Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Matatizo ya Wakulima

Matatizo ya Wakulima

Matatizo ya Wakulima

RICHARD hulima shamba lililolimwa na babu wa baba yake miaka 100 hivi iliyopita. Lakini, mnamo mwaka wa 2001, mkulima huyo Mkanada alikuwa mtu wa kwanza kutovuna chochote katika vizazi vinne vya familia yao. Mimea yake iliharibiwa na ukame. Na matatizo yake yamezidi kwa sababu katika miaka iliyotangulia bei za mazao zimeshuka na gharama zimeongezeka. Richard alilalamika hivi: “Matatizo yanazidi kuongezeka na hakuna suluhisho.”

Larry alikuwa na shamba ambalo lilikuwa limemilikiwa na familia yake kwa miaka 115 katika eneo linalokuza mahindi kwa wingi nchini Marekani. Anasema hivi: “Nilihisi nina wajibu wa kuendelea kulima shamba hilo na kulifanya litokeze faida nyingi . . . , lakini sikufua dafu.” Larry na mkewe walipoteza shamba lao.

Wakulima wengi wanakabili matatizo kama ya Larry na Richard. Kuenea kwa ugonjwa wa mifugo wa midomo na miguu nchini Uingereza kuliwaletea wakulima hasara kubwa ya kifedha na mfadhaiko. Taarifa moja ya habari ilisema: “Kila siku wakulima nchini Uingereza wanakumbwa na mahangaiko, upweke, na matatizo ya madeni, hata wale ambao hawajakabili ugonjwa huo wa mifugo.” Katika nchi fulani zinazoendelea, vita, ukame, ongezeko la haraka la idadi ya watu, na matatizo mengine mengi yamewatatiza wakulima. Serikali zinalazimika kununua chakula kutoka nje, na familia nyingi haziwezi kukinunua.

Kwa hiyo, matatizo ya wakulima yanawaathiri watu wengi. Hata hivyo, ni wakazi wachache wa mjini wanaojali dhiki za wakulima. Miaka 50 hivi iliyopita, Rais wa Marekani Dwight D. Eisenhower alitoa taarifa hii mwafaka: “Kilimo huonekana kuwa rahisi sana ikiwa unafanya kazi ofisini, na ikiwa unaishi mbali sana na shamba la mahindi.” Vivyo hivyo, leo wakulima wanahisi kwamba watu wengi ulimwenguni hawaelewi kilimo na umuhimu wa wakulima. Mkulima mmoja Mkanada analalamika hivi: “Hatujali chakula chetu chatoka wapi. Kazi kubwa huwa imefanywa kabla chakula hakijapakiwa na kuuzwa dukani.”

Matatizo ya wakulima hayawezi kupuuzwa kwani sote tunategemea bidhaa za kilimo. Wanasoshiolojia Don A. Dillman na Daryl J. Hobbs wanaonya hivi: “Katika jamii yetu inayotegemeana sana, matatizo ya mashambani husambaa upesi mjini, na matatizo ya mjini husambaa haraka mashambani. Jamii za mjini au za mashambani haziwezi kuendelea kwa muda mrefu ikiwa mojawapo inakabili matatizo.” Isitoshe, katika ulimwengu wa leo ulio kama kijiji, uchumi wa taifa moja unapozorota, unaweza kuathiri sana uuzaji wa mazao na gharama za uzalishaji katika nchi nyingine.

Basi, si ajabu kwamba kituo fulani cha kilimo huko New York kilisema hivi: “Kilimo ni mojawapo ya kazi 10 zinazosababisha mfadhaiko mwingi nchini Marekani.” Ni nini baadhi ya visababishi vya matatizo ya wakulima? Wakulima wanawezaje kukabiliana na matatizo hayo? Je, kweli matatizo hayo yanaweza kukomeshwa?

[Blabu katika ukurasa wa 4]

“Kilimo huonekana kuwa rahisi sana ikiwa unafanya kazi ofisini, na ikiwa unaishi mbali sana na shamba la mahindi”