Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Dawa za Kulevya Jalada la toleo la Aprili 8, 2003 (“Ufanye Nini Kijana Wako Akitumia Dawa za Kulevya?”) lilinivutia. Nimekuwa nikimfunza Biblia mwanamke anayeitwa Linda. Watoto wake wawili ni wazoefu wa dawa za kulevya. Asubuhi iliyofuata nilijifunza naye toleo hilo—fungu baada ya fungu. Lilimtia moyo na kumwimarisha sana. Habari hiyo ilimfaa sana.

C. M., Marekani

Ninasimamia shughuli za kusaidia familia kukabiliana na matumizi ya dawa za kulevya na vileo. Ingawa mimi ni Mkatoliki, mimi hupenda kusoma Amkeni! Ninataka kuwashukuru kwa makala kuhusu dawa za kulevya katika familia. Nilifurahia kuzisoma, nazo zitanisaidia katika kazi yangu ya kuwasaidia vijana.

H. C., Ekuado

Kutumia Mikono Nilisoma makala “Kula kwa Mikono” katika toleo la Aprili 8, 2003. Nina umri wa miaka kumi, na nilijaribu kutumia mikono kula kitoweo chenye moto cha nyama na viazi. Haikuwa rahisi. Lakini nilikifurahia, na kilikuwa kitamu! Asanteni kwa makala hiyo. Nimeanza kubeba Amkeni! shuleni na kulisoma wakati wa mapumziko.

M. T., Japan

Maswali ya Biblia Ninataka kuwajulisha kwamba ninapenda mafumbo ya kujaza maneno mnayochapisha. Yamenisaidia kujifunza mambo mengi.

R. N., Marekani

Nimewafundisha watoto wangu Biblia tangu walipokuwa wachanga sana. Lakini sasa kwa kuwa wamekua, ni vigumu kuwavutia kwa mambo ya kiroho. Kwa hiyo, nimekuwa nikitafuta njia za kuwasaidia. Nilipopokea toleo la Aprili 8 na kuchunguza makala “Je, Wajua?,” nilipata njia ya kuwasaidia. Mara moja, nikawapa watoto wangu majibu mbalimbali ya kuchagua na kubandika maswali hayo ukutani. Mwanzoni hawakupendezwa, lakini baada ya muda fulani walianza kujibu. Sasa tunatumia maswali hayo katika mazungumzo ya familia.

R. M., Japan

“Amkeni!” linaeleza: Maswali ya Biblia katika makala “Je, Wajua?” huchapishwa katika magazeti ya “Amkeni!” ya lugha ambazo hazina fumbo la kujaza maneno.

Nazi Nilifurahia sana kusoma makala “Mojawapo ya Matunda Muhimu Zaidi Duniani,” katika toleo la Machi 22, 2003. Mimi na rafiki yangu hufurahia kutengeneza sabuni. Tunatumia mafuta ya nazi kutengeneza sabuni kwa sababu ni nzuri kwa ngozi na hutokeza povu nyingi. Baada ya kusoma makala hiyo, nilithamini nazi hata zaidi.

C. B., Kanada

Uhuru wa Kusema Nimemaliza tu kusoma mfululizo wa makala wenye kichwa “Mahakama ya Juu ya Marekani Yatetea Uhuru wa Kusema.” (Januari 8, 2003) Niliposoma makala hizo nilishangaa kuona kwamba mjadala huo bado unaendelea huko Marekani, nilivutiwa na jinsi ndugu zetu Wakristo walivyoeleza msimamo wetu kwa ustadi, na kushukuru kwamba maamuzi ya haki yanaweza kutolewa hata katika ulimwengu huu usio na haki. Mimi hufurahia sana kuhubiri habari njema. Makala kama hizo huongeza ujuzi wetu.

O. S., Belarus

Faragha Makala zenye kichwa “Je, Faragha Yako Inaingiliwa?” (Januari 22, 2003) zilinisaidia kuelewa vizuri kinachomaanishwa na kuheshimu haki za wengine. Kwa kweli, kuingilia faragha za wengine ni aina ya wizi na huleta matokeo mabaya. Tukiwa Wakristo, sisi huwa na uhusiano wa karibu pamoja na wengine. Lakini ni rahisi kusahau kwamba kuna mipaka.

T. M., Jamhuri ya Cheki