Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Hutubariki kwa Kutupa Utajiri?

Je, Mungu Hutubariki kwa Kutupa Utajiri?

Maoni ya Biblia

Je, Mungu Hutubariki kwa Kutupa Utajiri?

“Baraka ya BWANA hutajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo.”—MITHALI 10:22.

JE, ANDIKO la Biblia ambalo limenukuliwa hapo juu lamaanisha kwamba Mungu huwabariki watu wake kwa kuwapa utajiri wa kimwili? Baadhi ya watu huamini hivyo. Hebu fikiria jinsi mhubiri mmoja wa Australia wa Pentekoste aliye pia mwandishi alivyodai: “Katika kitabu changu nitakueleza kwa nini unahitaji pesa nyingi zaidi na pili, jinsi unavyoweza kupata pesa nyingi zaidi . . . Ikiwa unaweza kubadili fikira zako na kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu pesa, naamini kwamba Mungu atakubariki na kukufanikisha nawe hutakuwa na tatizo la pesa tena kamwe.”

Hata hivyo, dai kama hilo, huonyesha kwamba wale walio maskini hawana kibali cha Mungu. Je, kwa kweli ufanisi wa kimwili huonyesha kwamba mtu amebarikiwa na Mungu?

Wabarikiwa kwa Kusudi Fulani

Biblia hutaja watumishi waaminifu wa Mungu waliobarikiwa kwa utajiri. Kwa mfano, Yakobo aliondoka nyumbani akiwa na fimbo yake tu lakini akarudi miaka 20 baadaye akiwa na kondoo, ng’ombe, na punda wa kutosha kambi mbili. Kulingana na Biblia, ufanisi wa Yakobo ulikuwa zawadi kutoka kwa Mungu. (Mwanzo 32:10) Mfano mwingine: Ayubu alipoteza mali yake yote, lakini baadaye Yehova alimbariki kwa “kondoo kumi na nne elfu, na ngamia elfu sita, na jozi za ng’ombe elfu, na punda wake elfu.” (Ayubu 42:12) Yehova alimpa Mfalme Sulemani utajiri mwingi sana hivi kwamba sifa zake zajulikana hata leo.—1 Wafalme 3:13.

Kwa upande mwingine, Biblia ina masimulizi mengi ya waabudu waaminifu na watiifu wa Mungu waliokuwa maskini. Kwa kweli, Mungu hakuwa akiwaadhibu watu fulani kwa umaskini huku akiwabariki wengine kwa ufanisi. Basi, kwa nini Mungu aliwapa watu fulani utajiri?

Jibu ni tofauti katika kila kisa. Utajiri wa Yakobo uliweka msingi wa taifa, akitayarisha kuja kwa Uzao ulioahidiwa. (Mwanzo 22:17, 18) Ufanisi wa Ayubu uliondoa shaka yoyote kuhusu yule aliyekuwa amemletea Ayubu msiba, na hivyo jina la Yehova likatakaswa. (Yakobo 5:11) Naye Sulemani alitumia utajiri wake aliopewa na Mungu kujenga hekalu lenye fahari. (1 Wafalme 7:47-51) Yehova alimtumia Sulemani pia kuandika kuhusu faida kidogo ya utajiri kutokana na yale aliyojionea maishani.—Mhubiri 2:3-11; 5:10; 7:12.

Jinsi Mungu Anavyotubariki

Yesu aliwafundisha wafuasi wake wawe na maoni yanayofaa kuhusu pesa alipowaambia ‘wakome kuhangaika’ kuhusu mali. Aliwaambia kwamba hata Sulemani katika utukufu wake wote hakuvaa vizuri kama mojawapo ya mayungiyungi ya kondeni. Hata hivyo, Yesu alisema: “Ikiwa Mungu huvisha hivyo mimea ya shambani, . . . je, si afadhali zaidi sana yeye atawavisha nyinyi, nyinyi wenye imani kidogo?” Yesu aliwahakikishia Wakristo kwamba ikiwa wafuasi wake wangetafuta kwanza Ufalme na uadilifu wa Mungu, basi wangeongezewa chakula, mavazi, na makao. (Mathayo 6:25, 28-33) Ahadi hiyo hutimizwaje?

Shauri la Biblia linapofuatwa, huleta baraka za kiroho. (Mithali 10:22) Hata hivyo, huleta mafanikio mengine. Kwa mfano, Neno la Mungu huwaagiza Wakristo hivi: “Mwibaji na asiibe tena, bali acheni afanye kazi ya bidii.” (Waefeso 4:28) Pia husema kwamba “Atendaye mambo kwa mkono mlegevu huwa maskini; bali mkono wake aliye na bidii hutajirisha.” (Mithali 10:4) Mara nyingi waajiri hupenda Wakristo wanyofu, wenye bidii wanaofuata shauri hilo. Hilo laweza kuwa baraka.

Pia, Biblia huwafundisha Wakristo waepuke kuwa na pupa kwa kucheza kamari, zoea chafu la kuvuta sigara, na zoea lenye kudhuru la kulewa. (1 Wakorintho 6:9, 10; 2 Wakorintho 7:1; Waefeso 5:5) Wanaofuata shauri hili hupunguza gharama zao na afya zao huwa bora zaidi.

Kitu Chenye Thamani Kuliko Fedha au Dhahabu

Hata hivyo, ufanisi wa kimwili peke yake hauonyeshi kwamba mtu ana kibali na baraka za Mungu. Kwa mfano, Yesu alifunua hali mbaya ya kiroho ya baadhi ya Wakristo katika Laodikia alipowaambia: “Wasema: ‘Mimi ni tajiri na nimejipatia utajiri na sihitaji kitu chochote hata kidogo,’ lakini hujui wewe ni mwenye taabu na wa kusikitikiwa na maskini na kipofu na uchi.” (Ufunuo 3:17) Kinyume na hilo, Yesu aliwaambia hivi Wakristo wa Smirna waliokuwa maskini kimwili lakini matajiri kiroho: “Najua dhiki na umaskini wako—lakini wewe ni tajiri.” (Ufunuo 2:9) Yaelekea Wakristo hao walipata hasara ya kifedha waliponyanyaswa kwa sababu ya uaminifu wao, lakini walikuwa na utajiri wenye thamani kuliko fedha au dhahabu.—Mithali 22:1; Waebrania 10:34.

Yehova Mungu huwabariki wale wanaojitahidi kufanya mapenzi yake. (Zaburi 1:2, 3) Yeye huwapa nguvu na uwezo wa kukabiliana na majaribu, kuruzuku familia zao, na kuutafuta kwanza Ufalme wake. (Zaburi 37:25; Mathayo 6:31-33; Wafilipi 4:12, 13) Basi, badala ya kuona vitu vya kimwili kuwa baraka ya pekee kutoka kwa Mungu, Wakristo wa kweli hujitahidi kuwa “matajiri katika kazi zilizo bora.” Kwa kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Muumba, Wakristo ‘wanajiwekea wenyewe kuwa hazina salama msingi bora kwa ajili ya wakati ujao.’—1 Timotheo 6:17-19; Marko 12:42-44.