Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dini Yangu Ilikuwa Sayansi

Dini Yangu Ilikuwa Sayansi

Dini Yangu Ilikuwa Sayansi

Simulizi la KENNETH TANAKA

“KWELI itawaweka huru.” Maneno hayo yanayopatikana katika muhuri mmoja wa Taasisi ya Tekinolojia ya California, yalinichochea niwe mwanasayansi bora kabisa. Nilipojiandikisha katika taasisi hiyo mwaka wa 1974, ndipo nilipoanza masomo ya kuwa mwanasayansi wa utafiti. Baada ya kupata shahada ya kwanza na ya pili katika somo la jiolojia (sayansi inayohusu miamba ya dunia) niliendelea na masomo yangu katika Chuo Kikuu cha California huko Santa Barbara.

Maoni yangu kuhusu mambo ya kiroho yalikuwa yakibadilika, huku nikifanya maendeleo katika taaluma ya sayansi. Ijapokuwa nilikuwa nimeacha kumwamini Mungu kwa sababu ya masomo yangu ya nadharia ya mageuzi, baadaye ilinibidi kubadili maoni yangu. Nilipataje kuwa mwabudu mwenye bidii wa Mungu huku nikiwa mwanajiolojia? Ebu nieleze.

Nilivutiwa na Anga Nilipokuwa Mvulana Mdogo

Nilianza kuvutiwa na anga nilipokuwa mtoto. Nililelewa huko Seattle, Washington, Marekani, na wazazi wangu walinihimiza nifanye vizuri shuleni. Nilifurahia kusoma juu ya mambo ya anga, kama vile chembe za vitu na uhai, kani nne za msingi, uwazi, wakati, na nadharia ya uwiano. Nilipokuwa na umri wa miaka minane hivi, walimu shuleni walitambua kwamba nilipendezwa sana na sayansi, kwa hiyo, nilipangiwa vipindi vya pekee shuleni kila juma ili nifundishwe na mwalimu wa sayansi.

Nilihudhuria shule ya Jumapili katika Kanisa la Baptisti, lakini hasa kwa sababu nilitaka kushiriki katika starehe kama vile kutembea porini na kupiga hema. Watu wa familia yangu hawakujishughulisha na dini wala Mungu. Nilipojifunza historia na mambo makatili ambayo dini zimefanya, dhamiri yangu ilinisukuma niache kushiriki katika shughuli za kanisa. Pia nilianza kuamini kuwa hakuna Mungu, kwa sababu ilionekana kama sayansi inaweza kueleza karibu kila jambo.

Mradi Mpya na Mabadiliko Mengine

Nilituma maombi ya kujiandikisha katika chuo nikiwa na kusudi la kujifunza fizikia, lakini katika mwaka wangu wa mwisho wa shule ya upili, nilianza pia kujifunza jiolojia. Hilo lilitia ndani kuchunguza miamba ya pekee katika Jimbo la Washington. Niliwaza, ‘Lingekuwa jambo zuri sana kama ningeweza kufurahia maumbile huku nikifanya utafiti wa sayansi.’

Basi, nilipoingia chuoni nilianza kujifunza jiolojia badala ya fizikia. Baadhi ya masomo yalihusisha zama za kijiolojia, na tulijifunza historia ya dunia kwa kuchunguza viumbe waliokufa wanaopatikana katika miamba ya dunia. Nilifundishwa kuwa viumbe hao ni uthibitisho wa mageuzi. Nilijua kwamba nadharia ya mageuzi haikuwa imethibitishwa bado. Hata hivyo, nilionelea kwamba nadharia hiyo ilipatana zaidi na uvumbuzi wa jiolojia kuliko maoni ya wengi juu ya masimulizi ya Biblia kuhusu uumbaji. Niliposikia kwamba kungekuwa na majadiliano chuoni kati ya watu wanaoamini masimulizi hayo na watu wanaoamini mageuzi, nikaamua kutokwenda. Nilijua kwamba dunia haikuumbwa kwa siku sita kama watu fulani wanaoamini masimulizi ya Biblia kuhusu uumbaji wanavyosema!

Ingawa sikupenda mambo ya dini, nilipokuwa nikichunguza miamba huko kusini-magharibi mwa Marekani, nililazimika kubadili maoni yangu na kukubali kwamba kuna Mungu. Nilipokuwa nikitazama mwezi na nyota usiku nilikata kauli kwamba Mungu ndiye aliyeumba ulimwengu. Wataalamu wa nyota walikuwa wamethibitisha kwamba ulikuwa na mwanzo, lakini nilielewa kwamba hakuna mwanasayansi ambaye angeweza kueleza ni kwa nini ulimwengu ulitokea. Lilikuwa jambo la akili kuamini kwamba Muumba mwenye akili na nguvu alikuwa amebuni na kuumba ulimwengu.

Nachora Ramani ya Mihiri na Kutafuta Kusudi la Maisha

Nilikuwa na umri wa miaka 27 nilipopata shahada ya tatu ya sayansi ya jiolojia mwaka wa 1983, na nilikuwa nikichora ramani ya kijiolojia ya Mihiri kwa niaba ya Taasisi ya Uchunguzi wa Jiolojia ya Marekani. Tangu wakati huo nimechapisha makala na ramani nyingi zinazohusu jiolojia ya sayari kwa ajili ya wanasayansi na watu wa kawaida. Nilisaidia katika miradi ya kurusha vyombo vya angani hadi Mihiri, kwa kuwa mimi ni mwanachama wa mabaraza ya ushauri ya Kituo cha Marekani cha Usimamizi wa Anga. Kwa sababu ya utafiti wangu na majukumu kazini, nimekutana na wataalamu mashuhuri wa sayari wa nchi nyingi, vyuo vikuu vingi, na taasisi nyingi za utafiti.

Masomo hayo yote na utafiti niliofanya zilibadili hatua kwa hatua maoni yangu kuhusu uwezo wa sayansi. Nilitambua kwamba sayansi haiwezi na haitaweza kamwe kujibu maswali yote kuhusu maisha. Hasa niliona kwamba sayansi haiwezi kufanya maisha yawe na kusudi la kudumu. Kwa sasa wanasayansi wanaamini kwamba nyota na sayari zitasongamana sana na kuzorota hivi kwamba hakutakuwa na utaratibu wowote tena angani. Ikiwa ulimwengu utakoma kuwapo hatimaye, basi, maisha yana kusudi gani?

Nabadili Mradi Wangu

Mnamo Septemba 1981, nilipokuwa nikiishi huko Flagstaff, Arizona, nilikutana na Mashahidi wa Yehova. Nilikubali kujifunza Biblia nikiwa na kusudi la kuthibitisha kwamba imani yao na Biblia si sahihi. Pia, funzo hilo lingenisaidia hatimaye kujua mafundisho ya Biblia.

Nilianza kutumia saa kadhaa kila juma kujifunza kwa makini mafundisho ya Biblia. Nilishangaa kuona kwamba Biblia ni kitabu chenye ujuzi na hekima. Nilivutiwa kuchunguza habari za Biblia na kuona jinsi zinavyopatana na sayansi na vilevile mamia ya unabii unaohusu mambo ambayo yamekuwa yakitukia katika kipindi cha maelfu ya miaka. Nilivutiwa hasa kuona jinsi unabii mbalimbali katika kitabu cha Danieli na Ufunuo unavyothibitisha kabisa kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.”—2 Timotheo 3:1.

Sikujua kwamba nilipojifunza Biblia nilifanya vile mtu mwingine maarufu alivyokuwa amefanya zamani. Baadaye nilikuta kwamba Bwana Isaac Newton, anayeonwa kuwa mmoja wa wanasayansi wenye akili zaidi ambao wamewahi kuishi, aliheshimu na kuchunguza Biblia sana. Kama Newton, nilikazia fikira unabii mbalimbali wa Danieli na Ufunuo unaohusu matukio na mambo makuu ambayo tayari yametukia. * Hata hivyo, heri mimi kwa kuwa nimeona utimizo wa unabii mbalimbali ambao Newton hakuuona, na mwingine bado unaendelea kutimizwa. Nilitambua kwamba unabii huo mbalimbali unahusu matukio mengi, vipindi vingi, na unatimizwa ulimwenguni pote, pia ni sahihi na haukanushiki. Nilishangaa nilipotambua kwamba Biblia iliyoandikwa na zaidi ya watu 40 katika miaka 1,600 hivi, ina habari zenye kuvutia, zisizojipinga, na zenye kupatana kuhusu masuala makuu yanayokabili wanadamu na wakati wao ujao.

Hata hivyo, haikuwa rahisi kwangu kuacha kuamini nadharia ya mageuzi. Nilijua kwamba nadharia hiyo ilibuniwa kwa kutegemea baadhi ya mambo ambayo wanasayansi wamegundua. Hata hivyo, nilitambua kwamba yote ambayo Biblia inasema kuhusu ulimwengu yanapatana kabisa na mambo ambayo yamethibitishwa na hayakanushiki.

Nilitambua kwamba ili kuelewa kikamili jinsi mafundisho yote ya Biblia yanavyohusiana, hupaswi kupuuza hata fundisho moja kutia ndani masimulizi ya uumbaji katika kitabu cha Mwanzo. Kwa hiyo nilitambua kwamba kukubali Biblia nzima ndilo jambo la akili.

Naendelea Kutafuta Kweli

Wakati uo huo, nilipoendelea kufanya utafiti wa sayansi, niliona kwamba nadharia nyingi zilizoaminiwa na watu wengi kwa muda, baadaye zilithibitishwa kuwa si sahihi. Kazi ya wanasayansi ni ngumu kwa sababu mambo tunayochunguza ni tata, lakini vifaa vyetu vya kufanyia utafiti ni duni. Kwa hiyo, mimi hujihadhari sana nisikubali nadharia mpya haraka hata ingawa zimebuniwa kwa akili sana.

Ni wazi kwamba wanasayansi hawawezi kueleza mambo yote yanayohusiana na maumbile. Kwa mfano, kwa nini chembe zote za viumbe na mimea, na vilevile sheria za asili zinazoziongoza zinafaa sana kuendeleza uhai wa viumbe, na mimea, na kudumisha mazingira? Sayansi haiwezi kumfunua Mungu, lakini Neno lake lililoongozwa kwa roho takatifu linatoa uthibitisho kumhusu Mungu na uumbaji wake. (2 Timotheo 3:16) Tukiwa na ujuzi huo wa kiroho tunaweza kumjua Yule aliyeumba ulimwengu huu maridadi kwa nguvu na hekima.

Nilithibitishiwa hata zaidi kwamba Biblia inapatana na sayansi kwa kusoma kwa makini sana vitabu vya Mashahidi wa Yehova, kama vile Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? na Je, Kuna Muumba Anayekujali? Vitabu hivyo vinazungumzia kindani habari tata za sayansi, utafiti unaoendelea, na maoni ya wataalamu maarufu. Isitoshe, vinazungumzia jinsi mambo ambayo yamethibitishwa kisayansi yanavyopatana na Biblia.

Kwa mfano, viumbe waliokufa wanapatikana katika miamba katika utaratibu uleule ambao waliumbwa kulingana na masimulizi ya kitabu cha Mwanzo. Isitoshe, watu wa kale waliamini kwamba siku ya uumbaji inaweza kumaanisha kipindi kirefu, kama maneno “zama” na “enzi” ambayo yanatumiwa na wanasayansi kueleza historia ya dunia. Kwa hiyo Biblia haipingi sayansi. Inaonyesha kwamba siku za uumbaji zilikuwa vipindi virefu sana. Biblia haiungi mkono watu fulani wanaoamini kwamba siku hizo zilikuwa za saa 24 tu.

Imani Inapaswa Kutegemea Uthibitisho

Kwa kuwa mimi ni mwanasayansi siwezi kukubali imani ambayo haijathibitishwa. Lakini ninaheshimu sana imani ya kweli iliyo na msingi. Imani ya aina hiyo inafafanuliwa hivi katika andiko la Waebrania 11:1: “Imani ni taraja lililohakikishwa la mambo yatumainiwayo, wonyesho dhahiri wa mambo halisi ingawa hayaonwi.” Tunaweza kuamini ahadi za Mungu kwa sababu tuna uthibitisho kwamba Biblia ni Neno lake. Niliona umuhimu wa kuepuka mafundisho ya kawaida ya dini yasiyo na msingi na yanayopinga Maandiko, kama vile Utatu, moto wa milele, nafsi isiyoweza kufa, na mengineyo. Mafundisho mengi ya uwongo kama hayo yalitokana na falsafa na hekaya za kale, au kwa sababu ya kutoelewa Biblia vizuri. Wanasayansi wengi hawaheshimu dini hata kidogo kwa sababu wanaona kwamba watu wengi wa dini wanaamini mafundisho ya uwongo yasiyo na uthibitisho wowote ule.

Mojawapo ya madaraka makuu ambayo nimekuwa nayo ni kueleza, kutetea, na kusambaza matokeo ya utafiti wangu wa kisayansi. Vilevile, nilisukumwa kuwafundisha watu kweli za Biblia, kwa kuwa ujuzi wa Biblia ni muhimu sana kuliko ujuzi mwingine wowote. Nilianza kufanya kazi hiyo yenye kuridhisha miaka 20 iliyopita nilipobatizwa ili niwe mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kisha, tangu Septemba 2000 nimetumia saa 70 kwa wastani kila mwezi katika kazi ya kuhubiri. Tangu wakati huo nimekuwa na pendeleo la kuongoza mafunzo ya Biblia pamoja na watu wanaopendezwa. Miezi fulani nimekuwa na wanafunzi kumi na baadhi yao sasa ni walimu wa Biblia wenye bidii.

Bado ninafurahia kuchunguza Mihiri na sehemu nyinginezo za ulimwengu kupitia vyombo vya angani ambavyo vimerushwa ili kuvumbua nyota na sayari zilizo karibu na dunia. Bado kuna mambo mengi ambayo wanasayansi wanahitaji kuchunguza. Ninatazamia kuishi wakati ambapo jitihada za wanadamu za kupata ujuzi wa kiroho na wa kisayansi zitatupatia majibu ya maswali yetu magumu. Nimeelewa kwamba ninaweza kuwa na kusudi maishani nikiwa na ujuzi sahihi kumhusu Mungu na makusudi yake kwa wanadamu. Hiyo ndiyo maana ya maneno haya ya Yesu ambayo yamechongwa katika muhuri mmoja wa Taasisi ya Tekinolojia ya California: “Kweli itawaweka huru.”—Yohana 8:32, Union Version.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Katika kitabu chake Observations Upon the Prophecies of Daniel, and the Apocalypse of St. John, kilichochapishwa mwaka wa 1733, Bwana Isaac Newton alichanganua unabii mbalimbali wa kitabu cha Biblia cha Danieli na Ufunuo.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

“Ilionekana kama sayansi inaweza kueleza karibu kila jambo”

[Blabu katika ukurasa wa 20]

“Sayansi haiwezi na haitaweza kamwe kujibu maswali yote kuhusu maisha”

[Blabu katika ukurasa wa 21]

“Nilishangaa kuona kwamba Biblia ni kitabu chenye ujuzi na hekima”

[Ramani katika ukurasa wa 18]

Ramani ya Mihiri

[Picha katika ukurasa wa 20]

Kama Newton, nilivutiwa na kitabu cha Biblia cha Danieli na Ufunuo

[Hisani]

University of Florida

[Picha katika ukurasa wa 21]

Ninawaelezea wengine yale ambayo nimejifunza katika Biblia

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 18]

Top left: Courtesy USGS Astrogeology Research Program, http://astrogeology.usgs.gov; Mars map: National Geographic Society, MOLA Science Team, MSS, JPL, NASA; Mars surface: NASA/JPL/Caltech

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 21]

Space photo: J. Hester and P. Scowen (AZ State Univ.), NASA