Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Baada ya Milipuko

Baada ya Milipuko

Baada ya Milipuko

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI EKUADO

NOVEMBA 20, 2002, ilikuwa siku yenye kupendeza katika jiji la Riobamba nchini Ekuado. Anga lilikuwa jangavu, na mawingu meupe yalitanda juu. Milima ya volkeno yenye vilele vya theluji ilivutia wee! Wakazi 124,000 wanaoishi kwenye eneo lenye kimo cha meta 2,700 katika Milima ya Andes, waliendelea na shughuli zao za kawaida bila kujua kwamba hali hiyo tulivu ingevurugwa kabisa. Kwa ghafula, kukatokea mlipuko mkubwa alasiri! Madirisha na sakafu zilianza kutetemeka. Wingu kubwa jeusi lilisambaa haraka.

Baada ya dakika kumi, mlipuko mwingine ukatokea na kusababisha tetemeko lenye nguvu lililopasua madirisha na kung’oa milango. Kisha kukatokea wingu la moto na moshi ambalo lilikuwa kubwa kuliko lile la kwanza. Halafu milipuko na mioto mingine ilifuata.

José na mkewe Ana, ambao ni Mashahidi wa Yehova walio na umri wa miaka 60 na kitu, walikuwa wakiishi meta 400 kutoka eneo la mlipuko. Walivurumishwa sakafuni na mlipuko huo. Ana alikuwa amesimama karibu na mlango wa mbele wakati ulipong’olewa na kurushwa ukutani. Wenzi hao walioshtuka walipokuwa wakikimbilia nyuma ya nyumba, dari lilianza kuwaangukia. Walifaulu kufika kwenye ua mdogo wa nyuma, ambako walikumbatiana na kuanza kusali. Dakika 15 baadaye, mwana wao aliwasili kwa gari na kuwachukua.

Hata hivyo, wengine hawakuponyoka. Kulitokea hali ya wasiwasi baada ya milipuko hiyo. Halaiki ya watu ilikimbia kwa miguu na wengine walipaaza kilio na kupiga kelele, huku wengine wakiteleza na kuangukia vioo vilivyotapakaa kwenye vijia. Magari, mabasi, na malori yaliendeshwa kasi kutoka jijini, huku madereva wengine wakipitia upande usiofaa wa barabara zinazoelekea upande mmoja! Wengi waliokimbia kutoka shuleni au kazini hawakujua hali ya familia zao kwa karibu saa 24.

Ni nini kilichosababisha hali hiyo ya taharuki? Moto uliotokea katika bohari ya silaha ya ardhini kwenye kambi ya kijeshi ulilipua gruneti, vifaru, na makombora. Milipuko ilipokuwa ikiendelea, magari ya polisi yalitangaza kwa vipaza-sauti kwamba watu wote walipaswa kuondoka jijini na kwenda umbali wa angalau kilometa 15.

Punde si punde, jiji la Riobamba halikuwa na watu. Maelfu ya wakazi walijaa na kukusanyika kwenye barabara kuu nje ya jiji usiku huku kukiwa na baridi—na wengi wao hawakuwa na makoti. Baada ya saa kadhaa, milipuko hiyo ilianza kupungua. Baridi kali sana iliwafanya wakazi hao waanze kurudi jijini pole kwa pole kwa uangalifu. Kulipokucha, wengi waligundua kwamba madirisha, milango, paa, madari, na kuta za nyumba zao zilikuwa zimeharibiwa vibaya. Familia moja ilipata vioo vyenye makali ndani ya godoro. Wengine walipata vipande vya chuma ndani na nje ya nyumba zao.

Taarifa za awali zilionyesha kwamba angalau watu 7 walikufa, 538 walijeruhiwa, na nyumba 18,000 ziliharibiwa. Kati ya Mashahidi wa Yehova 950 wanaoishi katika eneo hilo, hakuna yeyote aliyekufa ingawa wawili walijeruhiwa sana.

Msaada kwa Walioathiriwa

Asubuhi iliyofuata siku ya mlipuko, wazee wa makutaniko ya Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo walianza kuwatembelea ndugu zao Wakristo ili kuwajulia hali. Siku hiyohiyo, mwangalizi asafiriye wa Mashahidi wa Yehova alikutana na wazee wa makutaniko 13 ya karibu ili wachanganue hasara na hali ya waliojeruhiwa. Aliwatia moyo wazee washughulikie mahitaji ya kihisia na ya kiroho ya walioathiriwa. Ilikuwa muhimu sana wahudhurie mikutano ya Kikristo ingawa walikabili hali ngumu! (Waebrania 10:24, 25) Hivyo jioni iliyofuata, makutaniko yalifanya mikutano kama kawaida.

Siku ya Alhamisi na Ijumaa, ripoti kamili kuhusu nyumba za Mashahidi zilizoharibiwa ilitumwa kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Guayaquil. Ilionyesha kwamba mamia ya madirisha yaliyovunjwa yalihitaji kurekebishwa haraka ili kuwakinga wakazi kutokana na baridi. Baada ya saa kadhaa, ofisi ya tawi ilikuwa imenunua karatasi nyingi za plastiki, tepe za kuunganisha, na misumari inayopenya saruji, ili kufanya marekebisho ya muda.

Lori lenye vifaa lililotoka kwenye ofisi ya tawi liliwasili Jumamosi saa tatu asubuhi. Vikundi vya Mashahidi wanaume kwa wanawake tayari vilikuwa vimeanza kuwasaidia Mashahidi wenzao kuondoa vioo vilivyovunjika nyumbani mwao ili kazi ya kurekebisha ianze. Jumba la Ufalme lililo karibu lilitumiwa kama kituo cha kutoa msaada. Alama ziliwekwa sakafuni ili plastiki zipimwe haraka. Vipimo vilivyotayarishwa na wafanyakazi wa kujitolea vilitumiwa kukata plastiki kabla hazijapelekwa kwa wafanyakazi.

José, aliyetajwa mwanzoni, anaeleza hivi: “Tulipowasili nyumbani alasiri iliyofuata mlipuko, tuliwakuta akina ndugu wakiondoa vifusi. Siku ya Jumamosi, jirani yangu alikuja na kusifu kazi nzuri ya kuweka plastiki iliyofanywa nyumbani mwangu, kisha akaniuliza, ‘Kazi yote hii ilikugharimu pesa ngapi?’” Alishangaa sana nilipomwambia kwamba haikugharimu chochote!

Kufikia Jumamosi jioni, wafanyakazi wa kujitolea wapatao 200 kutoka makutaniko ya karibu walikuwa wameziba madirisha ya nyumba 91 za Mashahidi. Watu wengi wasio Mashahidi pia walisaidiwa. Gazeti moja lilionyesha picha ya nyumba iliyorekebishwa na Mashahidi na likataja kwamba kati ya watu wanane walioishi humo, ni mmoja tu aliyekuwa Shahidi wa Yehova.

Msaada wa Kihisia Watolewa

Bila shaka milipuko hiyo ilifadhaisha sana kihisia. Ili kuwafariji Mashahidi wa eneo hilo, mkutano wa pekee ulifanywa Jumatatu, Novemba 25, saa 11 jioni. Wawakilishi wa ofisi ya tawi walitumwa kuongoza mkutano huo. Mkutano huo haungefanywa usiku kwa sababu hakukuwa na umeme. Ilitarajiwa kwamba watu 600 hivi wangehudhuria kwa sababu ya saa za mkutano huo. Hata hivyo, watu 1,421, kutia ndani majirani ambao si Mashahidi walifurika kwenye Jumba la Kusanyiko la Riobamba! Andiko moja lililokaziwa katika programu hiyo lilikuwa Zaburi 4:8: “Katika amani nitajilaza na kupata usingizi mara, maana Wewe, BWANA, peke yako, ndiwe unijaliaye kukaa salama.” Watu wote waliohudhuria walithamini sana programu hiyo ya kiroho yenye kufariji.

Mwishoni mwa programu, wazazi walipewa mamia ya makala za Amkeni! zenye kichwa “Misiba ya Asili—Kumsaidia Mtoto Wako Kukabili Hali.” (Juni 22, 1996) Fungu moja la makala hiyo linasema hivi:

“Shirika la Serikali la Kushughulikia Hali ya Dharura la Marekani (FEMA) lasema kwamba mara tu baada ya msiba, kwa kawaida watoto huhofu kwamba (1) wataachwa peke yao, (2) watatenganishwa na familia, (3) jambo hilo litatukia tena, na (4) mtu fulani atajeruhiwa au kuuawa.” Kwa kutegemea makala hiyo, wazazi walihimizwa hivi:

1. Wajaribu kuleta familia yote pamoja.

2. Waeleze kuhusu hali hiyo kwa utulivu.

3. Wawatie moyo watoto waeleze hisia zao.

4. Wawahusishe watoto katika kazi ya kurekebisha.

Baadaye, majirani na wanafunzi wa Biblia walipewa nakala za ziada za makala hiyo ya Amkeni!

Majuma matatu baada ya mlipuko, vifaa vilinunuliwa kwa ajili ya kufanya marekebisho ya kudumu, kutia ndani kuweka madirisha mapya, madari, na paa. Baada ya majuma mengine matatu, kazi hiyo ilikuwa imemalizika na Majumba mawili ya Ufalme yalikuwa yamerekebishwa pia. Wengi walishukuru sana kwa sababu ya msaada huo wa upendo.

Misiba mbalimbali hutukia mara nyingi katika ‘siku hizi za mwisho.’ (2 Timotheo 3:1-5) Hata hivyo, msaada ambao Mashahidi wa Yehova huwapa wenzao na majirani wao huonyesha nguvu za Ukristo wa kweli. Kwa kufaa, José alisema hivi: “Tengenezo la Yehova halikawii kutusaidia tunapohitaji msaada.”

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mashahidi wapatao 200 walijitolea kufanya kazi ya kurekebisha. Vioo vipya vilipimwa, kukatwa na kuwekwa. Paa mpya ziliwekwa