Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maoni Yanayofaa Kuhusu Mitindo

Maoni Yanayofaa Kuhusu Mitindo

Maoni Yanayofaa Kuhusu Mitindo

BIBLIA husema kwamba Mungu “amefanya kila kitu kiwe chenye kupendeza kwa wakati wake.” (Mhubiri 3:11, NW) Sisi huona vitu vyenye kupendeza kila mahali ulimwenguni. Pia twawaona watu wenye kupendeza.

Lengo la mbuni wa mitindo ni kuboresha sura yetu kupitia mavazi tunayovaa. Lakini kama ilivyoonyeshwa katika makala iliyotangulia, mitindo imebadili maoni ya watu kuhusu urembo. Profesa wa saikolojia Ruth Striegel-Moore asema hivi: “Kwa kuwa tumezoea sana kuona wanawake wembamba kupita kiasi, tumeanza kufikiri kwamba huo ndio urembo.”

Ni wazi kwamba, si jambo la hekima kukubali maoni yaliyo ulimwenguni sasa kuhusu urembo yatuathiri. Katika kitabu chake Always in Style, Doris Pooser aeleza kwamba “mwanamke wa leo hana haja ya kuubadili au kuuficha mwili wake wakati wowote ‘dhana’ mpya zinapotokea.” Kwa kweli, kwa nini turuhusu vyombo vya habari vitufinyange? “Ingekuwa afadhali kama nini kukubali jinsi tulivyo, badala ya kujaribu sana kubadili sura yetu,” asema Pooser.

Urembo Usioharibika

Kujiamini na kuridhika maishani hakutegemei kuwa na sura nzuri tu. “Furaha ya kweli hutoka moyoni,” aandika Judy Sargent, aliyekuwa akijinyima chakula awali. “Haitokani na uzito wa mwili.” Biblia inatoa mashauri zaidi. “Kujipamba kwenu,” asema Petro, “kuwe utu wa moyoni usioonekana, katika mapambo yasiyoharibika; yaani, roho ya upole na utulivu, iliyo ya thamani kuu mbele za Mungu.”—1 Petro 3:4, Union Version.

Urembo usioharibika ambao Petro anazungumzia hupita sura yenye kuvutia kwa sababu unadumu na ni wenye thamani machoni pa Mungu. Karne nyingi zilizopita mfalme mwenye hekima alisema hivi: “Upendeleo hudanganya, na uzuri ni ubatili; bali mwanamke amchaye BWANA, ndiye atakayesifiwa.”—Mithali 31:30.

Ijapokuwa sura nzuri inaweza kuvutia zaidi leo, bado watu wengi humheshimu mtu mwenye sifa za Kikristo. Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo: “Mjivike wenyewe utu mpya, . . . shauku nyororo za huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, na ustahimilivu.”—Wakolosai 3:10, 12.

Kwa kawaida mitindo haidumu. Hata tuioneje, twaweza kutumia mitindo ya kisasa kwa muda mfupi tu. Sifa yoyote nzuri tunayopata kwa sababu ya sura yetu inaweza kuharibika ikiwa hatuna utu mzuri. Kumbuka kwamba, “matunda ya roho”—kutia ndani sifa ya upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, wema, na kujidhibiti—hayachakai kamwe.—Wagalatia 5:22, 23; 1 Timotheo 2:9, 10.

Hata hivyo, ni kweli kwamba, tunapaswa kuzingatia mavazi yetu. Aline, kutoka Ufaransa, akiri kwamba haikuwa rahisi kuwa na usawaziko kuhusu jambo hilo. “Nilipokuwa tineja,” asema, “nilipendezwa sana na mavazi. Nilitaka kufuatia mitindo ya kisasa kwa sababu ilinifanya nijiamini. Na ikiwa ningeweza kununua mavazi yenye jina la mbuni maarufu, nilifurahi hata zaidi.

“Lakini nilipokuwa mtu mzima,” Aline aendelea kusema, “nililazimika kujifunza kujitegemea kifedha, pia nikaanza kutumia wakati mwingi katika huduma ya Kikristo. Nilitambua kwamba ikiwa nilitaka kuishi kulingana na mapato yangu, singeweza kuendelea kuwa mtumwa wa mitindo. Nilianza kununua nguo zangu bei ziliposhuka na pia kwenye maduka ya bei rahisi. Niligundua kwamba bado ningeweza kuvalia vizuri—lakini kwa robo ya bei. Siri ni kununua mavazi yanayokufaa, mazuri, yanayopatana vizuri na mavazi uliyo nayo tayari, na ambayo hayatapitwa na wakati upesi. Badala ya kuruhusu mitindo iniamulie ninachopaswa kununua, sasa mimi hujaribu kuamua kinachonifaa. Sisemi kwamba sijali mavazi ninayovalia. Lakini utu wangu hautegemei tu sura yangu.”

Katika jamii ambayo hukazia sana sura badala ya sifa za mtu, Wakristo wanapaswa kuzingatia kikumbusho hiki cha Biblia: “Kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na wonyesho wa mtu wa kujivunia njia yake ya kutegemeza maisha—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu. Zaidi ya hilo, ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—1 Yohana 2:16, 17.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Urembo wa kweli hutoka moyoni, wala hautokani na mavazi

[Picha katika ukurasa wa 10]

Chagua mavazi mazuri na yatakayopatana vizuri na mavazi uliyo nayo tayari