Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuacha Udhalimu

Kuacha Udhalimu

Kuacha Udhalimu

‘Mdhalimu anaweza kubadili tabia yake.’—Dakt. C. Sally Murphy.

MDHALIMU na yule anayedhulumiwa wanahitaji msaada. Mdhalimu anahitaji kujifunza jinsi ya kushirikiana na wengine bila kuwadhulumu. Na yule anayedhulumiwa anahitaji kujua jinsi ya kukabiliana na tatizo hilo.

Mara nyingi, mdhalimu hajui jinsi ya kushirikiana na wengine wala haelewi jinsi wale ambao anawadhulumu wanavyohisi. Anahitaji kuongozwa na kufundishwa jinsi ya kueleza maoni yake vizuri. Kitabu Take Action Against Bullying kinasema hivi: “Wadhalimu wasipobadili tabia yao, wao huendelea daima kuwadhulumu wengine. Wao huwadhulumu wenzi wao, watoto wao, na hata labda wafanyakazi walio chini yao kazini.”

Msaada wa Kuacha Kuwadhulumu Wengine

Kuwazoeza watoto kuwa na huruma toka utotoni kwaweza kuwasaidia wasiwe wadhalimu. Walimu katika nchi fulani wameanza kuwafundisha watoto kuelewa hisia za wengine. Wao huwafundisha hata watoto walio na umri wa miaka mitano kuelewa hisia za wengine na kuwatendea watu kwa fadhili. Ijapokuwa hakuna habari nyingi kuhusu faida za kudumu za elimu hiyo, matokeo yaliyopatikana kufikia sasa yanaonyesha kwamba wale ambao wamefundishwa kuwahurumia wengine si wajeuri kama wale ambao hawajafundishwa.

Wewe mzazi unapaswa pia kuwafundisha watoto wako jinsi ya kuwahurumia wengine badala ya kutarajia tu wafundishwe jambo hilo shuleni. Ikiwa hutaki mtoto wako awe mdhalimu, unapaswa kumfundisha kwa maneno na kwa matendo jinsi ya kuwatendea wengine kwa heshima na adhama. Ni nini kinachoweza kukusaidia? Huenda tayari una kitu bora kinachoweza kukusaidia kufundisha lakini kinachopuuzwa sana, yaani, Neno la Mungu, Biblia. Kinaweza kukusaidiaje?

Kwa mfano, kinaeleza waziwazi maoni ya Mungu kuhusu dhuluma. Anaichukia kabisa! Biblia inasema hivi kumhusu Mungu: “Nafsi yake humchukia . . . mwenye kupenda udhalimu.” (Zaburi 11:5) Isitoshe, Mungu anajua mambo yanayoendelea. Biblia inaeleza jinsi alivyohuzunika wakati Waisraeli walipoteseka “kwa sababu ya watu wale waliowaonea na kuwasumbua.” (Waamuzi 2:18) Katika pindi nyingi, Mungu aliwaadhibu wale waliotumia nguvu zao kuwadhulumu wanyonge na wasioweza kujitetea.—Kutoka 22:22-24.

Biblia pia ina ushauri unaojulikana sana kuhusu kuelewa hisia za wengine. Yesu alisema hivi: “Mambo yote mtakayo watu wawafanyie nyinyi, lazima mwafanyie wao pia hivyohivyo.” (Mathayo 7:12) Si rahisi kuwafundisha watoto kuipenda na kuitumia hiyo Kanuni Bora maishani mwao. Ni lazima uwawekee mfano bora, ukazie jambo hilo mara nyingi, na ujitahidi sana, hasa kwa sababu watoto wachanga hujipenda. Lakini jitihada hizo zote zina faida kubwa. Watoto wako wakijifunza kuwa wenye fadhili na kuelewa hisia za wengine, wataepuka kabisa kuwadhulumu wengine.

Msaada kwa Wanaodhulumiwa

Watu wanaodhulumiwa, hasa vijana, wanakabili ugumu fulani, yaani, kutulia na kutenda kwa busara wanaposhambuliwa. Mtu anapokudhulumu, huenda anataka uumie kihisia. Anataka ukasirike sana au uogope. Ukipandwa na hasira au ukilia na kuonyesha kwamba umeumia au unaogopa, basi mdhalimu amefaulu. Kwa hiyo, huenda akajaribu kukuumiza tena na tena.

Unaweza kufanya nini? Zingatia madokezo yafuatayo. Yameandikwa hasa kwa ajili ya vijana, lakini kanuni zilizomo zinahusu pia watu wazima wanaodhulumiwa.

Tulia. Usipandwe na hasira. Biblia inatoa shauri hili la hekima: “Ukomeshe hasira, uache ghadhabu.” (Zaburi 37:8) Ukipanda mori, unamfanya mdhalimu akudhibiti, na huenda ukafanya mambo ambayo utayajutia baadaye.—Mithali 25:28.

Jitahidi kuepuka kufikiria kulipiza kisasi. Mara nyingi mtu anayelipiza kisasi ndiye anayeumia zaidi. Kulipiza kisasi hakuridhishi hata kidogo. Msichana mmoja ambaye alipigwa na vijana watano alipokuwa mwenye umri wa miaka 16, anasema hivi: “Niliazimia kulipiza kisasi. Kwa hiyo, niliwaomba marafiki zangu wanisaidie kuwashambulia vijana wawili kati ya wale walionipiga.” Matokeo yakawa nini? Anasema hivi: “Nilihisi vibaya sana.” Baada ya hapo tabia yake ikaharibika hata zaidi. Kumbuka maneno haya yenye hekima ya Biblia: “Msirudishe ovu kwa ovu kwa yeyote.”—Waroma 12:17.

Ukiona kwamba mambo yanachacha, ondoka haraka. Biblia inasema hivi: “Acheni ugomvi kabla haujafurika.” (Mithali 17:14) Yaani, jaribu kuwaepuka wadhalimu. Mithali 22:3 inasema hivi: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.”

Udhalimu ukiendelea, huenda ikakubidi useme waziwazi. Chagua wakati ambapo umetulia, umtazame mdhalimu ana kwa ana, na uzungumze kwa sauti thabiti bila wasiwasi. Mweleze kwamba hupendi yale anayofanya, kwamba hayafurahishi na yanaumiza. Usimtusi wala kumtisha.—Mithali 15:1.

Zungumza na mtu mzima anayetegemeka na anayejali kuhusu jinsi unavyodhulumiwa. Mweleze tatizo lako waziwazi, na umwombe msaada wa kukabiliana nalo. Pia, unaposali mwambie Mungu jambo hilo kwani yeye ndiye chanzo bora zaidi cha msaada na faraja.—1 Wathesalonike 5:17.

Kumbuka kwamba una thamani. Mdhalimu anaweza kukufanya uhisi kwamba wewe ni bure, kwamba unastahili kudhulumiwa. Lakini yeye hastahili kuamua lolote kukuhusu. Mungu ndiye hakimu, naye huona sifa nzuri za kila mmoja wetu. Mdhalimu ndiye anayejivunjia heshima kwa kuwadhulumu wengine.

Enyi Wazazi, Walindeni Watoto Wenu

Wazazi pia wanaweza kuanza mapema kuwafundisha watoto wao kutenda kwa busara wanapokabiliana na wadhalimu. Kwa mfano, wanaweza kucheza michezo ya kuigiza pamoja nao ili kuwafundisha jinsi wanavyoweza kuonyesha kwamba wanajiamini.

Hata kusimama wima kwaweza kuonyesha kwamba unajiamini na kuwafanya wadhalimu waogope kukudhulumu. Pia ni muhimu kumtazama mdhalimu uso kwa uso, kutuliza mikono, na kuzungumza kwa sauti imara. Wazazi wanatiwa moyo wamfundishe mtoto kuwaondokea na kuwaepuka wadhalimu, na kuomba msaada wa mtu mzima anayeaminika, kama vile mwalimu.

Kuielimisha familia ndiyo hatua ya kwanza ya kukomesha dhuluma. Wazazi wanaotumia wakati pamoja na watoto wao na kusikiliza matatizo yao kwa subira na huruma, huwafanya wahisi wanathaminiwa, wanaungwa mkono, na kwamba wanapendwa. Wataalamu wengi wanaotoa mashauri kuhusu kulea watoto na kushughulika na matatizo ya vijana huwatia moyo wazazi kuwasaidia watoto wao kuwa na maoni mazuri kujihusu. Wakiwa na maoni hayo mazuri, uwezekano wa kushambuliwa utapungua.

Lakini kuzungumza hakutoshi. Kila mtu katika familia anahitaji kujifunza kuwatendea wengine kwa heshima na kwa adhama na kuelewa hisia za wengine. Kwa hiyo, usikubali dhuluma yoyote katika familia yako. Fanya nyumba yako iwe mahali salama, mahali penye heshima na upendo.

Mwisho wa Dhuluma

“Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.” (Mhubiri 8:9, chapa ya 1989) Hivyo ndivyo Biblia inavyoeleza kwa ufupi historia ya wanadamu. Naam, wanadamu wamedhulumiwa kwa maelfu ya miaka. Mwandikaji mmoja wa Biblia alisema: “Nikarudi na kuona madhalimu yote yanayotendeka chini ya jua; na tazama, machozi yao waliodhulumiwa, ambao walikuwa hawana mfariji; na upande wa wale waliowadhulumu kulikuwa na uwezo, walakini wale walikuwa hawana mfariji.”—Mhubiri 4:1.

Hata hivyo, hapana shaka kwamba Mungu anaona dhuluma yote inayotukia ulimwenguni, na anawahurumia wale wanaodhulumiwa. Lakini je, ataleta suluhisho? Bila shaka! Ona ahadi yake kwenye Mika 4:4: “Wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu; kwa kuwa kinywa cha BWANA wa majeshi kimesema hivi.”

Hebu wazia jinsi ulimwengu utakavyokuwa ahadi hiyo itakapotimia. Hakuna mtu atakayewatia wengine hofu—la, hakutakuwa na wadhalimu! Je, unavutiwa na wazo hilo? Lakini zaidi ya kutoa ahadi hiyo, Mungu amefanya mengi zaidi. Sasa hivi kuna programu ya kuwafundisha watu Biblia ambayo inaendelea ulimwenguni pote, nayo ina matokeo mazuri sana. Wale wanaofaidika kutokana nayo wanafundishwa kubadili sifa zao mbaya za jeuri, kudumisha amani kati yao, na kuwatendea wengine kwa heshima na kwa adhama. (Waefeso 4:22-24) Hivi punde, matokeo ya mafundisho hayo bora yataonekana duniani pote, na dhuluma haitakuwapo tena. Ahadi za Mungu zilizomo katika Biblia zitatimia. Kila mtu atakayekuwapo wakati huo atafurahia kuishi katika ulimwengu usio na wadhalimu!

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kumwondokea mdhalimu si jambo la kuaibikia

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kukiwa na hali nzuri katika familia, watoto hufundishwa kukabiliana na aina zote za dhuluma

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wafundishe watoto wako kusema waziwazi na kwa uthabiti, lakini kwa busara