Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Malezi Yangu Yalinisaidia Niishi Maisha Yenye Kusudi

Malezi Yangu Yalinisaidia Niishi Maisha Yenye Kusudi

Malezi Yangu Yalinisaidia Niishi Maisha Yenye Kusudi

SIMULIZI LA ERNEST PANDACHUK

Nilizaliwa karibu na mbuga za Saskatchewan, nchini Kanada. Nilipokuwa na umri wa miaka 23, nilihamia Afrika, ambako kwa miaka 35 nilifurahia maisha ya umishonari. Nilipataje kuishi maisha yenye kuridhisha jinsi hiyo? Haikutukia tu kimuujiza. Acha nieleze.

MWANZONI tuliishi katika nyumba iliyotengenezwa kwa miti, udongo, na nyasi ambayo haikutukinga kutokana na majira ya baridi kali sana mbugani. Mnamo mwaka wa 1928, kabla ya wengi katika familia yetu ya watoto tisa kuzaliwa, Baba na Mama walikubali vitabu vya Biblia kutoka kwa mtu fulani aliyetutembelea nyumbani. Katika kipindi kirefu cha majira ya baridi kali, walijifunza Biblia wakitumia vitabu hivyo. Kufikia majira ya kuchipua, walikuwa wamesadiki kwamba wamepata kweli. Waliwahubiria marafiki, majirani, na watu wa familia, lakini hasa watoto wao.

Nilizaliwa mwaka wa 1931, na ndugu zangu watano wadogo walizaliwa punde baadaye. Familia yetu ilisoma na kujifunza Biblia kwa ukawaida. Nakumbuka vizuri mambo tuliyofanya kila siku asubuhi. Baba aliongoza mazungumzo ya andiko la Biblia, hata tulipokuwa na wageni. Mama na Baba, na vilevile wakubwa wangu, walisoma vitabu vya Biblia kwa sauti.

Licha ya kutufundisha kusoma na kuandika, Baba alitufundisha pia kufanya utafiti kwa kutumia faharisi za Biblia. Muda si muda, tulijifunza jinsi ya kuwaeleza wengine kuhusu imani yetu kwa kutumia Biblia. Mazungumzo hayo yenye kufurahisha yaliniwezesha kuwafundisha wengine Biblia. Baada ya muda, nilijua kutumia Biblia kupinga mafundisho ya uwongo ya kidini. Ningeweza kuthibitisha kwamba nafsi hufa, kwamba hakuna moto wa mateso, na kwamba Mungu na Yesu hawalingani wala si sehemu ya ule uitwao Utatu.—Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4; Yohana 14:28.

Baba na Mama pia walitufundisha kwa mfano wao mzuri na walitutia moyo kutetea kweli hata kama hatungependwa na watu. Kwa mfano, hawakuvuta tumbaku, na walituonya kwamba inachafua mwili na kwamba tungeshawishiwa kuivuta shuleni. Nakumbuka maneno haya ya Baba: “Huenda ukaitwa mwanamke usipovuta tumbaku. Lakini muulize mtu huyo hivi, ‘Mwanamume ni nani? Yule anayedhibitiwa na tumbaku au yule anayedhibiti tumbaku?’”

Nilipokuwa na umri wa miaka 11, mazoezi yangu ya Kibiblia ya tangu utotoni yalijaribiwa tena. Wakati huo, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilikuwa vimeanza na wanafunzi wa shule walipaswa kukariri kiapo cha uaminifu kwa bendera. Kupitia funzo langu la Biblia, nilitambua kwamba kiapo kama hicho kilikuwa tendo la ibada, kwa hiyo sikushiriki. Hivyo, nilifukuzwa shuleni kwa miezi sita.

Hata hivyo, baadaye nilimaliza shule, na katika Machi 1947, nilionyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova Mungu nilipobatizwa katika maji. Miezi sita baadaye nikawa painia, yaani, mhubiri wa wakati wote wa habari njema. Kwanza nilitumikia kusini mwa Saskatchewan, nikiwahubiria wakulima na wafugaji katika eneo hilo kubwa. Katika majira ya kiangazi, nilisafiri kwa farasi, na wakati wa baridi kali nilitumia kigari kilichovutwa na farasi. Kilipashwa joto kwa jiko la makaa, kwa hiyo nilikuwa mwangalifu kisianguke.

Wakazi wa mashambani walikuwa wakarimu na wenye urafiki. Nilipowatembelea jioni, mara nyingi waliniomba nilale kwao. Nilifurahia sana mazungumzo yetu motomoto ya Biblia katika pindi hizo! Familia ya Petersons ni mojawapo ya familia zilizokubali kweli baada ya mazungumzo ya usiku kucha. Earl na mama yake wakawa Mashahidi wa Yehova wenye bidii.

Kutumikia Huko Quebec

Mnamo mwaka wa 1949, niliitikia mwito wa kuwa painia katika mkoa wa Quebec. Karibu mapainia 200 kutoka magharibi mwa Kanada waliitikia mwito huo. Waliwasili jijini Montreal mwezi wa Septemba, wakiwa tayari kuanza migawo katika sehemu mbalimbali za Quebec. Wakati huo, Kiongozi Mkatoliki Maurice Duplessis aliapa kuwamaliza Mashahidi katika mkoa huo.

Hizo zilikuwa nyakati za kusisimua zenye shughuli na magumu mengi. Tulihitaji kujifunza Kifaransa, tulikamatwa, tulishambuliwa na umati, na makusanyiko yetu ya Kikristo yalivurugwa na watu wenye fujo. Hata hivyo, upinzani huo haukuniogopesha wala kunifanya niache kumtumikia Mungu. Wazazi wangu walikuwa wamenifundisha kupenda kweli na kunisadikisha kwamba kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote ambayo Yesu alitabiri ingetimizwa, licha ya upinzani.—Mathayo 24:9, 14.

Nilipokuwa Quebec, nilikutana na Emily Hawrysh, painia mwaminifu kutoka Saskatchewan. Tangu tulipooana mnamo Januari 27, 1951, Emily amekuwa mfanyakazi mwenzangu aliye mwaminifu na mwandamani mwenye kutia moyo. Kwa kuwa mradi wetu ulikuwa kufanya utumishi wa wakati wote kikamili zaidi, tuliomba na tukakubaliwa kuwa wanafunzi katika Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower, ambayo huwazoeza wahudumu kwa miezi sita ili wawe mishonari. Darasa letu la 20 lilihitimu mnamo Februari 1953.

Tulipokuwa tukisubiri stakabadhi zetu za kusafiri Afrika, tuliombwa kusaidia makutaniko ya Mashahidi wa Yehova huko Alberta na Ontario, Kanada. Siku hizo tulisafiri kutoka kutaniko moja hadi jingine tukitumia usafiri wa umma. Kwa hiyo, tulijifunza kuishi maisha sahili huku tukibeba vitu vyetu vyote katika sanduku moja. Miezi michache baadaye, wakati stakabadhi zetu zilipokuwa tayari, tulianza safari yetu kuelekea Rhodesia Kusini, ambayo leo huitwa Zimbabwe.

Kuzoea Maisha ya Afrika

Katika miezi yetu mitano ya kwanza, tulipewa mgawo wa kutembelea makundi ya Mashahidi wa Yehova nchini Zimbabwe na vilevile Botswana na sehemu za kusini za Rhodesia Kaskazini (leo ni Zambia). Tulipokuwa katika Shule ya Gileadi, tulifundishwa tusilinganishe mgawo wetu wa kigeni na hali za nchi ya kwetu na kukumbuka kwamba katika hali yoyote ile tungeweza kujifunza jambo fulani. Mafundisho hayo ya hekima yalitusaidia kubadilisha maoni yetu. Hadi leo, mimi na Emily tunakubaliana na msemo huu, “Tumia ifaavyo kila fursa; huenda usiipate tena.”

Tulisafiri kila mahali kwa gari la moshi, basi, lori, au baiskeli—kwa njia yoyote ile. Ijapokuwa njia hizo za usafiri zilichosha sana, kulikuwa na mambo mengine yaliyojaribu azimio letu la ‘kutumia ifaavyo kila fursa.’ Kwa miaka miwili ya kwanza, Emily alikatazwa kuandamana nami kwenye maeneo ya makabila kwa sababu ya vizuizi vya kisheria. Hivyo, mke wangu niliyekuwa nimeishi naye kwa miaka michache alibaki kwenye miji iliyokuwa karibu na kituo cha gari la moshi, ambako mara nyingi hakukuwa na Mashahidi wengine. Imani, ujasiri, na azimio la Emily lilinifanya nimpende zaidi na kuvutiwa naye na pia lilizalisha matunda ya Ufalme katika jamii hizo.

Punde tu alipoanza kuishi na mkazi mmoja wa eneo hilo, Emily alihubiri katika eneo hilo hadi niliporudi. Nyakati nyingine, alihubiri peke yake kwa mwezi mmoja. Aliimarishwa na kulindwa kwa kutegemea mkono wa Yehova wenye nguvu, na huduma yake ikawa na matokeo. Kwa mfano, Rita Hancock alikubali kweli ya Biblia na baadaye mumewe akajiunga naye. Akawa ndugu mwaminifu na akatumikia akiwa mzee Mkristo hadi kifo chake. Leo kuna makutaniko makubwa katika baadhi ya miji ambako Emily alipanda mbegu za kweli ya Biblia.

Ukarimu na Maarifa ya Waafrika

Nilipokuwa katika maeneo ya makabila, nilivutiwa sana kuona jinsi Mashahidi Waafrika wanavyothamini sana tengenezo la Yehova na wawakilishi wake wanaosafiri. Ndugu hao Wakristo wenye upendo walinitunza vizuri. Kila Jumatatu nilisafiri kutoka kusanyiko moja hadi jingine. Nililala katika nyumba mpya ya nyasi, na hilo lilinikumbusha nyumba ya familia yetu huko Saskatchewan. Nililala kwenye mkeka wa nyasi wenye unene wa sentimeta 30 uliotandazwa sakafuni na kufunikwa kwa shuka.

Kwa kawaida makusanyiko katika maeneo ya makabila yalifanywa msituni. Wahudhuriaji walifyeka vichaka, na kuacha miti yenye majani mengi kwa ajili ya kivuli. Matita ya nyasi yalifungwa na kupangwa vizuri katika safu ili yakaliwe. Hatimaye, ua wa nyasi ulijengwa kuzunguka uwanja huo. Sikuzote nilivutiwa na sauti tamu za ndugu na dada zetu Waafrika waliomwimbia Yehova sifa kwa upatano wa hali ya juu katika mazingira hayo ya kiasili.

Tukio Nisiloweza Kusahau

Nilipokuwa nikihubiri, nilikutana na Gideon Zenda, mkaguzi mkuu wa shule zilizoendeshwa na Kanisa la Anglikana. Gideon alisomeshwa na kanisa hilo hadi chuo kikuu. Hata hivyo, maswali yake mengi ya Biblia hayakujibiwa kikamili. Kwa hiyo, aliniomba nikutane naye pamoja na marafiki zake ili nijibu maswali hayo. Nilipomtembelea, nilikuta watu wapatao 50 wakiningojea, wakiwemo wakaguzi wa shule, walimu wakuu, na walimu wengine. Gideon alikuwa mwenyekiti wa mkutano huo. Tulizungumzia vichwa mbalimbali hatua kwa hatua. Nilizungumzia kila kichwa kwa dakika 15 kisha nikawaruhusu waulize maswali. Mkutano huo ulichukua saa kadhaa.

Kutokana na mazungumzo hayo, Gideon, familia yake, na idadi kubwa ya wafanyakazi wenzake wakawa watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu na kubatizwa. Askofu wa eneo hilo aliwafuta kazi walimu hao wa shule zilizoendeshwa na Kanisa la Anglikana. Hata hivyo, wote hawakuogopa na hawakuacha kumtumikia Yehova, na baadhi yao walifanya upainia.

Filamu Yavutia Wengi

Mnamo mwaka wa 1954, Mashahidi wa Yehova walitoa filamu yenye kichwa The New World Society in Action. Mwaka uliofuata, sheria zilizomzuia mke kuandamana na mume katika maeneo ya makabila zilifutiliwa mbali. Hivyo, Emily angesafiri pamoja nami katika maeneo hayo. Wakati huo tulipewa gari, jenereta, na projekta ili kuonyesha filamu hiyo katika maeneo yote ya makabila. Filamu yetu ilivutia halaiki ya watu kwani wengi hawakuwa wameona filamu. Filamu hiyo ilionyesha utaratibu wa kuchapisha vitabu na Biblia katika matbaa yetu kubwa huko Brooklyn, New York.

Filamu hiyo pia ilionyesha Mashahidi wa Yehova kutoka ulimwenguni pote wakiabudu pamoja katika Uwanja wa Yankee huko New York, mwaka wa 1953. Ilikuwa mara ya kwanza kwa Waafrika hao kuona watu kutoka makabila mbalimbali wakiwa na umoja na upendo. Filamu hiyo ilichochea familia nyingi nchini Zimbabwe zianze kujifunza Biblia na kushirikiana na Mashahidi. Tulipokea maombi mengi ya kuonyesha filamu kutoka kwa walimu wakuu kotekote nchini ambao walijua umuhimu wa kuwaelimisha wanafunzi kupitia filamu.

Usiku mmoja niliamshwa na Mashahidi waliotaka nionyeshe filamu hiyo. Nilishangaa kuwakuta watu 500 hivi ambao walikuwa wametembea kwa saa kadhaa ili kuja kuiona. Walikuwa wamesikia kwamba nilikuwa nikionyesha filamu hiyo katika eneo hilo. Kikundi kingine cha watu 300 kiliwasili kabla tu ya kikundi cha kwanza kuondoka. Kwa hiyo niliwaonyesha filamu hiyo tena. Kikundi cha mwisho kiliondoka saa tisa usiku! Watu zaidi ya milioni moja walitazama filamu hiyo yenye kusisimua katika kipindi cha zaidi ya miaka 17 nchini Zambia pekee!

Migawo Mipya Huko Afrika

Baada ya kutumikia kwa zaidi ya miaka mitano na nusu nchini Zimbabwe, tulihamishwa hadi Afrika Kusini. Kwa hiyo tulihitaji kujifunza Kiafrikana. Baadaye tulijifunza pia Kisesotho na Kizulu. Kufundisha Neno la Mungu kwa kutumia lugha hizo kulitusaidia kuwa na matokeo katika utumishi na tuliridhika sana.

Mapema katika miaka ya 1960, tulipewa mgawo wa kutembelea makutaniko katika eneo la kusini mwa Afrika. Kwa miaka 27 iliyofuata, tulitembea katika maeneo mengi ya Afrika Kusini, Lesotho, Namibia, na Swaziland na vilevile katika visiwa vya Ascension na St. Helena kwenye Bahari ya Atlantiki Kusini. Tulisafiri mamia ya maelfu ya kilometa kuwatumikia ndugu na dada zetu Wakristo. Imani na uaminifu wao wajapokabili hali ngumu, imetutia moyo tusichoke.

Kwa mfano, niliwafahamu Mashahidi wa Swaziland ambao hawakuvunja imani yao wakati Mfalme Sobhuza wa Pili alipokufa. Walifutwa kazi na kunyimwa haki zao wakiwa raia kwa kuwa walikataa kushiriki desturi zisizo za Kimaandiko zinazofanywa wakati wa kifo cha mheshimiwa kama huyo. Licha ya kukabiliana na umaskini na magumu kwa miaka mingi, hawakuacha imani yao. Daima nitamshukuru Yehova kwa sababu ya fursa ya kuwajua ndugu na dada hao Wakristo wa pekee na hata kuzungumza nao ana kwa ana.

Pia kuna painia anayeitwa Philemon Mafareka kutoka kijiji cha Mokhotlong, Lesotho, kilicho kwenye milima yenye urefu wa meta zaidi ya 3,000. Kwa kuwa hakukuwa na usafiri, yeye na mke wake mpendwa, watoto wao wawili, na wanafunzi wanne waliotarajia kubatizwa walitembea umbali wa kilometa 100 ili kuhudhuria kusanyiko lililofanywa kwenye eneo lenye mwinuko wa meta 1,000. Walihitaji kushuka miteremko mikali katika safari yao. Walipanda na kushuka mabonde na milima kwa mikono na kuvuka vijito na mito mingi.

Wakati wa kurudi nyumbani baada ya kusanyiko, walibeba nakala mia moja za kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele ili kuwapelekea watu wa Mokhotlong. Hata hivyo, walikutana njiani na watu wengi waliopendezwa na vitabu hivyo vya Biblia, kwa hiyo vilikwisha kabla hawajafika nyumbani. Mimi na Emily tumepata pendeleo kubwa la kuona bidii na ujitoaji wa ndugu na dada Wakristo kama Philemon na mke wake, na tunathamini pendeleo hilo hadi leo.

Nyakati nyingine, tulikabili hatari ya nyoka wenye sumu, kama vile swila, mafuriko ya ghafula na hatari nyinginezo. Mambo hayo yalituogopesha wakati huo, lakini hayawezi kulinganishwa na thawabu na shangwe za kumtumikia Yehova wakati wote. Tulijifunza kwamba Yehova hawaachi kamwe waaminifu wake.

Wakati Emily alipopata matatizo makubwa ya afya, Yehova alitupa hekima ya kuyashughulikia kwa njia ifaayo. Ili apone haraka ilimbidi kula vyakula vya aina fulani na kuzingatia usafi. Tulitengeneza gari la kulala ili Emily aishi katika hali nzuri wakati tuliposafiri, na baada ya muda akawa na afya nzuri.

Kurudi Kanada

Mnamo mwaka wa 1988, baada ya kufanya umishonari kwa miaka 35 katika bara la Afrika lenye kuvutia, tulipewa mgawo wa kurudi Kanada. Kisha, mnamo mwaka wa 1991, nilianza tena kuwa mwangalizi asafiriye. Miaka minane baadaye nilipata kiharusi. Ingawa utumishi wangu umeathiriwa sana tangu wakati huo, bado ninafurahia kutumikia nikiwa mzee katika kutaniko moja huku London, Ontario.

Nafurahi sana ninapokumbuka miaka 56 hivi iliyopita nilipoanza upainia nikitumia farasi kusini mwa Saskatchewan. Ninashukuru sana kwamba Baba alitufundisha daima kuwa watu wa kiroho na kutoogopa kamwe kutetea kweli na uadilifu! Alinifundisha Neno la Mungu, na hilo lilinisaidia niishi maisha yenye kusudi. Urithi huo umenifaidi siku zote. Siwezi kuacha utumishi wa Yehova kwa sababu ya kitu chochote cha ulimwengu huu unaopitilia mbali.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Familia yetu ya watoto tisa mnamo mwaka wa 1949, Mama amembeba kitinda-mimba. Nimesimama nyuma yake

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nilitengeneza kigari hiki kwa ajili ya utumishi

[Picha katika ukurasa wa 20]

Wanawake huko Quebec waliokamatwa kwa sababu ya kuhubiri

[Picha katika ukurasa wa 22, 23]

Nilishiriki kuwafundisha waangalizi hawa wasafirio nchini Zimbabwe

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tulitengeneza gari hili la kulala ili Emily apone

[Picha katika ukurasa wa 23]

Picha ya karibuni nikiwa na Emily