Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Nitiwe Alama ya Chanjo?

Je, Nitiwe Alama ya Chanjo?

Vijana Huuliza . . .

Je, Nitiwe Alama ya Chanjo?

“Alama nyingine za chanjo ni maridadi. Zinapendeza sana.”—Jalene. *

“Kwa miaka miwili nilitamani sana kutiwa alama ya chanjo.”—Michelle.

INAONEKANA kila mahali watu wana alama za chanjo. Wanamuziki mashuhuri wa roki, wanamichezo, wanamitindo, na waigizaji wa sinema, wote hujivunia alama hizo. Vijana wengi pia wametiwa alama hizo kwenye mabega, mikono, viuno, na kwenye viwiko vya miguu, nao hujivunia alama hizo. Andrew anasema hivi: “Alama za chanjo ni nzuri. Kutiwa alama hizo ni uamuzi wa mtu binafsi.”

Kitabu World Book Encyclopedia kinasema hivi: “Kutia alama za chanjo ni kuweka madoido ya kudumu mwilini. Mtu hutiwa alama hizo kwenye ngozi kwa kutumia kijiti au mfupa ulionolewa, au sindano iliyotumbukizwa kwenye rangi ya kiasili.”

Ingawa ni vigumu kujua idadi kamili ya watu ambao wametiwa alama za chanjo, habari fulani inasema kwamba asilimia 25 ya vijana wote wenye umri wa miaka 15 hadi 25 nchini Marekani wana alama hizo. Sandy anasema hivi: “Hilo ni jambo linalopendwa na wengi.” Kwa nini vijana wengi wanapenda kutiwa alama za chanjo?

Kwa Nini Zinapendwa?

Baadhi ya watu hutiwa alama hizo ili kuonyesha kwamba wanampenda sana mtu fulani wa jinsia tofauti. Michelle anasema hivi: “Ndugu yangu ana jina la msichana ambaye alikuwa rafiki yake zamani kwenye kiwiko cha mguu.” Jambo hilo limeleta tatizo gani? “Wao si marafiki tena.” Kulingana na gazeti Teen, “madaktari wanakadiria kwamba zaidi ya asilimia 30 ya watu wanaotaka kuondoa alama zao za chanjo ni wasichana ambao wanataka majina ya wavulana waliokuwa marafiki wao zamani yafutwe.”

Vijana fulani huona alama za chanjo zikiwa maridadi sana. Wengine huziona kuwa ishara ya kuwa huru kujiamulia mambo. “Ninahisi nina uhuru wa kujiamulia mambo,” alisema Josie, na kuongeza kwamba kupata alama ya chanjo ni “uamuzi pekee wa maana niliowahi kufanya maishani mwangu.” Vijana wengine hutiwa alama za chanjo ili waonekane tofauti—wanataka kuhisi wako huru kuamua vile sura yao itakavyokuwa. Pia alama za chanjo zinaweza kuwa ishara ya uasi au mwenendo usiokubalika katika jamii. Hivyo alama nyingine za chanjo huwa na maneno au picha chafu.

Hata hivyo, huenda vijana wengi wanaiga mtindo fulani tu. Lakini kwa kuwa watu wengine wana alama za chanjo, je, inamaanisha wewe pia unapaswa kuwa nazo?

Zoea la Tangu Zamani

Kutiwa alama za chanjo si jambo jipya. Maiti zilizohifadhiwa miaka mingi kabla ya Kristo, zimepatikana nchini Misri na Libya zikiwa na alama za chanjo. Nyingine zimepatikana huko Amerika Kusini. Alama zote hizo zilihusiana moja kwa moja na ibada ya miungu ya kipagani. Kulingana na mtafiti Steve Gilbert, “alama ya chanjo ya kale zaidi yenye michoro ya vitu hususa iliwakilisha mungu aliyeitwa Bes. Kulingana na hekaya za Misri, Bes alikuwa mungu mwovu wa anasa.”

Basi si ajabu kwamba Sheria ya Musa inasema kwamba watu wa Mungu hawakupaswa kutiwa alama za chanjo. Andiko la Mambo ya Walawi 19:28, Biblia Habari Njema linasema hivi: “Msijitie alama zozote mwilini mwenu kwa ajili ya kuomboleza au kujikatakata mwilini au kujichanja chale. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.” Waabudu wapagani, kama vile Wamisri walizoea kuandika majina au alama za miungu yao kwenye kifua au mikono yao. Waisraeli wangekuwa tofauti na mataifa mengine kwa kutii sheria ya Yehova iliyokataza kutiwa alama za chanjo.—Kumbukumbu la Torati 14:1, 2.

Ijapokuwa Wakristo leo hawako chini ya Sheria ya Musa, wanapaswa kuifikiria kwa uzito sheria iliyokataza kutiwa alama za chanjo. (Waefeso 2:15; Wakolosai 2:14, 15) Iwapo wewe ni Mkristo, bila shaka hungependa kutiwa alama zinazotumiwa katika ibada ya kipagani au ya uwongo mwilini mwako, hata kama ni kwa muda mfupi tu.—2 Wakorintho 6:15-18.

Madhara ya Kiafya

Pia unapaswa kufikiria madhara ya kiafya. Profesa msaidizi wa utaalamu wa ngozi, Dakt. Robert Tomsick, anasema hivi: “Unadungwa ngozi na kutiwa rangi kwenye kidonda hicho. Hata kama sindano hupenya kidogo tu kwenye ngozi, kuna hatari ya kupata maambukizo ya bakteria au virusi. Kwa ufupi, naona [kutiwa alama ya chanjo] ni hatari.” Dakt. Tomsick anaendelea kusema hivi: “Baada ya rangi kutiwa ngozini, hata kama hakutakuwa ambukizo lolote, kuna uwezekano kwamba ngozi itaumbuka, kuvimba, kuwa na magamba, na kuwasha kwa sababu ya kuguswa na vitu fulani au kutokana na ugonjwa wa ngozi.”

Ingawa alama za chanjo ni za kudumu, kuna njia kadhaa ambazo hutumiwa kujaribu kuzifuta, kama vile kuziondoa kwa kutumia miale ya leza, upasuaji, kuzisugua kwa burashi ya nyaya ili kuondoa matabaka mawili ya juu ya ngozi, kuzilowesha kwa maji ya chumvi, au kuzifuta kwa asidi na kuacha kovu mahali pa alama za chanjo. Njia hizo hugharimu pesa nyingi na zinaweza kusababisha maumivu makali. Gazeti Teen linasema kwamba “mtu husikia uchungu mwingi anapojaribu kuiondoa alama ya chanjo kwa kutumia miale ya leza kuliko wakati anapotiwa alama hiyo.”

Wengine Watakuonaje?

Unapaswa kufikiri sana kabla hujatiwa alama ya chanjo kwa kuwa watu wengine hawazipendi. (1 Wakorintho 10:29-33) Nchini Taiwan, mwanamke anayeitwa Li alitiwa alama ya chanjo alipokuwa na umri wa miaka 16. Sasa ana umri wa miaka 21 na anafanya kazi ofisini. Anasema hivi: “Mimi huudhika ninapoona jinsi wafanyakazi wenzangu wanavyoiangalia alama yangu ya chanjo.” Mtaalamu wa akili Mwingereza Theodore Dalrymple anasema kwamba watu wengi huona alama za chanjo “kuwa ishara zinazoonyesha kwamba . . . mtu anashirikiana na watu wajeuri, wakatili, waasi, na wahalifu.”

Makala moja katika gazeti American Demographics inasema hivi: “Ni wazi kwamba Wamarekani wengi huona ni hatari kudungwa mwilini ili kujirembesha. Asilimia 85 [ya vijana] wanakubali kwamba ‘watu wenye alama za chanjo . . . wanapaswa kujua kwamba njia hizo za kujitambulisha huenda zikawaletea magumu katika kazi yao au mahusiano yao.’”

Pia fikiria kama kutiwa alama ya chanjo kunaweza kuathiri jinsi wengine wanavyokuona ukiwa Mkristo. Je, kunaweza kuwa ‘sababu ya kukwaza’ wengine? (2 Wakorintho 6:3) Ni kweli kwamba vijana wengine wametiwa alama za chanjo katika sehemu za mwili ambazo hufunikwa na mavazi. Huenda hata wazazi wao wasijue wana alama hizo za siri. Hata hivyo, jihadhari! Huenda siri yako ikafunuliwa kutakapokuwa na uhitaji wa kumwona daktari kwa dharura au unapooga kwenye bafu shuleni! Afadhali “kujiendesha wenyewe kwa kufuata haki katika mambo yote,” badala ya kuwapumbaza wengine kipumbavu.—Waebrania 13:18.

Kama ilivyo na mitindo mingine yote, alama za chanjo huenda zisipendeze baada ya muda fulani. Kwa kweli, hata kama unalipenda sana vazi fulani, iwe ni suruali ya jinzi, shati, rinda, au viatu, huwezi kulivaa maisha yako yote. Mitindo, mishono, na rangi za nguo huacha kuvutia. Hata hivyo, tofauti na mavazi, alama za chanjo hazifutiki kwa urahisi. Isitoshe, jambo lililokuvutia ulipokuwa na umri wa miaka 16 huenda lisikuvutie unapokuwa na umri wa miaka 30.

Wengi wamejuta kwa kutiwa alama za chanjo ambazo zinadumu maisha yao yote. “Nilitiwa alama ya chanjo kabla sijajifunza kumhusu Yehova,” Amy anaeleza. “Mimi hujaribu kuificha. Mimi huaibika wengine kutanikoni wanapoiona.” Tunajifunza nini? Fikiri kabla ya kutiwa alama ya chanjo. Usifanye jambo ambalo utalijutia baadaye.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mara nyingi alama za chanjo huonwa kuwa ishara ya uasi

[Picha katika ukurasa wa 26]

Baada ya muda fulani, wengi hujuta kwa kutiwa alama ya chanjo

[Picha katika ukurasa wa 27]

Fikiri kabla ya kutiwa alama ya chanjo