Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuokoa Dunia

Jinsi ya Kuokoa Dunia

Jinsi ya Kuokoa Dunia

LICHA YA hali mbaya ya kimazingira inayokumba dunia, tungependa sana mambo yabadilike kwa sababu hayo ndiyo makao yetu, na labda ya watoto wetu, na watoto wao. Je, kuna jambo tunaloweza kufanya ili mataraja yetu yatimie?

Ukweli ni kwamba ingawa watu wengi wanahangaikia mazingira, wengi hutupa takataka chini, mtoni, au huacha taa zikiwaka wakati ambapo hawazitumii. Huenda mambo hayo yakaonekana kuwa madogo, lakini iwapo kila mmoja wa mabilioni ya watu duniani angezingatia jinsi anavyoitendea dunia, kungekuwa na mabadiliko. Tunaweza kuchangia uhifadhi wa mazingira kwa kutumia nishati vizuri, kushirikiana na miradi ya kutumia taka kwa manufaa, na kutupa taka mahali pafaapo. Matendo yetu yanaweza kuonyesha kwamba tunaitunza dunia.

Hata hivyo, hatuwezi kudhibiti matendo ya watu wengi. Je, hilo linamaanisha kwamba hakuna suluhisho lolote?

Suluhisho la Kudumu Liko Karibu

Thilo Bode wa shirika la Greenpeace alitoa maelezo yafuatayo kuhusu kiini cha matatizo ya mazingira, ambayo yalinukuliwa na gazeti Time: “Lengo letu kuu ni kwamba mashirika yanapaswa kuzingatia jinsi mabaki ya bidhaa zao yanavyopaswa kutupwa. Mashirika hayo yanapaswa kuzingatia mambo matatu: kutengeneza, kutumia, na kutupa.” Tunaweza kutengeneza bidhaa, tunajua jinsi ya kuzitumia, lakini inasikitisha kwamba hatujui jinsi ya kuzitupa ifaavyo. Wakati mwingine, watu hawajui tu jinsi ya kuzitupa bila kuchafua mazingira.

Wanadamu wamepungukiwa, lakini Muumba wa dunia hajapungukiwa. Tayari ameonyesha hekima yake isiyo na kifani kupitia vitu alivyoumba duniani. Anajua kutengeneza, kutumia, na kutupa vitu ifaavyo. Vitu vingi ambavyo ametengeneza hujiendesha vyenyewe. Mbegu huota, na mmea hukua na kuzaa matunda. Kisha mmea huo hunyauka, na bila kuchafua mazingira mabaki yake huwa mbolea inayoweza kutumiwa tena. Hiyo ni njia bora ya kutupa takataka! Haitokezi sumu!

Muumba hakusudii kuiacha dunia ichafuliwe kabisa na kuwa pipa la takataka lisiloweza kukaliwa. Biblia inasema hivi kwenye Isaya 45:18: “Yehova, . . . Yeye Mungu wa kweli, Mfanyizaji wa dunia na Mtengenezaji wake, Yeye aliyeifanya imara, ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu.”

Ikiwa Mungu aliiumba dunia ikaliwe, kwa nini ameruhusu iharibiwe sana? Biblia inaeleza kwamba hapo mwanzoni mwanadamu aliwekwa katika paradiso. Kwa hakika, Mungu alikusudia kwamba Paradiso hiyo ienee duniani pote na ijae watu. (Mwanzo 1:28) Hata hivyo, uasi ulitokea. Mwanamume na mwanamke wa kwanza hawakutaka kuendelea kujitiisha kwa utawala wa Mungu.

Mungu aliwaruhusu wanadamu wajaribu njia zao wenyewe za kutawala. Matokeo yanaonekana leo, yaani, wameshindwa kabisa. Wanadamu wameonyesha wazi kwamba hawawezi kutatua matatizo yanayowakumba. Mungu hapaswi kulaumiwa. Ni kama tu vile Biblia inavyosema kuhusu jamii ya wanadamu: “Wametenda kwa uharibifu; wao si watoto wake, kasoro ni yao wenyewe. Kizazi kilicho kombo na kilichopotoka!”—Kumbukumbu la Torati 32:5.

Hata hivyo, si kwamba Mungu amepuuza uharibifu wa dunia. Atatenda bila kukawia, kabla dunia haijawa mahali pasipokalika. Twajuaje hilo? Andiko la Ufunuo 11:18 laeleza hivi: “Mataifa wakawa na ghadhabu, nayo ghadhabu yako mwenyewe ikaja, na wakati uliowekwa . . . kuwaharibu wale wanaoiharibu dunia.” Uharibifu wa dunia utakomeshwa.

Bado kusudi la awali la Mungu, kwamba dunia iwe paradiso, litatimizwa. Maneno ya Mungu yanaonyesha kwamba itakuwa hivyo. Kwa mfano, alisema: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu linalotoka katika kinywa changu. Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.” (Isaya 55:11) Utafurahia kusoma Isaya sura ya 35, ambapo Mungu anaeleza jinsi maeneo yaliyoharibiwa yatakavyofanywa kuwa bustani na mashamba yenye kuzaa matunda.

Hata sasa, imeonekana kwamba dunia inaweza kujifanyiza upya ikiwa uchafuzi utakomeshwa. Mungu aliiumba na uwezo huo. Iwapo uchafuzi utakomeshwa, aina nyingi za vijiumbe vilivyo majini na udongoni vinaweza kurekebisha sehemu kubwa iliyoharibiwa. Isitoshe, tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu akichukua hatua na kuongoza mambo, kazi ya kusafisha dunia itafanywa vizuri zaidi. Anaweza kutoa mazoezi na mwongozo mkamilifu ambao wanadamu wamekosa leo.

Kwa hiyo, kuna tumaini kwa dunia. Mimea na wanyama wataokolewa. Viumbe hawatatokomea tena. Hewa na maji yetu yatakuwa safi tena. Wanadamu watiifu watakuwapo ili kuyafurahia. Je, ungependa kuona mambo hayo? Unaweza. Unapaswa kufanya nini? Biblia inaeleza yale unayopaswa kufanya. Mbona usiichunguze Biblia hatua kwa hatua ili ujue la kufanya? Waombe wachapishaji wa gazeti hili wakusaidie kupata mtu anayeweza kukufunza mambo hayo. Mbona upoteze fursa ya kujifunza jinsi ambavyo wewe na familia yako mnavyoweza kufurahia mazingira safi milele?