Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kulala Mfululizo wa makala “Je, Unalala vya Kutosha?” (Machi 22, 2003) ulinifaa sana. Kwa kuwa binti yangu aliugua ghafula, nilianza kukosa usingizi. Baada ya siku tano au sita nilienda kwenye hospitali iliyo karibu nikatibiwa, sasa ninaweza kulala vizuri. Hata hivyo, makala zenu zilidokeza kwamba nifanye mazoezi ya kutosha mchana na si kabla ya kulala. Nitajaribu kutumia ushauri huo kadiri niwezavyo.

T. M., Japan

Hivi majuzi, nimekuwa nikichoka sana. Daktari wa familia yetu alinichunguza na akakata kauli kwamba silali vya kutosha usiku na kwamba dawa za kifafa nilizokuwa nikitumia zilikuwa zikiniathiri. Sikuamini uchunguzi wake. Juma moja baadaye nikapata makala zenu kuhusu usingizi. Nilizisoma zote, na baada ya kufanya jaribio lililo kwenye ukurasa wa 9, nikakubaliana na daktari wangu. Sasa ninajaribu kufuata madokezo yaliyo kwenye makala hiyo. Asanteni sana kwa habari hiyo iliyonifaa.

M. B., Marekani

Nazi Nataka kuwashukuru kwa makala “Mojawapo ya Matunda Muhimu Zaidi Duniani.” (Machi 22, 2003) Hivi majuzi nilitembelea Mexico, na nilijionea mwenyewe jinsi nazi zilivyo na faida nyingi! Niliona zikitumiwa kwa kila njia inayotajwa katika makala hiyo. Unaweza pia kutengeneza mgwisho wa kuwafukuzia nzi kwa kukata matawi ya mnazi, kuondoa majani yake, na kufunga tita la matawi 10 hadi 15!

D. S., Marekani

Makala hiyo ilinikumbusha jinsi nyanya yangu alivyotengeneza vikombe kutokana na mafuvu ya nazi katika miaka ya 1930. Majirani zake wengi walijenga nyumba kwa mbao za mnazi, na waliezeka mapaa kwa makuti yake yaliyokauka. Asanteni kwa makala hizo nzuri.

M. B., Marekani

Kumnyonyesha Mtoto Sehemu yenye kichwa “Faida za Kuwanyonyesha Watoto” katika makala “Kuutazama Ulimwengu” (Machi 22, 2003) ilinishtua. Ninakubali kwamba watoto ambao hawakunyonyeshwa wanaweza kuwa na matatizo ya mfumo wa kinga. Sikunyonyeshwa na nimepata mafua mara nyingi. Lakini inaumiza kunukuu uchunguzi unaoonyesha kwamba wale ambao hawakunyonyeshwa hawana akili nyingi kama wale ambao walinyonyeshwa.

C. B., Italia

“Amkeni!” linajibu: Hatukukusudia kumuumiza yeyote. Tulikuwa tu tunaripoti kuhusu utafiti uliofanywa nchini Denmark kuhusu kunyonyesha. Kuchapisha habari kama hizo huwasaidia wazazi wafanye maamuzi yafaayo kuhusu njia za kuwalea watoto.

Methali za Kiafrika Ama kweli, makala za Amkeni! huwa na habari mbalimbali. Nimesoma gazeti hilo kwa miaka 40 hivi, na nilifurahia sana makala yenye kichwa “Methali za Waakan—Zinaonyesha Maadili ya Kijamii.” (Machi 22, 2003) Ilinisaidia kuelewa jinsi tabia njema zinavyotusaidia kupatana na wanadamu wenzetu. Niliandika baadhi ya methali hizo ili nizisome mara kwa mara.

D. Z., Marekani

Sijawahi kamwe kusoma makala nzuri yenye kuchekesha na yenye kuarifu kama hiyo kuhusu methali. Ni jambo lenye kufurahisha kama nini kusoma kuhusu desturi za tamaduni nyingine. Baada ya kila methali, nilitua na kujaribu kutambua maana yake. Mara nyingi nilinoa!

J. K., Ujerumani