Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Misiba ya Hali ya Hewa Itakoma!

Misiba ya Hali ya Hewa Itakoma!

Misiba ya Hali ya Hewa Itakoma!

“MWANADAMU WA KISASA ameidharau dunia kwa sababu ya pupa yake ya kupata raha na pesa, na kuharakisha mambo.” Hivyo ndivyo jalada la kitabu 5000 Days to Save the Planet (Siku 5000 za Kuokoa Dunia) linavyosema. Tumeathiriwa na matokeo ya pupa ya mwanadamu. Na haidhuru kama dhana za kuongezeka kwa joto duniani ni za kweli au la, ni jambo la hakika kwamba mwanadamu anaharibu sayari yetu maridadi. Tumaini letu liko tu katika ahadi ya Biblia inayosema kwamba Mungu ‘atawaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia.’—Ufunuo 11:18.

Mungu ataharibu mfumo mwovu wa utawala wa wanadamu na kuleta mfumo mpya kabisa. Hebu kidogo. Kabla hujasema kwamba huo ni upuuzi wa kidini tu, fikiria jambo hili: Ni nani anayependezwa na dunia kuliko Muumba wake? Si dunia ni mali yake? Kwenye Isaya 45:18, Biblia inaunga mkono jambo hilo inaposema kwamba Yehova “ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu.” Ili kutimiza kusudi hilo, Mungu ataingilia kati, naye ana uwezo wa kufanya hivyo.

Mungu atafanya hivyo kwa kuleta serikali, au ufalme mpya, ili itawale dunia. Wakristo wanaposali ile inayoitwa Sala ya Bwana na kusema, “Ufalme wako uje,” wao huomba serikali hiyo ianze kutawala dunia. (Mathayo 6:9, 10) Ufalme wa Mungu, au serikali yake, utatenda kupatana na mizunguko ya asili ya dunia. Hivyo, utaweza kurekebisha maeneo ya dunia ambayo yameharibiwa na uchafuzi na uharibifu wa mazingira. Isaya 35:1, 6 inasema: ‘Jangwa litachanua maua kama waridi. Maana katika nyika maji yatabubujika; na vijito jangwani.’

Hadi Mungu Atakapoingilia Kati

Baada ya mafuriko ya mwaka wa 2002, Helmut Schmidt, aliyekuwa waziri mkuu wa Ujerumani Magharibi, aliandika hivi: “Hakuna mtu anayeweza kuzuia mafuriko yasivunje kingo za mabwawa. Misiba huendelea kutokea.” Hilo ni kweli. Hali mbaya ya hewa inaposababisha misiba, wanadamu hawana lingine la kufanya ila kustahimili hali hiyo. Ingawa misiba hiyo husababisha shida nyingi, inaweza kuleta faida pia. Inaweza kuwachochea watu kuonyesha kwamba wanawapenda na kuwajali majirani zao. (Marko 12:31) Kwa mfano, mafuriko yaliyotukia huko Ulaya yaliwachochea watu wengine kufanya hivyo. Gazeti moja liliandika hivi: “Watu wenye bidii wamekuja kutoka sehemu zote za Ujerumani ili kutoa msaada. Hii ndiyo kazi kubwa ya kujitolea iliyowahi kufanywa tangu wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu.”

Mashahidi wengi wa Yehova walikuwa miongoni mwa watu hao waliosaidia. Makala inayofuata inaeleza kazi ya kutoa msaada iliyofanywa na Mashahidi katika nchi nne zilizokumbwa na dhoruba kali. Matendo ya Wakristo hao yanaonyesha wazi jinsi maisha yatakavyokuwa chini ya utawala wa Mungu, wakati ambapo kutakuwa na upendo na udugu wala si pupa na ubinafsi.—Isaya 11:9. *

Wakristo wanaweza kufarijiwa na ahadi ambayo Mungu aliwapa Waisraeli wa kale: ‘Nitawapa mvua ya nchi yenu kwa wakati wake, mvua ya masika, na mvua ya vuli, upate kuvuna nafaka yako, na divai yako, na mafuta yako.’ (Kumbukumbu la Torati 11:14) Wale watakaopendelewa kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu watafurahia utimizo wa ahadi hiyo katika ulimwengu usio na misiba inayosababishwa na hali ya hewa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ikiwa ungependa kujifunza zaidi kuhusu ahadi ya Biblia ya utawala wa Ufalme, tafadhali wasiliana na Mashahidi wa Yehova mahali unapoishi au uwaandikie wachapishaji wa gazeti hili.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Hali Kamilifu ya Hewa

Katika ulimwengu mpya wa Mungu, hakuna mtu atakayehofu kwamba nyumba yake au mazao yake yataharibiwa na dhoruba kali. (2 Petro 3:13) Biblia inaonyesha wazi kwamba Mungu na Mwana wake, Yesu Kristo, wanaweza kudhibiti kabisa hali ya hewa. Hebu ona maandiko yafuatayo.

Mwanzo 7:4: “Baada ya siku saba nitainyeshea dunia mvua, siku arobaini mchana na usiku.”

Kutoka 14:21: “BWANA akaifanya bahari irudi nyuma kwa upepo wa nguvu utokao mashariki, usiku kucha, akaifanya bahari kuwa nchi kavu, maji yakagawanyika.”

1 Samweli 12:18: “Samweli akamwomba BWANA, naye BWANA akapeleka ngurumo na mvua siku ile; nao watu wote wakamwogopa BWANA sana, na Samweli pia.”

Yona 1:4: “BWANA alituma upepo mkuu baharini, ikawa tufani kubwa baharini, hata merikebu ikawa karibu na kuvunjika.”

Marko 4:39: “Ndipo [Yesu, akiwa amepewa nguvu na Mungu] akajiamsha mwenyewe akakemea upepo na kuiambia bahari: ‘Usu! Nyamaa!’ Na upepo ukapunguka, kukawa shwari kubwa.”

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Katika ulimwengu mpya wa Mungu, hatutaogopa hali mbaya za hewa