Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nawezaje Kutambuliwa Bila Kuwategemea Wazazi?

Nawezaje Kutambuliwa Bila Kuwategemea Wazazi?

Vijana Huuliza . . .

Nawezaje Kutambuliwa Bila Kuwategemea Wazazi?

“Babangu ni mzee anayejulikana sana katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova. Namheshimu, lakini nyakati nyingine mimi huudhika kwa sababu kila mahali ninapoenda mimi huitwa tu mtoto wa ndugu Bill.”—Larry. *

“Kwa kuwa babangu ni mzee maarufu, niliona kwamba kila mtu alinitarajia nifanye mengi, na ilikuwa vigumu sana kuishi maisha ya kawaida.”—Alexander.

ADIRI unavyokua ndivyo unavyotamani kujitegemea, kujijengea jina au sifa. Ulipozaliwa, wazazi wako walikupa jina lililowapendeza. Sasa kwa kuwa unabalehe, unataka kujijengea “jina,” yaani kujifanyia sifa.

Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi; na neema kuliko fedha na dhahabu.” (Mithali 22:1) Hata ukiwa bado kijana, huenda ukataka kujifanyia sifa.

Kutambuliwa kwa Sababu ya Wazazi

Kama Larry na Alexander, vijana fulani huona kwamba wanatambuliwa kwa sababu ya sifa au mafanikio ya wazazi wao. Labda wazazi wao ni maarufu katika jamii kwa sababu ya kazi yao au elimu. Au huenda ikawa wanajulikana sana katika kutaniko la Kikristo. Ikiwa wazazi wako ni maarufu, huenda nyakati nyingine ukaona kwamba unachunguzwa nyakati zote. Huenda ukajilazimisha kutenda kwa njia fulani kwa sababu tu ya sifa za wazazi wako.

Kwa mfano, baba ya Ivan ni mzee katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova. Ivan anasema hivi: “Kwa kuwa wengi walimjua na kumheshimu babangu, sikuzote niliona kwamba ninapaswa kuwa mfano mzuri shuleni na nyumbani. Nilihisi kwamba wazazi wengine walitaka watoto wao waniige. Ijapokuwa hilo lilinifurahisha, ilinibidi niwe mfano mzuri kwa wengine. Kwa hiyo, nyakati nyingine sikuwa mwenye kiasi na sikutambua udhaifu wangu.” Alexander anasema: “Nilihisi kwamba nilikuwa nikitazamwa kila wakati na ikiwa ningekosea watu wangekuwa tayari kunishutumu.”

Larry, aliyenukuliwa mwanzoni, alijaribu kuepuka kukaziwa fikira na wengine kwa kuficha jina la familia yao. Anasema: “Nilipokutana na watu nisiowajua kwenye tafrija, niliwasalimu hivi, ‘Vipi, naitwa Larry,’ kisha nilikomea hapo bila kutaja jina la familia. Nyakati nyingine nilipojaza fomu, niliandika tu jina langu la kwanza. Niliogopa watu wangenitendea tofauti ikiwa wangemjua babangu. Nilitaka marafiki zangu wanitendee kama kawaida.”

Bila shaka, ni kawaida kwa wengine kutazamia utimize mengi ikiwa baba yako ni mzee Mkristo au mtumishi wa huduma. Kwa kweli, wanaume waliowekwa rasmi wanapaswa wawe “wakisimamia watoto na watu wa nyumbani mwao wenyewe kwa njia bora.” (1 Timotheo 3:5, 12) Basi, si ajabu kwamba watu wanatarajia uwe mfano bora! Lakini, je, hilo ni jambo baya? Hakuna ubaya wowote unapozingatia kwamba kijana Mkristo Timotheo huenda hakuwa amefikisha umri wa miaka 20 alipochaguliwa na Paulo kusafiri pamoja naye, na kufanya kazi muhimu katika huduma. (1 Wathesalonike 3:1-3) Hivyo, unapaswa kujitahidi kuwa mfano bora, iwe baba yako ni mzee katika kutaniko au la.

Si Hekima Kuasi

Vijana wengine hujaribu kuepuka sifa nzuri za wazazi wao kwa kuasi. Ivan anasema hivi: “Nyakati nyingine niliudhika watu walipotarajia niwe mfano bora. Niliasi kwa kufuga nywele ndefu ili nione ikiwa mtu yeyote atanishauri.”

Absalomu, mwana wa Mfalme Daudi aliamua kuasi. Baba yake alijulikana sana kwa sababu ya kujitoa kwa Yehova, naye alipendwa na wengi katika taifa la Israeli. Absalomu alitarajiwa afanye mengi akiwa mwana wa Daudi. Lakini badala ya kutenda ipasavyo, Absalomu aliamua kujijengea jina kwa kumwasi baba yake. Kwa kuwa Daudi alikuwa mwakilishi wa Yehova aliyetiwa mafuta, Absalomu alikuwa akimwasi Yehova. Matendo yake yaliiaibisha familia yao na kumletea msiba.—2 Samweli 15:1-15; 16:20-22; 18:9-15.

Vivyo hivyo, uasi unaweza kukuletea msiba. Fikiria yale ambayo Biblia inasema kumhusu Nehemia. Maadui fulani walijaribu kutunga hila ili amwasi Yehova. Kwa nini? Nehemia alisema: “Kwa njia hii wangepata mwanya wa kuniharibia jina langu ili kushusha hadhi yangu.” (Nehemia 6:13, Biblia Habari Njema) Ukiasi utajiharibia jina, na watu hawatasahau.

Ni muhimu pia kufikiria jinsi uasi unavyoweza kuwaathiri wengine. Kwanza, utawahuzunisha wazazi wako bure. (Mithali 10:1) Matendo yako yanaweza pia kuwaathiri sana vijana wengine. Ivan anasema: “Tabia yangu ilimwathiri sana ndugu yangu. Kwa muda fulani alijitenga kabisa na kutaniko la Kikristo na akaanza kufanya mambo ambayo alijua hayapatani na kanuni za Biblia. Hata hivyo, baadaye alijuta na sasa anafurahia kumtumikia Yehova tena.”

Njia Bora

Sulemani, aliyekuwa ndugu nusu ya Absalomu, hakutenda kama Absalomu. Alikuwa na nia ya kuiga kwa unyenyekevu mfano wa Daudi baba yake. (1 Wafalme 2:1-4) Badala ya kujitukuza, Sulemani aliazimia kujenga jina zuri mbele za Mungu. Kadiri alivyofanya hivyo, aliiletea familia yao heshima, naye akajulikana kuwa mmoja wa wafalme wakuu wa Israeli.—1 Wafalme 3:4-14.

Mfano bora wa Sulemani unatufundisha mambo mawili muhimu: Kwanza, mtu hujijengea jina kwa kuiga sifa nzuri za familia yao, badala ya kujitenga nayo. Jarida Adolescence linasema hivi: “Wakati wa kubalehe si wakati wa kijana kujitenga na wazazi wake ili ajijengee jina.” Jarida hilo linaendelea kusema kwamba “msaada wa wazazi wako haukuzuii” kujijengea jina “bali unakusaidia kufanya hivyo.”

Inafaa kabisa kwamba Sulemani mwenyewe aliandika hivi: “Msikilize baba yako aliyekuzaa, wala usimdharau mama yako akiwa mzee.” (Mithali 23:22) Inaonekana Sulemani hakuwa akiwaandikia watoto wadogo maneno hayo, kwa sababu wazazi ‘wakiwa wazee,’ mara nyingi mtoto huwa mtu mzima. Tunajifunza nini? Hata ukiwa mtu mzima na uwe na familia, bado unaweza kufaidika kutokana na hekima ya wazazi wako. Ivan alitambua jambo hilo baadaye. Anasema: “Kadiri ninavyozeeka, ninajaribu kuiga sifa nzuri za wazazi wangu na kuepuka makosa yao.”

Jambo la pili tunalopaswa kuzingatia ni kwamba jambo kuu maishani mwa Sulemani halikuwa kujijengea jina bali kumpendeza Yehova. Ni kweli kwamba alitarajiwa atimize mengi akiwa mwana wa Daudi. Lakini Sulemani alitekeleza madaraka yake kwa sababu alimtegemea Yehova. Sasa Alexander ana mtazamo kama huo. Anasema hivi: “Sasa nimejua kwamba watoto wa wazee hutazamiwa watimize mengi. Niliamua kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu jambo hilo, na umenilinda. Ninatambua kwamba jambo la maana zaidi ni jinsi Yehova anavyoniona. Ananijua mimi binafsi wala haangalii tu mimi ni mtoto wa nani.”

Baba ya Daryn alihitimu Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower * inayowazoeza mishonari. Daryn amejua jinsi ya kuishi akiwa na wazazi wanaojulikana sana. Anasema hivi: “Nilipobatizwa nilijiweka wakfu kwa Yehova na si kwa mwanadamu yeyote. Ninapojitahidi niwezavyo kuishi kupatana na wakfu wangu, ninapata amani ya moyoni kwa sababu ninajua kwamba Yehova anapendezwa nami, hata ingawa siwezi kufanya mambo yote ambayo wazazi wangu walifanya.”

Mfalme Sulemani alisema hivi: “Hata mtoto hujijulisha kwa matendo yake; kwamba kazi yake ni safi, kwamba ni adili.” (Mithali 20:11) Lolote liwalo, watu watakukumbuka kwa sababu ya maneno na matendo yako wala si kwa sababu ya wazazi wako. Uwe mfano mzuri “katika kusema, katika mwenendo, katika upendo, katika imani, katika usafi wa kiadili.” Ukifanya hivyo, watu watakupenda na kukuheshimu kwa sababu ya sifa zako!—1 Timotheo 4:12.

Mbali na hayo, vijana wengine hutamani watambuliwe bila kuwategemea ndugu au dada zao wenye mafanikio mengi. Makala nyingine wakati ujao itazungumzia jinsi unavyoweza kushughulikia hali hiyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 22 Shule ya Gileadi huendeshwa na kusimamiwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 26]

Ukiasi, utawahuzunisha wazazi wako na kujiharibia jina

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mfano wako mzuri unaweza kuwafaidi wengine