Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nawezaje Kuacha Kutarajia Ukamilifu?

Nawezaje Kuacha Kutarajia Ukamilifu?

Vijana Huuliza . . .

Nawezaje Kuacha Kutarajia Ukamilifu?

“Mimi hutarajia kila kitu kiwe kikamilifu maishani mwangu.”—Carly.

VIJANA wengi wanafikiri kimakosa kwamba kila kitu wanachofanya lazima kiwe kikamilifu.

Kitabu Perfectionism—What’s Bad About Being Too Good? kinasema hivi: “Kuna tofauti kubwa kati ya kutamani kufanikiwa na kujaribu juu chini kufikia kiwango kisichowezekana. Watu wanaotaka kufanikiwa wanaweza kuwa na utaratibu wa hali ya juu na matumaini makubwa, lakini wao pia hukubali makosa yao na kutafuta njia mwafaka za kushughulika nayo. . . . Kwa upande mwingine, wale wanaotarajia ukamilifu daima huishi na wasiwasi kwamba watakosea. Wao hujiwekea miradi ya juu sana.”

Je, wewe una matarajio kama hayo? Ukijiwekea miradi ya juu sana, huenda ukashindwa kutenda jambo lolote. Hata unaweza kuepuka kufanya jambo lolote jipya. Au unaweza kuahirisha kufanya mambo muhimu kwa sababu unaona hutafanikiwa. Huenda hata ukavunja uhusiano na watu wanaoshindwa kufikia viwango ambavyo umeweka na kujikuta bila marafiki.

Iwapo una mwelekeo kama huo, fikiria maneno haya ya Biblia kwenye Mhubiri 7:16: “Usiwe na haki kupita kiasi; wala usijiongezee hekima mno; kwani kujiangamiza mwenyewe?” Ndiyo, mtu anayetarajia mengi kupita kiasi anaweza “kujiangamiza”! Ama kweli, tabia ya kutarajia mengi kupita kiasi huchangia maradhi hatari kama vile ugonjwa wa kujinyima chakula na ule wa kula na kujitapisha. *

Huenda ukauliza, ‘Nawezaje kuacha kutarajia ukamilifu?’ Kwa kweli huenda isiwe rahisi kwako kubadili mtazamo huo. Lakini inawezekana kwa msaada wa Mungu. Basi ebu tuone maoni ya Mungu ni nini kuhusu kutarajia ukamilifu.

Je, Ukamilifu Unawezekana?

Kwanza, je, inawezekana mtu awe mkamilifu kabisa? La, kwani Biblia inasema hivi: “Hakuna mtu mwadilifu, hakuna hata mmoja . . . Watu wote wamekengeuka, wote pamoja wamekuwa wasiofaa kitu.” (Waroma 3:10-12) Hayo ni maneno yenye kuvuta fikra zetu sana. Yanaonyesha kwamba mtu anayejaribu kuwa mkamilifu kabisa hatafanikiwa.

Mfikirie mtume Paulo, ambaye bila shaka, alikuwa mtu mwenye imani nyingi. Hata hivyo, Paulo hangeweza kumtumikia Mungu bila kukosea. Alikiri hivi: “Nitakapo kulifanya lililo sawa, lililo baya lipo pamoja nami. Kwa kweli napendezwa na sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani, lakini mimi naona katika viungo vyangu sheria nyingine ikifanya vita dhidi ya sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu.” (Waroma 7:21-23) Paulo alikuwa Mkristo mwaminifu kwa msaada wa Mungu tu.

Inapendeza kama nini kwamba Mungu hatulazimishi wala kutarajia tuwe wakamilifu. “Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zaburi 103:14) Ni katika ulimwengu mpya wa Mungu tu ndipo wanadamu watakapofikia ukamilifu.

Fikiria Upya Matarajio Yako

Kwa hiyo, si jambo la akili kufikiri kwamba unaweza kuwa mkamilifu kabisa. Hata unapaswa kutazamia kufanya makosa mara kwa mara. (Waroma 3:23) Wakati mwingine hata hatutambui kuwa tumekosea! Zaburi 19:12 inauliza hivi: “Ni nani awezaye kuyatambua makosa yake?” Mvulana anayeitwa Matthew alisema: “Wewe si mkamilifu—hakuna mtu duniani ambaye amekamilika. Ukitarajia ukamilifu, hutapata furaha. . . . Ni jambo lisilowezekana.”

Ukizingatia hilo, mbona usijaribu kufikiria upya baadhi ya matarajio yako? Kwa mfano, je, unajichosha kwa kujaribu kuwa bingwa katika jambo fulani? Biblia inasema kwamba kujichosha hivyo ni “ubatili na kujilisha upepo.” (Mhubiri 4:4) Ukweli ni kwamba ni wachache ambao hufanikiwa kuwa wa kwanza. Baada ya muda fulani, hata wale wanaofaulu kuwa wa kwanza hushindwa na wengine walio bora.

Mtume Paulo alishauri hivi: “Naambia kila mtu huko miongoni mwenu kati yenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri; bali afikiri ili awe na akili timamu.” (Waroma 12:3) Fikiri kwa utimamu. Fikiria upya matarajio yako na uyabadili kupatana na uwezo na udhaifu wako. Jaribu kufanikiwa katika kazi yako, lakini usitarajie ukamilifu. Jiwekee miradi hususa unayoweza kutimiza.

Kwa mfano, Paulo alimhimiza Timotheo awe ‘mtenda-kazi asiye na lolote la kuaibikia, akilitumia sawasawa neno la ile kweli.’ (2 Timotheo 2:15) Naam, Paulo alizungumzia kufanikiwa si ukamilifu. Vivyo hivyo, jiwekee miradi unayoweza kufikia. Na ikiwa hujui ile “unayoweza kufikia,” zungumzia jambo hilo na wazazi wako au mtu mwingine mkomavu ambaye unamtumaini.

Wengine husema tujaribu kufanya mambo fulani ambayo hatujazoea, kama vile kucheza mchezo mpya au kutumia ala fulani ya muziki. Kwa kweli utakosea mara nyingi unapojifunza jambo jipya. Hilo ni jambo la kawaida. Huenda likakusaidia kutambua kwamba sisi hujifunza kupitia makosa.

Haidhuru jambo unalotaka kutimiza, iwe ni kuandika insha shuleni au kujifunza kucheza muziki mpya kwenye piano, zingatia shauri hili la mtume Paulo: ‘Usicheze-cheze katika shughuli yako.’ (Waroma 12:11) Naam, usiahirishe mambo kwa kuwa unaona utakosea.

Msichana mmoja alizoea kuahirisha kufanya kazi ya shule akitoa udhuru kwamba alikuwa “akijipanga.” Ingawa ni vizuri kujipanga, uwe mwangalifu usitumie jambo hilo kuwa udhuru wa kuahirisha mambo. Msichana huyo alikuja kutambua kwamba “ikiwa itakubidi kuchagua kati ya kumkabidhi mwalimu kazi ya shule isiyokuridhisha au kukosa kuipeleka, ni vyema uchague kumkabidhi.”

Ondoa Mawazo Yanayodhuru!

Huenda isiwe rahisi kuacha kutarajia ukamilifu katika mambo unayofanya. Huenda bado ukawa na mawazo yasiyofaa na kuendelea kujichambua. Unaweza kufanya nini? Ukweli ni kwamba mawazo hayo yanaweza kukudhuru. Kwa hiyo, epuka kujifikiria vibaya. Hata unaweza kujicheka unapokosea kwani kuna “wakati wa kucheka.” (Mhubiri 3:4) Pia, kumbuka kwamba Yehova hapendi usemi wenye kuudhi, hata kama mtu anajielekezea usemi huo.—Waefeso 4:31.

Badala ya kujiona kuwa hufai, tumia maneno ya Mithali 11:17: “Mwenye rehema huitendea mema nafsi yake; aliye mkali hujisumbua mwili wake.” Hivyo jiulize, Je, kujiwekea miradi ya juu sana kumenisaidia kupata marafiki? Huenda ukajibu la. Labda hata umevunja urafiki na watu fulani kwa sababu wao si wakamilifu. Basi unaweza kufanya nini?

Tumia shauri hili la Biblia: “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine.” (Wakolosai 3:13) Naam, ukiacha kutarajia mengi kupita kiasi kutoka kwa wengine, itakuwa rahisi kwako kuwa na marafiki.

Huenda ukajiuliza hivi: ‘Kwa nini watu waniepuke kwa sababu ninatarajia ukamilifu?’ Fikiria jinsi kutarajia ukamilifu kunavyoweza kuwaathiri wengine. Kitabu When Perfect Isn’t Good Enough kinasema hivi: “Kulalamika sana kwa sababu hukupata alama ya A katika mtihani ni jambo lenye kuumiza wengine ambao walijikakamua kupata alama ya B au C.” Kwa hiyo jitahidi kuondoa mawazo yasiyofaa na usijifikirie kupita kiasi. Watu watafurahia zaidi kushirikiana nawe.

Msichana anayeitwa Carly anasema hivi: “Mimi hujaribu juu chini kuacha kutarajia ukamilifu.” Unawezaje kufanya hivyo pia? Fikiria jinsi Mungu anavyoona mambo. Iwapo bado una tatizo la kutarajia ukamilifu, zungumza jambo hilo pamoja na wazazi wako au na Wakristo wakomavu kutanikoni. Sali kwa Mungu ukimwomba msaada wa kubadili maoni yako. Sala inaweza kukusaidia sana kushinda tatizo la kutarajia ukamilifu.—Zaburi 55:22; Wafilipi 4:6, 7.

Sikuzote kumbuka kwamba Yehova hatarajii ukamilifu kutoka kwetu; yeye hutaka tu tuwe waaminifu kwake. (1 Wakorintho 4:2) Iwapo unajitahidi kuwa mwaminifu, utakuwa na furaha kwelikweli, ijapokuwa wewe si mkamilifu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona makala “Kwa Nini Nataka Kila Kitu Ninachofanya Kiwe Kikamilifu?” katika toleo la Amkeni! la Julai 22, 2003.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kuogopa kushindwa kunaweza kukuzuia usitende lolote

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kujifunza mambo mapya kunaweza kukusaidia ukabiliane na makosa yako