Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nawezaje Kujijengea Jina Bila Kuwategemea Ndugu Zangu?

Nawezaje Kujijengea Jina Bila Kuwategemea Ndugu Zangu?

Vijana Huuliza . . .

Nawezaje Kujijengea Jina Bila Kuwategemea Ndugu Zangu?

“Nilitaka kutambuliwa, lakini sikuzote nilihisi kwamba nilihitaji kuwaiga dada zangu. Nilihisi kwamba singeweza kutimiza mambo ambayo walikuwa wamefanya.”—Clare.

JE, UNA ndugu au dada ambaye hufanikiwa katika karibu mambo yote? Je, wazazi wako hukuhimiza kila wakati uwe kama ndugu au dada yako? Ikiwa ni hivyo, huenda ukahofu kwamba sikuzote utatambuliwa kwa sababu yake tu, au kwamba utaheshimiwa tu ukitimiza yale ambayo ametimiza.

Ndugu za Barry * wakubwa ni wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma * inayoheshimiwa sana na ni Wakristo wenye sifa nzuri sana. Barry akiri hivi: “Sikujiamini kwa kuwa nilihisi kwamba singeweza kuwa na ustadi wa kuhubiri au kuwa msemaji mzuri kama wao. Nilishindwa kupata marafiki kwa sababu niliandamana tu na ndugu zangu walipoalikwa. Nilihisi kwamba watu walinichangamkia tu kwa sababu ya ndugu zangu.”

Ni rahisi kuona wivu ikiwa una ndugu ambaye husifiwa mara nyingi. Katika nyakati za Biblia, kijana Yosefu alikuwa mashuhuri kuliko ndugu zake. Ndugu zake walimwonaje? ‘Walianza kumchukia, nao hawakusema naye kwa amani.’ (Mwanzo 37:1-4) Bila shaka, Yosefu alikuwa mnyenyekevu. Lakini ndugu au dada yako anaweza kuchochea chuki na hasira akitajataja mafanikio yake kila wakati.

Vijana fulani huamua kuasi—labda kwa kutofanya vizuri shuleni kimakusudi, kupunguza bidii yao katika utendaji wa Kikristo, au kuwa na mwenendo mbaya. Huenda wakafikiri kwamba ikiwa hawawezi kufanya vyema kama ndugu zao, hakuna haja ya kujitahidi. Lakini, mwishowe uasi utakuumiza tu. Unawezaje kujijengea jina bila kuwategemea ndugu zako na bado ujiheshimu?

Sitawisha Maoni Yanayofaa Kuwahusu

Unapoona ndugu yako akisifiwa, huenda ukafikiri kwamba yeye ni mkamilifu na kwamba huwezi kamwe kufaulu kama yeye. Lakini, je hiyo ni kweli? Biblia inaeleza wazi hivi: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.”—Waroma 3:23.

Naam, hata ndugu zetu wawe na uwezo au vipawa vya aina gani, bado ni ‘wanadamu walio na udhaifu’ kama sisi. (Matendo 14:15) Hakuna haja ya kuwaheshimu kupita kiasi au kuwaabudu. Mwanadamu pekee aliyeweka mfano mkamilifu ni Yesu Kristo.—1 Petro 2:21.

Jifunze Kutokana Nao!

Jitahidi kuona hali yako kuwa fursa ya kujifunza. Kwa mfano, wafikirie ndugu na dada za Yesu Kristo. (Mathayo 13:55, 56) Wazia mambo ambayo wangeweza kujifunza kutokana na ndugu yao mkamilifu! Hata hivyo, “ndugu zake walikuwa hawamwamini.” (Yohana 7:5) Huenda hawakumwamini kwa sababu ya kiburi na wivu. Ndugu za kiroho wa Yesu, yaani wanafunzi wake, ndio walioitikia mwaliko wake: “Mjifunze kutoka kwangu.” (Mathayo 11:29) Baada ya ufufuo wake, ndipo ndugu za Yesu walitambua kwamba wangejifunza kutokana naye. (Matendo 1:14) Kabla ya wakati huo, walipoteza nafasi za pekee za kujifunza kutokana na ndugu yao mashuhuri.

Kaini alifanya kosa hilohilo. Abeli, ndugu yake, alikuwa mtumishi wa Mungu mwenye sifa nzuri. Biblia inasema kwamba “Yehova alikuwa akimtazama Abeli na toleo lake kwa kibali.” (Mwanzo 4:4) Hata hivyo, kwa sababu fulani Mungu “hakumtazama Kaini na toleo lake kwa kibali chochote.” Kaini angejinyenyekeza na kujifunza kutokana na ndugu yake. Badala yake, “Kaini akawaka hasira” na mwishowe akamuua Abeli.—Mwanzo 4:5-8.

Bila shaka huwezi kumkasirikia hivyo ndugu yako. Lakini unaweza pia kupoteza fursa za pekee ukiruhusu kiburi na wivu ukuzuie. Ikiwa ndugu yako anajua sana hesabu, ni hodari katika historia, ni bingwa katika mchezo unaoupenda, anajua Maandiko sana, au ni msemaji stadi, hupaswi kumwonea wivu! Kwani, “wivu hufanya mifupa iwe na ubovu” na unaweza tu kukudhuru. (Methali 14:30; 27:4) Badala ya kumkasirikia ndugu yako, jaribu kujifunza kutoka kwake. Tambua kwamba ana vipawa au stadi ambazo huna. Tazama jinsi anavyofanya mambo au hata umwombe akusaidie.

Barry, aliyetajwa mapema, alifaidika kutokana na mfano mzuri wa ndugu zake. Anasema hivi: “Niliona jinsi ndugu zangu walivyokuwa na furaha kwa sababu walikuwa tayari kuwasaidia wengine kutanikoni na katika mahubiri. Kwa hiyo niliamua kuiga mfano wao, na nikashiriki ujenzi wa Majumba ya Ufalme na Betheli. Uzoefu niliopata umenisaidia kujiamini na kukuza uhusiano wangu pamoja na Yehova.”

Kutambua Vipawa Vyako

Huenda hutaki kumwiga ndugu yako kwa sababu unataka kuwa tofauti. Lakini haimanishi utabadilika. Mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo wa karne ya kwanza hivi: “Iweni waigaji wangu.” (1 Wakorintho 4:16) Je, inamaanisha kwamba Paulo hakutaka wawe na utu wao wenyewe? Sivyo hata kidogo. Mtu anaweza kufanya mambo mengi kwa njia tofauti. Haimaanishi kuwa una kasoro eti kwa sababu huwezi kufanya hesabu vizuri kama ndugu yako. Ni kwamba tu mnatofautiana.

Paulo anatoa shauri hili: “Kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.” (Wagalatia 6:4) Mbona usijitahidi kusitawisha stadi na vipawa vyako? Kujifunza lugha ya kigeni, kucheza ala ya muziki, au kutumia kompyuta kwaweza kukusaidia ujiheshimu zaidi, na kuwa na stadi muhimu. Usijaribu kuwa mkamilifu! Jifunze kufanya mambo kwa ukamili, kwa uwezo wako wote, na kwa ustadi. (Methali 22:29) Huenda usiwe na kipawa fulani, lakini “mkono wa wenye bidii ndio utakaotawala,” yasema Methali 12:24.

Hata hivyo, unapaswa hasa kusitawisha sifa zako za kiroho. Stadi za kiroho hudumu kuliko kipawa chochote kinachoweza kuwavutia wengine. Wafikirie wale ndugu mapacha Esau na Yakobo. Esau alisifiwa sana na baba yake kwa sababu alikuwa “mwanamume anayejua jinsi ya kuwinda, mwanamume wa mbugani.” Mwanzoni, huenda Yakobo ndugu yake, hangetambuliwa kwa urahisi kwa sababu alikuwa “mwanamume asiye na lawama, akikaa katika mahema.” (Mwanzo 25:27) Esau alishindwa kusitawisha sifa za kiroho akakosa baraka. Yakobo alisitawisha upendo kwa mambo ya kiroho akabarikiwa sana na Yehova. (Mwanzo 27:28, 29; Waebrania 12:16, 17) Unajifunza nini? Sitawisha hali yako ya kiroho, ‘acha nuru yako iangaze,’ na “maendeleo yako [yatakuwa] wazi kwa watu wote.”—Mathayo 5:16; 1 Timotheo 4:15.

Clare, aliyetajwa mwanzoni, anasema hivi: “Niliridhika kuwafuata dada zangu wakubwa. Lakini nikaamua kutii shauri la Maandiko la ‘kupanuka’ katika upendo wangu. Nilihubiri na washiriki mbalimbali wa kutaniko, na kutafuta njia za kuwasaidia wenye uhitaji kutanikoni. Pia niliwaalika ndugu na dada wa umri mbalimbali nyumbani kwetu na kuwaandalia chakula. Sasa nina marafiki wengi na ninajiheshimu zaidi.”—2 Wakorintho 6:13.

Mara kwa mara, wazazi wako wanaweza kukuhimiza uwe kama ndugu au dada yako. Lakini ukitambua kwamba wazazi wako wana nia nzuri, hutahuzunika sana. (Methali 19:11) Hata hivyo, huenda ikafaa uwaambie wazazi wako kwa heshima jinsi unavyohisi wanapokulinganisha na wengine. Labda watatumia njia nyingine za kukushauri.

Usisahau kamwe kwamba Yehova Mungu anakuona unapomtumikia. (1 Wakorintho 8:3) Barry akata kauli hii: “Kadiri ninavyomtumikia Yehova, ndivyo ninavyokuwa mwenye furaha zaidi. Watu wananiheshimu na kunithamini kama wanavyowathamini ndugu zangu.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 5 Inayopangwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Je, ndugu yako husifiwa mara nyingi?

[Picha katika ukurasa wa 26]

Tambua vipawa na mapendezi yako

[Picha katika ukurasa wa 26]

‘Acha nuru yako iangaze’ kwa kusitawisha sifa za kiroho