Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Anakubali Ngono Isiyo ya Asili?

Je, Mungu Anakubali Ngono Isiyo ya Asili?

Maoni ya Biblia

Je, Mungu Anakubali Ngono Isiyo ya Asili?

“NI LINI nitakapojua ngono inayonifaa?” Hivyo ndivyo msichana mwenye umri wa miaka 13 alivyouliza katika makala ya kuwashauri vijana. Swali lake linaonyesha mtazamo wa wengi wanaodhani kwamba wako huru kufanya ngono ya aina yoyote ile.

Huenda watu fulani wakatatanishwa na hisia zao za ngono. Wengine hufanya ngono zisizo za asili kama vile ngono kati ya watu wa jinsia moja. Na wengine huvalia na kutenda kama watu wa jinsia tofauti bila kujali. Hata wengine hufanyiwa upasuaji wa kubadilisha jinsia. Isitoshe, kuna wale ambao hudai kwamba watu wazima wanapaswa kuruhusiwa kufanya ngono na watoto.

Je, kweli watu wanapaswa kujichagulia ngono na jinsia? Neno la Mungu linasema nini kuhusu mambo hayo?

“Mwanamume na Mwanamke Aliwaumba”

Kitabu cha Biblia cha Mwanzo kinasema kwamba Mungu mwenyewe ndiye aliyewaumba wanaume na wanawake wakiwa tofauti. Simulizi hilo linasema hivi: “Mungu akaumba mtu kwa mfano wake . . . mwanamume na mwanamke aliwaumba. Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha.”—Mwanzo 1:27, 28.

Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na uhuru wa kuchagua na akawapa fursa za kufurahia uhuru wao. (Zaburi 115:16) Mwanadamu alipewa kazi ya kuwatunza viumbe wote duniani, na hata akapewa ruhusa ya kuwapa majina yanayofaa. (Mwanzo 2:19) Lakini Mungu alitoa mwongozo hususa kuhusu masuala ya ngono.—Mwanzo 2:24.

Kwa kuwa Adamu hakutii, sote tumerithi kutokamilika. Hivyo inatubidi kupambana na udhaifu wetu wa kimwili na tamaa zenye nguvu ambazo hazipatani na kusudi la Mungu la awali. Hiyo ndiyo sababu katika sheria alizompa Musa, Mungu alitaja waziwazi ngono zinazomchukiza kama vile uzinzi, ngono ya watu wa ukoo, ngono kati ya watu wa jinsia moja, na ngono na wanyama. (Mambo ya Walawi 18:6-23) Pia Mungu alikataza waziwazi kujifanya mtu wa jinsia tofauti kwa makusudi yasiyo ya adili. (Kumbukumbu la Torati 22:5) Biblia hufundisha kwamba ngono pekee ambayo Mungu anakubali ni kati ya watu wa jinsia tofauti ambao wameoana. (Mwanzo 20:1-5, 14; 39:7-9; Mithali 5:15-19; Waebrania 13:4) Je, kanuni hizo zinafaa?

Je, Ni Uamuzi wa Kibinafsi?

Biblia hulinganisha uhusiano wa mwanadamu na Mungu na udongo ulio mikononi mwa mfinyanzi. Inasema hivi: “Ewe mtu, kwa kweli wewe ni nani hata uwe ukimjibu Mungu? Hakika je, kitu kilichofinyangwa kitamwambia yeye aliyekifinyanga, ‘Kwa nini ulinifanya mimi kwa njia hii?’” (Waroma 9:20) Ni wazi kwamba Mungu aliwaumba wanaume na wanawake kwa njia ambayo wanavutiana kingono. Kwa hiyo, si jambo la kiasili kwa mtu kuvutiwa kingono na mtu wa jinsia ileile, mnyama, au mtoto.—Waroma 1:26, 27, 32.

Kwa sababu hiyo, watu wanaotamani ngono za aina hiyo hushindana na Mungu. Biblia inaonya hivi: “Ole wake ashindanaye na Muumba wake! Kigae kimoja katika vigae vya dunia! Je! Udongo umwambie yeye aufinyangaye; Unafanya nini?” (Isaya 45:9) Ama kweli, inafaa Muumba wa wanadamu awape maagizo kuhusu ngono. Pia, inafaa wanadamu wafuate maagizo hayo, sivyo?

Kupata Umiliki wa Chombo Chako

Mwandishi wa Biblia Paulo alitumia mfano kama huo alipowashauri Wakristo kuhusu mambo ya ngono. Alisema hivi: “Kila mmoja wenu apaswe kujua jinsi ya kupata umiliki wa chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima, si katika hamu yenye tamaa ya ngono.” (1 Wathesalonike 4:4, 5) Paulo analinganisha mwili na chombo. Kumiliki chombo hicho humaanisha kupatanisha mawazo na tamaa zako na sheria za Mungu za maadili.

Ni kweli kwamba huenda isiwe rahisi kufanya hivyo. Mtu aliyetendewa vibaya kingono alipokuwa mtoto, mtu aliyekuwa na wazazi au walezi wenye maoni mabaya kuhusu wanaume au wanawake, au yule aliyetazama picha chafu alipokuwa mtoto mchanga huenda akaona ni vigumu kufanya hivyo. Hisia za ngono zinaweza kuathiriwa pia na chembe za urithi, homoni, na hali ya mtu ya akili. Hata hivyo, inafariji kujua kwamba Muumba wetu anaweza kuwasaidia na kuwategemeza wale wanaohitaji msaada.—Zaburi 33:20; Waebrania 4:16.

Acha Mfinyanzi Mkuu Akufinyange

Kabla ya mfinyanzi kuanza kufinyanga udongo, ni lazima auweke katikati ya gurudumu la mfinyanzi. Kisha gurudumu linapozunguka, mfinyanzi hutumia vidole vyake kuufinyanga kwa utaratibu katika umbo analotaka. Kabla hatujafinyangwa na kuwa watu wanaompendeza Mungu, tunapaswa kufuata kanuni na sheria za Mungu zisizobadilika. Tunapoanza kutia bidii, kwa upendo Mungu hutufinyanga kwa utaratibu akitumia Biblia, roho yake takatifu, na ndugu zetu Wakristo. Ndipo mtu anapoanza kuona kwamba Mungu anamtunza maishani.

Bila shaka, ni lazima tusitawishe tumaini letu katika hekima ya Muumba, tukisadiki kwamba anajua mambo yanayotufaa. Tumaini hilo husitawishwa kupitia sala na kujifunza Biblia kwa bidii. Mtu anayepambana na hisia zisizofaa za ngono kwa mtazamo huo hufinyangwa na Muumba kwa njia inayofaa. Andiko la 1 Petro 5:6, 7 linasema hivi: “Kwa hiyo, jinyenyekezeni chini ya mkono wa Mungu wenye uweza, ili apate kuwakweza nyinyi katika wakati upasao; huku mkitupa hangaiko lenu lote juu yake, kwa sababu yeye huwajali nyinyi.”

Tunaposoma Biblia kwa ukawaida, tunapata kuwajua watumishi wengi waaminifu wa Mungu ambao walipambana na tamaa za mwili bila kuchoka. Mifano yao inatutia moyo sana! Tunaweza kuwazia mfadhaiko ambao mtume Paulo alihisi nyakati nyingine aliposema hivi: “Mwenye taabu mimi! Ni nani ataniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki?” Lakini alituonyesha chanzo kikuu cha msaada alipojibu swali lake: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!”—Waroma 7:24, 25.

Kani Itakayokusaidia Kubadilika

Tunaweza pia kuruhusu roho takatifu ya Mungu ituongoze. Ni kani yenye nguvu itakayokusaidia kubadilika. Roho takatifu hutusaidia ‘tuweke mbali utu wa hapo zamani’ na ‘tuvae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na uaminifu-mshikamanifu.’ (Waefeso 4:22-24) Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo hakosi kamwe kuwapa roho takatifu wale wanaomwomba kwa unyoofu ili iwasaidie kufanya mabadiliko. Yesu anatuhakikishia kwamba Baba “atawapa roho takatifu wale wanaomwomba.” (Luka 11:13) Hata hivyo, ni muhimu kudumu katika sala kama maneno yake yanavyoonyesha: “Fulizeni kuomba, nanyi mtapewa.” (Mathayo 7:7) Ni muhimu kufanya hivyo hasa unapojitahidi kudhibiti tamaa za ngono zenye nguvu.

Mungu pia hutusaidia kupitia ndugu zetu wa kweli Wakristo ambao wanatoka katika jamii zote. Hapo awali, Wakristo fulani katika kutaniko la karne ya kwanza la Korintho walikuwa “wanaume watunzwao kwa makusudi yasiyo ya asili” na “wanaume walalao pamoja na wanaume.” Lakini walibadilika. Damu ya Kristo iliwatakasa, nao wakakubaliwa na Mungu. (1 Wakorintho 6:9-11) Watu fulani leo wanahitaji kufanya mabadiliko kama hayo. Watu hao wanaweza kutegemezwa na kutaniko la Kikristo wanapopambana na tamaa mbaya.

Je, hilo linamaanisha kwamba mtu anapokuwa Mkristo tamaa mbaya au mawazo yasiyofaa kuhusu jinsia yatatoweka yenyewe? Si lazima. Baadhi ya watu ambao wamejitahidi kutumia kanuni za Biblia wameshinda tamaa mbaya. Lakini mara nyingi imewabidi Wakristo hao wapambane na tamaa hizo kila siku. Kwa hiyo, wanamtumikia Mungu wajapokuwa na “mwiba katika mwili.” (2 Wakorintho 12:7) Mradi wanaendelea kupambana na mielekeo mibaya na kudumisha uadilifu, Mungu huwaona kuwa watumishi waaminifu walio safi. Wanaweza kutazamia wakati ambapo wanadamu ‘watawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.’—Waroma 8:21.

Kwa sasa, ni lazima wote wale wanaotaka kumpendeza Mungu wafuate kanuni zake za uadilifu. Wakristo wa kweli huchagua kumtumikia Mungu wala hawafuati tamaa zao za ubinafsi. Wale wanaotii mapenzi ya Mungu kwa unyenyekevu katika shughuli zote maishani watapata shangwe na furaha milele.—Zaburi 128:1; Yohana 17:3.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Mungu alitoa mwongozo hususa kuhusu masuala ya ngono

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Hapo awali, Wakristo fulani katika kutaniko la karne ya kwanza la Korintho walikuwa “wanaume watunzwao kwa makusudi yasiyo ya asili” na “wanaume walalao pamoja na wanaume.” Lakini walibadilika

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kujifunza Biblia humsaidia mtu kusitawisha kanuni bora za maadili