Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jina la Yehova Huko Pasifiki

Jina la Yehova Huko Pasifiki

Jina la Yehova Huko Pasifiki

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI FIJI

UMATI uliduwaa. Wageni waliotembelea kisiwa kimoja cha Pasifiki walifunga macho yao kabla ya kula chakula kwenye karamu waliyokuwa wameandaliwa. Wakazi wa kisiwa hicho waliuliza hivi: “Mnafanya nini?”

“Tunamshukuru Mungu kwa ajili ya zawadi Zake,” walijibu.

“Mungu wenu anaishi wapi?” wakazi hao wakauliza.

“Mbinguni,” wakajibiwa.

“Anaitwa nani?”

“Yehova.”

“Je, Mungu wenu hula chakula?” wakazi wakauliza.

“Mungu ni Roho,” wakajibu wageni. “Yeye si kama sisi; Yeye huishi milele. Ndiye aliyeiumba dunia, anga, bahari, na vitu vyote. Ndiye aliyetuumba.”

Wakazi wa kisiwani walishangaa kusikia kweli hizo sahili na wakataka kujua kwa nini wageni walitembelea kisiwa chao. Wageni walijibu hivi: “Tumekuja kuwajulisha Mungu wa kweli Yehova, na kuhusu Mwanawe Yesu aliye Mwokozi wetu.”—From Darkness to Light in Polynesia.

Wageni hao walikuwa nani? Je, walikuwa Mashahidi wa Yehova? La. Walikuwa Watahiti wawili waliokuwa walimu na wainjilisti ambao walitembelea kisiwa cha Mangaia (katika Visiwavya kusini vya Cook) mnamo Juni 15, 1824. Kwa nini walitumia jina Yehova? Je, ni wao tu waliolitumia jina hilo? Majibu ya maswali hayo yanaonyesha kwa nini jina la Yehova ni muhimu sana kwa watu wengi katika visiwa vya Pasifiki.

Jina la Mungu Lilitumiwa Sana

Mishonari wengi waliowasili Pasifiki kutoka Uingereza na Marekani katika karne ya 19 walitumia jina Yehova katika mazungumzo ya kila siku na katika maandishi yao. Kwa kweli, mwanahistoria mmoja hata alifikiria kimakosa kwamba mishonari hao wa mapema “walikuwa wafuasi wa Yehova badala ya kuwa wanafunzi wa Kristo.”

Mara nyingi, mishonari hao walianza barua zao kwa maneno kama haya: “Na uokolewe na Mungu, naam, Bwana Wetu Yehova na Yesu Kristo mfalme wa amani.” Basi, haishangazi kwamba mtaalamu maarufu wa lugha Albert J. Schütz anasema kwamba kitabu kimoja sahili cha Fiji kilichochapishwa mwaka wa 1825 kilikuwa na neno moja tu lililotokana na Kiingereza. Neno hilo ni Jehova.

Wakazi wa visiwa vya Pasifiki walivutiwa sana walipowasikia mishonari wa awali wakitumia jina Yehova. Baadhi ya wakazi hao waliofundishwa walitumwa wakiwa mishonari, au walimu, ili kueneza ujumbe wao katika visiwa vingine. Kitabu The Covenant Makers−Islander Missionaries in the Pacific kinatoa maelezo haya juu ya kisa kilichotajwa juu kuhusu wale mishonari wawili Watahiti waliowasili katika kisiwa cha Mangaia: “Walimu Watahiti walijua Yehova ndiye Mungu wa kweli. Aliumba ulimwengu mzima na wanadamu pia. . . . Pia [walidai] kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli na Mwanawe Yesu Kristo ndiye Mwokozi wa wanadamu.”

Baadhi ya mishonari wa mapema walikabili hatari nyingi sana walipokuwa wakieneza ujumbe wa Biblia katika visiwa vingine kwa kuwa nyakati nyingine wakazi wa visiwa hivyo walikuwa wajeuri. Kitabu Mission, Church, and Sect in Oceania chasema hivi kuhusu magumu waliyopata: “Imani yenye nguvu katika Yehova iliwasaidia mara nyingi kushinda hofu na kutokata tamaa.”

Mfano mmoja mzuri kuhusu imani ya aina hiyo ulionekana mwaka wa 1823 wakati ujumbe wa Biblia ulipohubiriwa kwa mara ya kwanza huko Rarotonga, kimojawapo cha Visiwa vya Cook. Mishonari John Williams, aliyekuwa baharia, aliwasili huko na kutuma familia mbili kisiwani kuwafunza Wararotonga. Hata hivyo, mishonari hao walipigwa vibaya baada ya kukosana na mfalme aliyekuwa amelewa kupindukia. Mali zao zote ziliibwa, na wakaponea chupuchupu.

Waliporudi melini, mishonari hao walisema kwamba Wararotonga ni washenzi wakatili kupita wote. Akiogopa kushambuliwa, Williams aliamua kutoka katika kisiwa hicho angalau kwa muda fulani. Kisha Papeiha, mwalimu kijana, alijitolea kuhubiri katika kisiwa hicho akiwa peke yake. Alisema: “Washenzi hao waniue wasiniue, nitaenda kuwahubiria.”

Papeiha amenukuliwa mara nyingi katika matukio ya mishonari wa mapema, akieleza hivi: “Ko Jehova toku tiaki! Tei roto au i tona rima! (Yehova ni mchungaji wangu! Nimo mkononi Mwake!)” Kisha, akiwa amevalia mavazi mepesi na akiwa na kitabu chenye maandiko kadhaa ya Biblia ya Kitahiti, akaruka majini akaogelea hadi ufuoni. Badala ya kufa alitimiza mengi. Alipofika kisiwani, wengi walipendezwa na mafundisho yake.

Baadaye Mrarotonga mmoja anayeitwa More Ta’unga akawa mishonari. Mnamo mwaka wa 1842, akawa mishonari wa kwanza kuanzisha kituo cha mishonari kwenye kisiwa cha New Caledonia. Katika kitabu chake cha kumbukumbu, aliandika hivi kumhusu mwenyeji mmoja ambaye alimfunza kusoma na kuandika: “Alijifunza polepole. Punde si punde akaniambia, ‘Nataka kusali.’ Lakini nikamshauri asiwe na haraka. Baadaye akaniuliza hivi, ‘Hutaniruhusu nisali?’ Kisha akaniuliza kwa nini sikumruhusu asali na nikamwambia hivi, ‘Lazima utupilie mbali sanamu zako kwanza, halafu unaweza kusali kwa Yehova. Ni yeye tu anayeweza kukusikia.’ Basi akaniletea kikapu chake chenye miungu, akisema, ‘Ichome. Sasa Yehova atakuwa Mungu wangu.’ Akajua kusali vizuri.”

Wakazi wa Pasifiki Wamkubali Yehova

Kwa kuwa mishonari walitumia jina la Mungu mara nyingi, haishangazi kwamba wale waliowahubiria walimkubali Yehova kuwa Mungu wao. Kitabu Missionary Adventures in the South Pacific chaelezea mkutano mkubwa uliofanywa katika kimojawapo cha visiwa vya Pasifiki kaskazini baada ya kuwasili kwa meli ya mishonari ya Morning Star. Kitabu hicho kinasema kwamba wakazi wa kisiwa hicho “waliinua mikono yao, huku wengi wakiinua mikono yote miwili kwa muda mrefu kuonyesha kwamba wangeacha kuabudu sanamu na kuanza kumwabudu Yehova. Isitoshe, walikubali kuwatunza walimu hao. Uwanja ulitengwa na kuwekwa wakfu kwa Yehova ili kujenga kanisa na nyumba ya kasisi.”

Kitabu Wiliamu—Mariner-Missionary—The Story of John Williams chaeleza hivi kuhusu kugeuzwa imani kwa Malietoa, chifu mkuu wa Samoa: “Malietoa aliwahutubia watu wake kwa muda mrefu na akawaahidi waziwazi kwamba atamwabudu Yehova na kujenga kanisa kwa ajili ya ibada Yake. Aliwaamuru watu waliobaki nyumbani waanze kujifunza kumhusu Yehova na Yesu Kristo.”

Jitihada hizo zote zilibadili maisha ya wakazi wengi wa Visiwa vya Pasifiki. Hata leo ni jambo la kawaida kusikia jina la Yehova likitajwa kwenye redio au kwenye magazeti katika nchi za Fiji na Samoa.

Lakini jina la Mungu lilikuwa na matokeo zaidi. Pearl Binder alieleza umuhimu wa jina la Yehova kwa Wabanaba katika kitabu chake Treasure Islands kilichochapishwa kwa mara ya kwanza mwaka wa 1977. Wabanaba waliishi Kiribati hapo awali na baadaye walihamishiwa kwenye kisiwa cha Rabi, huku Fiji. Binder anaandika hivi: “Mishonari waliokuja Banaba waliwapa Wabanaba kitu chenye thamani sana. . . . Imani yao katika Yehova imekuwa jambo kuu maishani mwao, imewaunganisha kuliko kitu kingine chochote katika miaka sabini yenye matatizo au magumu mengi yenye kufadhaisha na hata leo imani hiyo inawaimarisha kiroho. Kama wazungu hawangewafundisha Wabanaba kumhusu Yehova (ambaye wazungu wenyewe wamempuuza zaidi) Wabanaba wangekosa mwongozo.”

Jina la Mungu Katika Tafsiri za Biblia

Mishonari wa mapema walikusudia hasa kutafsiri Biblia katika lugha inayoeleweka ya wakazi wa Visiwa vya Pasifiki. Kutokana na jitihada zao nyingi, Biblia ilitafsiriwa katika lugha nyingi zinazozungumzwa kotekote katika eneo la Pasifiki. Watafsiri hao waliona kwamba inafaa kutohoa jina la Yehova kama walivyotohoa majina mengine yote katika Biblia.

Wanafunzi makini wa Biblia hupendezwa kuona kwamba watafsiri hao wa mapema walitumia jina la Yehova katika tafsiri zao za Maandiko ya Kiebrania na vilevile Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ambayo kwa kawaida huitwa Agano Jipya. Uchunguzi wa lugha saba za Visiwa vya Pasifiki unaonyesha kwamba jina la Yehova limetumiwa katika mistari 72 ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Baadhi ya tafsiri hizo si za karne ya 19. Tafsiri hizo zinatia ndani pia tafsiri ya kisasa ya Kirotuma iliyotolewa mwaka wa 1999. Biblia hiyo ina jina la Yehova katika mistari 48 ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

Mwishoni mwa karne ya 19, mishonari wa muda mrefu katika Visiwa vya Pasifiki, William Wyatt Gill, aliandika hivi kuhusu mojawapo ya tafsiri za mapema: “Kwa kuwa nimetumia Biblia ya Kirarotonga kwa muda wa miaka arobaini na miwili, sikosei ninaposema kwamba hiyo ni tafsiri mwafaka ya maandiko ya awali. . . . Kama ilivyo na tafsiri nyingine zote za Pasifiki na New Guinea, jina takatifu ‘Yehova’ limetoholewa, halijatafsiriwa, na hivyo kuonyesha wazi tofauti kati ya Mungu aishiye milele na vitu vinavyoabudiwa na makafiri.”

Kwa Nini Walitumia Jina la Mungu?

Kwa nini mishonari hao, watafsiri wa Biblia, na walimu walitumia sana jina la Mungu, Yehova? Hasa kwa sababu waliona inafaa kumtofautisha Yehova, Mungu wa pekee wa kweli, na miungu mingi ya uwongo iliyoabudiwa na wakazi wa visiwa vya Pasifiki. (Yohana 17:3; 1 Wakorintho 8:5, 6) Miungu yote hiyo ilikuwa na majina, kwa hiyo haishangazi kwamba watu walioiabudu waliuliza hivi, “Mungu wenu ni nani? Anaitwa nani?” Kutumia jina “mungu” kungewatatanisha watu hao au labda wangefikiri kwamba Mweza-Yote ni mungu tu kama miungu mingi waliyokuwa nayo. Hivyo, si ajabu kwamba mishonari hao wa mapema walitumia sana jina la Yehova.

Je, hiyo inamaanisha kwamba wale wote wanaotumia jina Yehova wanamjua kikweli? La. Hiram Bingham, mishonari mtafsiri aliyekuwa mwana wa yule mishonari maarufu wa Hawaii mwenye jina hilo, aliwahubiria wakazi wa Abaiang (huko Kiribati) na wakapaaza sauti, “kuna Mungu mmoja tu—Yehova” huku wakiharibu sanamu yao. Lakini kitabu Missionary Adventures in the South Pacific kinasema hivi kuhusu tukio hilo:

“Lakini, Bingham alijua kwamba kuharibu sanamu hiyo hakukumaanisha kwamba watu hao walikubali Ukristo kikweli. Hawakuwa wameelewa kabisa injili, lakini walikuwa wameanza.” Ni wazi kwamba haitoshi tu kujua jina Yehova. Wakristo wa kweli wanahitaji kumjua Yehova kibinafsi na kumtii katika kila jambo.—Waroma 10:13-17.

Hata Musa mwaminifu, aliyejua jina la Yehova na kulitumia, alihitaji kujua mengi zaidi. Alisali hivi: “Basi, sasa nakuomba, ikiwa nimepata neema mbele zako, unionyeshe njia zako, nipate kukujua, ili nipate neema mbele zako.” (Kutoka 33:13) Naam, Musa hakutosheka tu kujua jina la Yehova. Alitaka kujua sifa za Yehova na jinsi ya kumpendeza. Mungu alijibu ombi la Musa kwa kumpa pendeleo la pekee la kuona tukio lililoonyesha maana ya jina la Yehova.—Kutoka 33:19; 34:5-7.

Vivyo hivyo leo, maelfu ya Mashahidi wa Yehova kotekote katika eneo la Pasifiki wanatumia Biblia ambazo mwanzoni zilitafsiriwa na mishonari wa mapema ili kuwasaidia watu wanyoofu waelewe maana ya jina la Yehova na matakwa yake ya kumwabudu “kwa roho na kweli.” (Yohana 4:23, 24) Naam, jina la Yehova linatukuzwa katika “visiwa vya bahari.” Kwa hiyo, maelfu ya watu wanalitumaini jina hilo tukufu.—Isaya 24:15; 42:12; 51:5; Mithali 18:10.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Wakazi wa Pasifiki waliofundishwa jina la Mungu na mishonari wa mapema wa Jumuiya ya Wakristo, waliwajulisha wengine jina hilo

[Hisani]

Palm tree and photo at left: From the book Gems From the Coral Islands

[Picha katika ukurasa wa 13]

John Williams

[Hisani]

Culver Pictures

[Picha katika ukurasa wa 13]

Papeiha

[Hisani]

Courtesy Institute of Pacific Studies, from Mission Life in the Islands of the Pacific, by Aaron Buzacott

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mashahidi wa Yehova hujulisha jina la Mungu ulimwenguni pote