Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tahiti na Jitihada za Kutafuta Paradiso

Tahiti na Jitihada za Kutafuta Paradiso

Tahiti na Jitihada za Kutafuta Paradiso

Meli ilikuwa imerushwa huku na huku kwa siku nyingi na mawimbi ya Bahari ya Pasifiki. Mabaharia walikuwa wamefanya kazi ya jasho katika jua kali, na bila shaka walikuwa wamechukizwa na divai kali, maji yenye harufu mbaya, na chakula kilichokuwa kimeoza. Ghafula, mtu alipaaza sauti: “Nchi kavu! Nchi kavu inaonekana upande wa kushoto!” Kisiwa kilionekana kwa mbali sana. Saa chache baadaye hakukuwa na shaka yoyote kwamba hicho kilikuwa kisiwa.

Tangu kisiwa cha Tahiti kilipovumbuliwa kwa mara ya kwanza na Wazungu, watu wamekiona kuwa “paradiso.” Mvumbuzi Mfaransa wa karne ya 18, Louis-Antoine de Bougainville, aliyeongoza safari ya uvumbuzi iliyofafanuliwa mwanzoni, aliandika hivi baadaye: “Nilidhani nimeingia katika bustani ya Edeni.” Miaka mia mbili baadaye wageni bado hupenda kutembelea Tahiti. Kama wale waliokuja zamani, wengi leo pia huja kutafuta paradiso.

Lakini kwa nini mwanadamu huvutiwa sana na wazo la paradiso? Na kisiwa cha Tahiti kilipataje kuonwa kuwa paradiso? Ili kujibu swali hilo, tuchunguze jinsi hali ilivyokuwa mwanadamu alipoumbwa.

Paradiso Iliyopotea

Neno “paradiso” linatuvutia sana kwa sababu tuliumbwa kuishi katika Paradiso. Biblia inasema kwamba Mungu aliwabariki wazazi wetu wa kwanza kwa kuwapa “paradiso,” yaani, bustani nzuri sana. (Mwanzo 2:8) Yaelekea, bustani hiyo ilikuwa sehemu ya eneo lililoitwa Edeni, jina ambalo linamaanisha “Raha.” Ijapokuwa wasomi wa siku hizi huona Edeni kuwa hekaya, Biblia inaonyesha kwamba ilikuwa mahali halisi, na inataja mambo hususa kuhusu sehemu ilipokuwa. (Mwanzo 2:10-14) Leo, haijulikani mahali ambapo Mto Pishoni na Gihoni inayotajwa katika simulizi hili ilipokuwa. Kwa hiyo hatujui mahali hasa ambapo bustani hiyo ilikuwa.

Wazazi wetu wa kwanza walimwasi Mungu na hivyo kupoteza Paradiso. (Mwanzo 3:1-23) Hata hivyo, mwanadamu ameshindwa kuondoa tamaa ya kuishi katika paradiso. Hata hekaya za nchi nyingi zinataja mambo yanayofanana na paradiso inayosimuliwa katika Biblia. Kwa mfano, Wagiriki walikuwa na hekaya kuhusu Zama za Ustawi, yaani, muhula mkamilifu ambapo watu waliishi maisha ya raha mustarehe.

Wengi wametafuta bustani ya Edeni iliyopotea. Baadhi ya watu waliitafuta bustani hiyo huko Ethiopia, wasiipate. Hata hekaya moja inasema kwamba kasisi mmoja aliyeitwa Brendan aliyeishi katika miaka ya 500 W.K., alipata paradiso katika kisiwa kimoja katika sehemu ya kusini-magharibi ya Bahari ya Atlantiki. Hekaya nyingine zilisema kwamba paradiso imefichwa kwenye mlima mrefu. Kwa sababu ya kuchanganyikiwa na hekaya hizo, mvumbuzi mashuhuri Christopher Columbus alilalamika hivi: “Sijapata wala sijasoma maandishi katika lugha ya Kilatini au Kigiriki yanayoonyesha kwa hakika mahali ambapo paradiso inapatikana duniani.” Hatimaye, alisadikishwa kwamba ilikuwako kwenye upande wa kusini wa dunia.

Baada ya safari yake ya tatu hadi Ulimwengu Mpya (mabara ya Amerika), Columbus alisema hivi: “Yaonekana nchi hiyo ndiyo paradiso hapa duniani, kwa kuwa inalingana na maelezo ya watakatifu na wasomi wa dini ambao nimewataja.” Hata hivyo, Ulimwengu huo Mpya, haukuwa paradiso kama Columbus alivyowazia.

Hekaya za Baadaye za Jamii Kamilifu

Hata hivyo, baadhi ya wasomi hawakuvunjika moyo. Badala ya kutafuta njia ya kurudi katika bustani ya Edeni, walibuni wazo la paradiso ya wakati ujao iliyotengenezwa na mwanadamu. Waandishi walianza kubuni hadithi kuhusu jamii “kamilifu,” jambo ambalo liliwavutia watu walioishi katika jamii zenye ufisadi mwingi. Hata hivyo, jamii hizo za kuwaziwa hazikufanana na bustani ya Edeni. Badala ya kuwazia maisha yenye uhuru katika bustani isiyo na mipaka, watu hao waliona paradiso kuwa majiji yenye mpango wa hali ya juu. Kwa mfano, katika miaka ya 1500, mwanasiasa Mwingereza Bwana Thomas More alisimulia kuhusu safari ya kuwaziwa hadi nchi aliyoita Utopia. Neno hilo la Kiingereza linamaanisha “Mahali pa Kuwaziwa.”

Waandishi walioishi baadaye walipanua mawazo ya More kwa kuyaongezea mawazo yao. Waandishi wengi wa Ulaya waliandika kuhusu “jamii kamilifu” katika karne zilizofuata. Tena jamii hizo “kamilifu” hazikuwa bustani za raha hata kidogo. Katika jamii hizo furaha ilikuwa iletwe kwa kudhibiti watu kabisa. Lakini jambo hilo lilizuia uhuru na ubunifu wa watu. Hata hivyo, profesa wa historia, Henri Baudet, alisema kwamba hekaya hizo zilionyesha “tamaa isiyotoshelezwa ya kupata maisha bora . . . na jamii yenye uadilifu.”

Hekaya Kuhusu Tahiti

Bahari za Kusini zilikuwa eneo la mwisho la dunia kuvumbuliwa na hivyo jitihada za mwisho za kutafuta paradiso iliyopotea zilielekezwa huko katika miaka ya 1700. Hata hivyo, Bougainville alipoanza safari yake kuelekea Bahari ya Pasifiki mnamo Desemba 1766, kusudi lake lilikuwa hasa kuvumbua, kutwaa makoloni mapya, na kupanua biashara.

Baada ya kusafiri kwa miezi mingi baharini, Bougainville alifika Tahiti. Alikuwa ameshindwa kufika pwani ya visiwa vile vingine ambavyo alikuwa ameviona kwa sababu ya miamba ya tumbawe. Kwenye kisiwa cha Tahiti alipata bandari nzuri. Mabaharia waliokuwa wamechoka sana walikuta watu wakarimu na vitu vingi vya kuwatosheleza. Kwa maoni ya mabaharia hao, kisiwa hicho kilikuwa bora kuliko paradiso. Kisiwa cha Tahiti kilikuwa chenye joto na mambo mengi yalifanana na zile jamii kamilifu za hadithi zilizobuniwa.

Kwa mfano, hadithi kuhusu jamii kamilifu zilihusu visiwa, na Tahiti kilikuwa kisiwa vilevile. Isitoshe, mandhari ya kisiwa hicho yalikuwa kama ya paradiso. Kwenye kisiwa hicho kuna mamia ya mito yenye maporomoko, mimea inayositawi, na mandhari yenye kuvutia sana. Ni kana kwamba mimea ilisitawi bila kulimwa. Mbali na mandhari nzuri, hali ya hewa huko Tahiti ilikuwa nzuri kwa afya na hakukuwa na hatari zozote ambazo ni za kawaida katika nchi zenye joto. Katika kisiwa hicho hakukuwa na nyoka, wadudu hatari, wala volkeno ambazo zingeweza kulipuka.

Kisha, wenyeji walikuwa watu warefu wenye sura nzuri na wenye afya. Mabaharia waliokuwa wamepoteza meno yao na ambao fizi zao zilikuwa zimevimba kwa sababu ya kiseyeye, walivutiwa na meno meupe ya watu wa Tahiti. Wenyeji walikuwa pia wachangamfu; mabaharia walivutiwa mara moja na ukarimu wao. Ilionekana pia, angalau kwa kuangalia mambo kijuujuu kwamba watu wote walikuwa sawa. Hilo lilikuwa jambo moja la msingi katika hadithi za jamii kamilifu. Hakukuwa na umaskini. Watu wa Tahiti hawakuwa na sheria kuhusu mahusiano ya kingono. Mabaharia walifanya uasherati pamoja na wanawake warembo wa Tahiti.

Ndiyo, kwa maoni ya Bougainville na mabaharia wake kisiwa cha Tahiti kilikuwa bustani ya Edeni. Kwa hiyo, Bougainville aliondoka kwenye kisiwa hicho akiwa na tamaa ya kueleza kuhusu paradiso aliyokuwa amevumbua. Alipomaliza safari yake ya miaka mitatu ya kuzunguka dunia, aliandika kitabu kuhusu safari yake. Kitabu hicho kilishinda vitabu vingine kwa mauzo na kilikuwa chanzo cha hekaya iliyosema kwamba kisiwa cha Tahiti ni kisiwa kikamilifu kwa kila njia. Paradiso ilikuwa imepotea, lakini kisiwa cha Tahiti kilikuwa paradiso kwa wakati huo!

Hatari za Kuamini Hekaya

Hata hivyo, hekaya hazielezi jinsi mambo yalivyo. Kwa mfano, watu wa Tahiti waliugua na kufa kama watu wengine. Badala ya watu wote kuwa sawa, waliishi katika jamii ambamo watu wenye vyeo waliwaonea wengine, nyakati nyingine kwa ukali sana. Walipigana vita vya kikabila na kutoa wanadamu kama dhabihu. Kama ilivyo katika jamii zote, si watu wote wa Tahiti waliokuwa warembo au wenye sura nzuri. Na mwanahistoria K. R. Howe anasema kwamba huenda wanawake ambao watu wa Bougainville waliwapata walikuwa “wameamriwa kufanya uasherati,” ili kuwastarehesha wale wavamizi.

Hata hivyo, hekaya kuhusu “paradiso iliyopatikana” ilienea. Waandishi na wasanii, kama vile mchoraji Mfaransa Paul Gauguin, walimiminika huko. Michoro ya Gauguin ya maisha ya Tahiti ilifanya watu wavutiwe na kisiwa hicho hata zaidi. Matokeo yalikuwa nini? Hekaya hiyo ilifanya watu wawe na maoni finyu kuhusu kisiwa hicho na wakazi wake. Baada ya kurudi nyumbani, kwa kawaida wageni waliambiwa, “Tueleze kuhusu wasichana wa Tahiti.”

Je, Kuna Matumaini ya Kupata Paradiso Tena?

Katika miaka ya majuzi kisiwa cha Tahiti kimekabili magumu mengine. Tufani zilikumba kisiwa hicho mapema katika miaka ya 1980 na kuharibu miamba yake ya tumbawe. Hata hivyo, mwanadamu ndiye ambaye ameleta madhara makubwa zaidi. Miradi ya ujenzi imesababisha mmomonyoko wa ardhi na uchafuzi. Mtaalamu wa kushughulikia takataka, Donna Leong, anasema hivi: “Biashara ya utalii husababisha uchafuzi mwingi sana. . . . Ikiwa uchafuzi wa mazingira hautashughulikiwa, kisiwa cha Tahiti na vile visiwa vingine havitaendelea kuwa na mimea na wanyama wengi, na havitakuwa na maji ya samawati nyangavu.”

Hata hivyo, tumaini la paradiso bado lipo. Yesu Kristo mwenyewe aliahidi mkosaji aliyetubu hivi: “Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso”! (Luka 23:43) Yesu hakusema juu ya jamii kamilifu yenye sheria kali, inayoelezwa katika hekaya, bali alisema kuhusu paradiso ya duniani pote itakayotawaliwa na serikali ya mbinguni. * Mashahidi wa Yehova zaidi ya 1,700 wanaoishi kisiwani Tahiti wanatarajia Paradiso hiyo. Wanajitolea kutumia wakati wao kuwaeleza watu kuhusu tumaini hilo. Kwa maana, ijapokuwa kisiwa cha Tahiti kinafanana na paradiso kwa njia nyingi, hakiwezi kulinganishwa na Paradiso ya duniani pote ambayo Mungu ataleta hivi karibuni. Jitihada ya kutafuta Paradiso hiyo si ya bure.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 24 Ukitaka kupata habari zaidi juu ya ahadi za Mungu kuhusu Paradiso ona kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Kisiwa cha Tahiti kilionekana kuwa paradiso

[Hisani]

Mchoro wa William Hodges, mwaka wa 1766

Yale Center for British Art, Paul Mellon Collection, USA/Photo: Bridgeman Art Library

[Picha katika ukurasa wa 17]

Bougainville alikaribishwa kwa ukarimu na watu wa Tahiti wenye urafiki

[Hisani]

By permission of the National Library of Australia NK 5066

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mashahidi wa Yehova hufurahia kuwaeleza watu kuhusu Paradiso itakayokuja

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 17]

Photo courtesy of Tahiti Tourisme

[Picha katika ukurasa wa 19]

Page 18: Canoeists, waterfall, and background: Photos courtesy of Tahiti Tourisme