Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Matatizo ya Wakulima Yatakoma

Matatizo ya Wakulima Yatakoma

Matatizo ya Wakulima Yatakoma

“BAADHI ya watu wanaoona matatizo ya wakulima kijuujuu, hawaelewi kwa nini wakulima huendelea kulima,” anasema Rodney, mkulima wa kizazi cha tatu. Hata hivyo, mamilioni ya watu ulimwenguni pote huendelea kulima. Katika nchi fulani zinazoendelea, hakuna kazi za kutosha; angalau familia zinazolima zinaweza kupata chakula kila siku.

Isitoshe, familia nyingi huona kilimo kuwa sehemu ya maisha wala si kazi tu. Idadi ya watu wanaoendelea kulima licha ya ukame, magonjwa, hali mbaya za kiuchumi, na matatizo mengine inaonyesha uvumilivu wao na kwamba wanapenda maisha ya mashambani. Kabla ya kuchunguza jinsi matatizo ya wakulima yatakavyosuluhishwa, na tuchunguze jinsi wakulima fulani wamesaidiwa kukabiliana na hali hiyo.

Jinsi Wengine Wanavyokabiliana na Matatizo

Wakulima hukabili matatizo fulani yasiyoepukika. Ni lazima tukubali kwamba hali ya hewa, uchumi, na mambo mengine mengi yanayosababisha mfadhaiko hayawezi kudhibitiwa. Ripoti iliyochapishwa na Mpango wa Elimu ya Ziada wa North Carolina inasema: “Wakulima wengi wametambua kwa masikitiko kwamba kazi ngumu haifanikiwi sikuzote. Jitihada nyingi ambazo kila mkulima huweka katika kazi yake, haziwi na matokeo mazuri nyakati zote. Kila mkulima hukabili hali ambazo hawezi kuzidhibiti.” Mkulima mmoja mzee alieleza siri ya furaha yake aliposema hivi: “Nimejifunza kubadilika kulingana na hali zisizoweza kuepukika.”

Mithali moja ya kale inasema hivi: “Mwenye kuuangalia upepo hatapanda; naye ayatazamaye mawingu hatavuna.” (Mhubiri 11:4) Mtu mwenye wasiwasi na mwenye kusitasita hawezi kutenda lolote. Kuchukua hatua zinazofaa na kuepuka maoni mabaya kwaweza kupunguza mfadhaiko.

Kula vizuri, kupumzika vya kutosha, na kufanya mazoezi yafaayo kunasaidia sana pia. Gazeti The Western Producer linaripoti kwamba wakulima wenye afya “hufanya maamuzi mazuri.” Mkulima anayeitwa Eugene na mkewe, Candace, waliliambia gazeti la Amkeni! hivi: “Kupumzika vya kutosha hutusaidia kupunguza mfadhaiko. Matatizo huonekana madogo na rahisi kusuluhishwa baada ya kupumzika. Kula vizuri husaidia pia, hasa familia yote inapokula pamoja.” Shauri hilo linapatana na maneno haya ya Biblia: “Tena ni karama ya Mungu kila mtu apate kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote.”—Mhubiri 3:13.

Kuiruzuku Familia

Mkulima mmoja aliliambia gazeti la Amkeni! hivi: “Familia nyingi za mashambani zimelazimika kufanya kazi nyingine mbali na kilimo. Ingawa hatua hiyo huchukuliwa ili kupunguza matatizo ya kifedha, inaweza kuathiri mahusiano katika familia. Familia fulani za mashambani zilikuwa na umoja hapo awali, lakini sasa zimesambaratika.” Familia zinawezaje kukabiliana na matatizo hayo?

Yapata miaka 2,700 iliyopita, vichwa vya familia walishauriwa hivi: “Tengeneza kazi yako huko nje, jifanyizie kazi yako tayari shambani, ukiisha, jenga nyumba yako.” (Mithali 24:27) Randy, ambaye ni baba na mkulima wa kizazi cha nne, anasema: “Ni lazima umshukuru kila mtu katika familia. Kila mtu katika familia anahitaji kutiwa moyo na kupendwa. Maneno na matendo ya fadhili huwafanya wote wahisi kwamba wanahitajiwa na kuthaminiwa.”

Watoto hasa wanahitaji kutiwa moyo mabadiliko makubwa yanapotokea. Familia inapopoteza shamba, watoto huathiriwa kama watoto wa wazazi waliotalikiana au kufa. Wanahitaji kujua kwamba hawakusababisha tatizo hilo na kwamba familia haitavunjika.

Jinsi Wengine Wanavyoweza Kusaidia

Huenda wakulima waliofadhaika wakajitenga na wengine, hata kuwaepuka marafiki zao. (Mithali 18:1) Hata hivyo, wakati wa shida mtu anahitaji sana kutiwa moyo na wengine!

Je, una marafiki au majirani wakulima ambao wamekumbwa na matatizo? Unaweza kuwatia moyo sana ukionyesha kwamba unawajali. Mkulima anayeitwa Ron anasema hivi: “Tunafarijiwa tunapojua kwamba marafiki zetu wanatambua matatizo yetu.” Naam, watembelee marafiki zako na uwasikilize wanapoeleza yaliyo moyoni mwao.

Jack alifaidika alipotembelewa na kutiwa moyo. Anasema hivi: “Nakumbuka vizuri sana wakati ambapo marafiki zangu waliona kwamba nimefadhaika na kwa upendo wakaja kunitia moyo.” Si lazima mtu awe na ujuzi mwingi kuhusu kilimo ili awafariji wengine. Rodney, aliyenukuliwa mwanzoni, anasema hivi: “Mimi hupata nguvu na tamaa ya kufanya yote niwezayo ninapojua kwamba marafiki zangu wanatambua kazi nyingi nilizo nazo.” Hilo linatukumbusha mithali hii ya Biblia: “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.”—Mithali 17:17.

Suluhisho la Kudumu

Matatizo ya wakulima ni kati ya mambo yanayoonyesha kwamba wanadamu hawawezi kuisimamia vizuri dunia na rasilimali zake. Nabii Yeremia alisema hivi: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Ama kwa hakika, mwanadamu anahitaji msaada wa Mungu. Hapana shaka kwamba msaada huo utatolewa hivi karibuni.

Biblia inasema: “BWANA Mungu akamtwaa huyo mtu, akamweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza.” (Mwanzo 2:15) Naam, agizo hilo la Muumba wetu ndilo lililoanzisha kilimo! Karne nyingi baadaye, Mungu aliwaingiza watu wake Waisraeli katika nchi ya Kanaani. Biblia inasema hivi kuhusu nchi hiyo: “Hunyweshwa maji ya mvua ya mbinguni; nayo ni nchi itunzwayo na BWANA, Mungu wako; macho ya BWANA Mungu wako, ya juu yake, tangu mwanzo wa mwaka hata mwisho wa mwaka.” (Kumbukumbu la Torati 11:11, 12) Yehova pia alitunga sheria zilizozuia Nchi ya Ahadi isiharibiwe. Kwa mfano, kila mwaka wa saba, Waisraeli hawakupaswa kulima mashamba yao, mashamba ya mizabibu, na mashamba ya mizeituni. (Kutoka 23:10, 11) Hivyo, udongo wa nchi hiyo uliendelea kuwa na rutuba.

Tunaweza kuwa na uhakika kwamba wakati ujao dunia itapata mazao mengi kutokana na kilimo wakati wa utawala wa Ufalme wa Mungu, serikali inayoongozwa na Yesu Kristo kutoka mbinguni. (Isaya 35:1-7) Yesu Kristo, Mtawala aliyewekwa kuongoza Ufalme huo, alipokuwa duniani, alionyesha kwamba anaweza kudhibiti nguvu za asili zinazoathiri kilimo. (Marko 4:37-41) Zaburi 72 inaeleza jinsi hali zitakavyokuwa wakati atakapotumia uwezo wake kurekebisha dunia na kuponya wakazi wake. Inatuhakikishia hivi: “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima; matunda yake na yawaye-waye kama Lebanoni, na watu wa mjini wasitawi kama majani ya nchi.” (Zaburi 72:16) Watu wa Mungu watavuna kwa wingi na kwa shangwe katika ulimwengu huo mpya ulioahidiwa.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

“Wakulima wengi wametambua kwa masikitiko kwamba kazi ngumu haifanikiwi sikuzote”

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kushughulikia mahitaji ya kiroho na ya kihisia ya watu wa familia kunaweza kuwasaidia kukabiliana na matatizo

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wakati wa utawala wa Mungu, dunia itazaa chakula tele

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 9]

Garo Nalbandian