Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ufanye Nini Iwapo Watu wa Ukoo Si wa Dini Yako?

Ufanye Nini Iwapo Watu wa Ukoo Si wa Dini Yako?

Maoni ya Biblia

Ufanye Nini Iwapo Watu wa Ukoo Si wa Dini Yako?

INAKADIRIWA kwamba kuna zaidi ya dini na madhehebu 10,000 ulimwenguni. Katika nchi moja, asilimia 16 hivi ya watu wazima wamewahi kubadili dini. Basi si ajabu kwamba watu wa ukoo na marafiki wana mafundisho ya kidini yanayotofautiana. Nyakati nyingine hilo huharibu mahusiano. Hivyo swali hili linazuka, Wakristo wanapaswa kuwatendeaje watu wa ukoo ambao si wa dini yao?

Uhusiano wa Pekee

Kwa mfano, fikiria yale ambayo Biblia inasema kuhusu uhusiano wa pekee kati ya wazazi na watoto wao. Amri inayopatikana katika Kutoka 20:12 yaani, “mheshimu baba yako na mama yako,” inapasa kufuatwa na watu wa kila umri. Kwa hakika, Yesu alipozungumzia amri hiyohiyo inayotajwa kwenye Mathayo 15:4-6, ni wazi kwamba alikuwa akizungumzia heshima ambayo watu wazima wanapaswa kuwaonyesha wazazi wao.

Kitabu cha Biblia cha Methali kinawaonya watu wasiwadharau wazazi wao. Methali 23:22 inasema “usimdharau mama yako kwa sababu tu amezeeka.” Methali 19:26 inaonya vikali kwamba yule “anayemtendea vibaya baba yake na ambaye humfukuza mama yake ni mwana anayetenda kwa aibu na bila heshima.”

Maandiko yanaonyesha wazi kwamba hatupaswi kuwapuuza wazazi wetu. Bado tuna uhusiano na wazazi wetu hata kama hawakubali dini yetu. Kanuni hizo za Biblia zinahusu pia watu wengine wa ukoo na wenzi wa ndoa. Ni wazi kwamba Wakristo wana wajibu wa kimaadili na wa Kimaandiko wa kuwapenda watu wao wa ukoo.

Usawaziko Ni Muhimu

Bila shaka, Biblia inaonya kuhusu mashirika mabaya na huenda hata yakahusisha watu wa ukoo wa karibu. (1 Wakorintho 15:33) Watumishi wengi waaminifu wa Mungu wa kale walitetea kweli wajapopingwa na wazazi. Ndivyo ilivyokuwa na wana wa Kora. (Hesabu 16:32, 33; 26:10, 11) Wakristo wa kweli hawapaswi kuacha imani yao ili kuwafurahisha wengine, hata kama ni watu wao wa ukoo.—Matendo 5:29.

Nyakati nyingine, wazazi au watu wengine wa ukoo hupinga vikali imani ya Mkristo. Huenda baadhi yao wakachukia kabisa Ukristo wa kweli. Katika hali kama hizo, Wakristo hutenda kwa usawaziko ili kulinda hali yao ya kiroho. Yesu alisema hivi kwa kufaa: “Adui za mtu watakuwa watu wa nyumbani kwake mwenyewe. Anayempenda baba au mama kuliko mimi hanistahili; naye anayempenda mwana au binti kuliko mimi hanistahili.”—Mathayo 10:36, 37.

Hata hivyo, mara nyingi Wakristo hawapingwi vikali na watu wa ukoo. Ni kwamba tu hawakubaliani na mafundisho yao ya Biblia. Maandiko Matakatifu huwahimiza wanafunzi wa Kristo wawatendee wasioamini “kwa upole” na “heshima kubwa.” (2 Timotheo 2:25; 1 Petro 3:15) Biblia inatoa shauri hili linalofaa: “Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote.” (2 Timotheo 2:24) Mtume Paulo pia aliwashauri Wakristo “wasiseme vibaya juu ya yeyote, wasiwe wataka-vita, wawe wenye usawaziko, wakionyesha upole wote kuelekea watu wote.”—Tito 3:2.

Wasiliana Nao na Uwaonyeshe Unawapenda

Wakristo wanahimizwa hivi kwenye 1 Petro 2:12: ‘Dumisheni mwenendo wenu ukiwa mzuri katikati ya mataifa [wasioamini], ili likiwa tokeo la matendo yenu mazuri ambayo wameshuhudia kwa macho, wamtukuze Mungu.’ Mara nyingi, watu wa ukoo ambao si waamini huona jinsi ambavyo Biblia imebadili maisha yetu. Usisahau kwamba watu wengi waliochukia au hata kupinga kweli ya Biblia wamebadili maoni yao. Huenda walitazama kwa miaka mingi mwenendo mzuri wa mtoto au mwenzi wao wa ndoa, halafu wakaamua kuchunguza sababu ya mwenendo wao mzuri. Mkristo hapaswi kuwafanya watu wa ukoo wakatae kweli ya Biblia kwa sababu amewapuuza.

Ni kweli kwamba hali hutofautiana, na Wakristo fulani Mashahidi huishi mbali na wazazi wao. Hivyo huenda wasiweze kuwatembelea mara nyingi wapendavyo. Lakini tunaweza kuwahakikishia kwamba tunawapenda kwa kuwaandikia barua, kuwapigia simu, au kwa kuwasiliana nao kwa ukawaida kwa njia nyingineyo. Wengi ambao si Wakristo wa kweli huwapenda wazazi na watu wao wa ukoo na huwasiliana nao kwa ukawaida licha ya kuwa na dini tofauti. Ikiwa wanafanya hivyo, sembuse Wakristo wa kweli?

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ukiwasiliana na watu wa ukoo, utawahakikishia kwamba unawapenda