua kazi ya ujenzi walitembelea kila nyumba na Jumba la Ufalme lililoharibika ili kukadiria madhara. Hadi leo, yapata nyumba 258 zimerekebishwa na nyumba mpya 172 zimejengwa. Pia, Majumba ya Ufalme 19 yanajengwa upya kwa wakati huu.

Mzee mmoja wa kutaniko katika jimbo la Yucatán alisukumwa kusema hivi: “Nimesoma katika vitabu vyetu juu ya msaada unaotolewa katika nchi nyingine. Hata hivyo, kujionea jambo hilo ni tofauti sana. Imani yangu na ile ya ndugu wengi imeimarishwa kwa kuona jinsi tengenezo la Yehova na ndugu zetu wapendwa wametuhangaikia na kutusaidia bila kukawia.”

Mwanamke mmoja alisema hivi: “Ningalifurahi kama kanisa langu lingalitoa msaada kama nyinyi Mashahidi.” Mwanamke mwingine aliyesaidiwa na Mashahidi alisema hivi: “Mashahidi wa Yehova waliokoa maisha yetu. Kwa upendo walihatarisha maisha yao ili kutuokoa nyumba yetu ilipofurikwa.”

Kimbunga Chapiga Korea

Kimbunga kinachoitwa Rusa kiliathiri sehemu kubwa ya Korea tarehe 31 Agosti, na Septemba 1, 2002. Mzee mmoja wa kutaniko anayeitwa Song-pil Cho, alisema hivi: “Ilikuwa kana kwamba nimesimama chini ya mfereji. Iliendelea kunyesha na kunyesha na kunyesha.” Zaidi ya milimeta 870 za mvua zilikunya kwa muda usiozidi saa 24. Haijawahi kunyesha mvua kubwa hivyo kwa siku moja katika eneo hilo.

Gazeti la The Korea Herald linasema kwamba nyumba 28,100 na ekari 210,000 za mashamba zilifurikwa kotekote nchini. Watu 70,000 hivi walilazimika kuhama. Mifugo 301,000 ilikufa, meli 126 zikazama, na mamia ya nguzo za umeme zikaanguka kwa sababu ya kimbunga hicho. Zaidi ya watu 180 walikufa au kupotea. Miongoni mwao walikuwa Mashahidi wa Yehova wawili.

Kama ilivyokuwa huko Ulaya na Mexico, Mashahidi wa Yehova nchini Korea walitenda kwa haraka. Mashahidi kotekote nchini Korea walitoa vitu vingi, kama vile nguo, mablanketi, na vitu vingine, ili kuwasaidia watu walioathiriwa. Lakini baadhi ya ndugu na dada waliishi katika maeneo ambayo hayakuweza kufikiwa. Barabara na madaraja yalikuwa yameharibiwa. Hakukuwa na umeme na simu haikufanya kazi. Kwa hiyo, watu walipangwa waende kwa miguu kupeleka msaada. Song-pil Cho, ambaye alikuwa katika kikundi kimoja, anasema hivi kuhusu eneo moja ambapo walipeleka msaada: “Madaraja saba na sehemu kubwa za barabara zilikuwa zimeharibika. Hatimaye tulipofika mjini tuliona nyumba zilizokuwa zimeharibika kotekote. Kulikuwa na uvundo, na mizoga ya wanyama ilionekana kila mahali. Lakini tulifurahi sana tulipokutana na ndugu na dada sita Wakristo! Walikuwa wamepoteza mali zao zote, lakini wote walikuwa hai na salama.”

Kwa kweli, Mashahidi wa Yehova walikuwa tayari kushughulikia msiba huo. Kwa kuwa mafuriko ni ya kawaida katika majira ya pepo za msimu, Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa katika eneo la Seoul ilikuwa imeanza kupanga utoaji wa msaada kwa ajili ya misiba iliyotarajiwa. Tangu mwaka wa 1997, imepanga kuwazoeza watu wanaojitolea kila mwaka, ili wawe tayari kusaidia wakati wa dharura.

Watu waliojitolea kusaidia waliwasili pwani ya mashariki ya jiji la Kangnŭng Septemba 2, na kupanga kituo kikuu cha kutoa msaada kwenye Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova. Jambo muhimu zaidi lilikuwa nini? Kuwaandalia watu walionusurika maji safi. Wakati wa mafuriko makubwa mara nyingi mabomba ya maji hutoboka, na maji ya mtoni ni machafu sana. Halmashauri hiyo ilipanga malori makubwa yaliyobeba maji yatumwe hadi maeneo yaliyoathiriwa.

Maji yanapopungua baada ya mafuriko, kila kitu huwa kimefunikwa kwa matope yanayonuka vibaya sana. Hata hivyo, njia nzuri ya kusafisha nyumba imebuniwa. Kwa kuwa karibu nyumba zote katika eneo hilo zimejengwa kwa saruji, zinaweza kusafishwa kwa kuondoa karatasi za ukutani na mazulia ya plastiki, kisha zikasafishwa kwa kutumia maji yanayotoka kwa nguvu.

Mafuriko huharibu vifaa vyote vya umeme. Hata hivyo, vitu kama vile friji na vyombo vya kupasha nyumba joto vikibomolewa na mafundi wa umeme, na kusafishwa kabisa, kukaushwa, na kisha kuunganishwa tena kabla ya muda mrefu kupita, mara nyingi hufanya kazi tena. Ndugu katika Halmashauri ya Ujenzi hufanya kazi hiyo. Vyombo vya kupasha nyumba joto ambavyo havijaharibika hutumiwa kukausha nyumba. Kazi ya kukausha nyumba huchukua kati ya majuma mawili na majuma matatu.

Nguo na mablanketi yanahitaji pia kuoshwa upesi ili yasiharibike. Mashahidi wa Yehova wa kutaniko moja walisaidia kukusanya nguo chafu za ndugu zao Wakristo. Ilikuwa vigumu sana kufua nguo hizo zenye matope mengi na iliwabidi kuzifua kwa mkono mtoni katika maji yaliyokuwa baridi sana. Mwandishi mmoja wa habari aliposikia kuhusu kazi hiyo iliyofanywa kwa upendo, aliweka picha kubwa ya Mashahidi wanaofua katika gazeti la eneo hilo.

Mafuriko mabaya huko Ulaya, Amerika Kaskazini, na Asia yaliharibu nyumba na mali, na watu wengi sana wasio na hatia wakafa. Ijapokuwa matukio kama hayo ni yenye kuhuzunisha sana, ni ya kawaida katika siku “za mwisho” za ulimwengu huu, ambazo ni “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Misiba kama hiyo inaweza kutukumbusha jambo hili: Wakristo wa kweli wanawapenda Wakristo wenzao na watu wenzao. Upendo huo usio na ubinafsi hauwezi kuharibiwa na dhoruba yoyote ile.

[Picha katika ukurasa wa 10]

UJERUMANI—Nyumba iliyoharibiwa na dhoruba

[Picha katika ukurasa wa 11]

UJERUMANI—Zaidi ya watu 2,000 walijitolea kutoa msaada upesi

[Picha katika ukurasa wa 12]

AUSTRIA—Jumba la Ufalme huko Ottensheim linarekebishwa

Kushoto: Kikundi cha watu waliojitolea wanarudi baada ya kuwasaidia Mashahidi na watu ambao si Mashahidi katika eneo la Au

[Picha katika ukurasa wa 13]

MEXICO—Kulia: Halmashauri ya kutoa msaada inawaandalia maji ya kunywa watu walionusurika dhoruba

Chini: Kujenga nyumba mpya

[Picha katika ukurasa wa 15]

KOREA—Kuanzia kushoto hadi kulia: Sehemu ya jiji iliyofurika; kusafisha nyumba kwa maji yanayotoka kwa nguvu; kufua nguo katika mto ulio karibu