Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unawezaje Kushinda Tamaa Mbaya?

Unawezaje Kushinda Tamaa Mbaya?

Maoni ya Biblia

Unawezaje Kushinda Tamaa Mbaya?

“Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.”—WAROMA 7:21.

HUENDA Paulo ndiye aliyejitahidi sana kuendeleza viwango vya juu vya Kikristo kuliko mtume mwingine yeyote. (1 Wakorintho 15:9, 10) Na bado aliungama kama inavyoonyeshwa hapa juu. Sikuzote alikabiliana na pambano kati ya akili yake na tamaa mbaya. Je, umewahi kuhisi kama alivyohisi mtume Paulo? Tukiwa viumbe wasiokamilika, ni nani kwa kweli hajakabiliana na pambano hilo?

Kwa watu wengi pambano hilo ni kali zaidi. Wengine hupambana na tamaa zisizofaa za ngono. Wengine ni watumwa wa kucheza kamari, tumbaku, dawa haramu, au vileo. Tunapokabili tamaa mbaya zinazodhuru, tunaweza kuzishindaje? Kuna msaada gani? Je, pambano dhidi ya tamaa mbaya litakwisha?

Upendo—Njia Bora ya Kushinda Tamaa Mbaya

Yesu alitaja amri mbili zilizo kubwa zaidi katika Sheria ya Musa. Ya kwanza ni: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:37) Ikiwa tunampenda Mungu kama Yesu alivyoamuru, tamaa yetu kuu inapaswa kuwa kumfurahisha. Tukifanya hivyo, tamaa hiyo nzuri inaweza kutusaidia hata tunapokabili tamaa zenye nguvu sana! Jambo hilo linawezekana. Kila siku mamilioni ya Wakristo hushinda tamaa mbaya. Unawezaje kusitawisha upendo huo wenye nguvu kwa Mungu? Kwa kutafakari na kuthamini wema wake ambao unaonekana katika uumbaji, katika Biblia, na jinsi anavyotutendea tukiwa mtu mmoja-mmoja.—Zaburi 116:12, 14; 119:7, 9; Waroma 1:20.

Amri ya pili iliyo kuu zaidi ambayo Yesu alitaja ni: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Mathayo 22:39) Mtume Paulo alisema kwamba upendo “haujiendeshi bila adabu” na “hautafuti faida zake wenyewe.” Upendo kama huo wa kweli hutusaidia tuepuke mwenendo unaoweza kuwaumiza wengine. (1 Wakorintho 13:4-8) Unaweza kusitawishwaje? Kwa kujiweka katika hali za wengine na kuhangaikia hisia zao na masilahi yao kwa unyoofu.—Wafilipi 2:4.

Kuna Msaada Gani?

Kwa kuwa Mungu anaelewa ni vigumu kwetu kufanya yaliyo sawa, ametusaidia kwa njia mbalimbali. Kupitia Neno lake, Biblia, anatufundisha kuchukia lililo baya na kumpa heshima anayostahili. (Zaburi 86:11; 97:10) Biblia ina masimulizi yanayoonyesha matokeo mabaya ya kuongozwa na tamaa mbaya. Zaidi ya hilo, Yesu alisema kwamba tukimwomba Mungu, atatupatia roho takatifu, ambayo ni kani yenye nguvu zaidi duniani. (Luka 11:13) Inaweza kuimarisha azimio letu la kufanya yaliyo sawa. Tunaweza pia kutegemezwa na kutiwa moyo na Wakristo wengine wanaopambana na tamaa mbaya. (Waebrania 10:24, 25) Tunapoimarishwa jinsi hiyo tunasaidiwa kutenda yaliyo sawa. (Wafilipi 4:8) Je, misaada hiyo ina matokeo?

Mfikirie Fidel, aliyejulikana kuwa mlevi katika eneo lao. Alivuta sigara, alicheza kamari, na alipigana na wengine alipolewa. Kujifunza Biblia na kushirikiana na Mashahidi wa Yehova kulimsaidia ashinde mazoea hayo. Sasa anaishi maisha yenye furaha pamoja na mkewe na watoto wao wawili.

Huenda mtu akajiuliza, ‘Vipi nikirudia tabia mbaya?’ Mtume Yohana alizungumzia jambo hilo. Aliandika hivi: “Watoto wangu wadogo, ninawaandikia ninyi mambo haya ili msitende dhambi. Na bado, yeyote akitenda dhambi, tuna msaidizi kwa Baba, Yesu Kristo, mtu mwadilifu. Na yeye ni dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu, lakini si kwa ajili ya zetu tu bali pia kwa ajili ya zile za ulimwengu wote.” (1 Yohana 2:1, 2) Naam, dhabihu ya Yesu hufunika makosa ya mtu anayetubu na kujitahidi kwa unyoofu kufanya mabadiliko ili ampendeze Mungu. Kukiwa na msaada huo, je, kuna sababu yoyote ya kuacha kujitahidi kufanya yaliyo sawa?

Tamaa Mbaya Zitakomeshwa

Tukisitawisha upendo kwa Mungu na jirani na kutumia misaada ambayo Mungu anatupatia, tunaweza kushinda tamaa mbaya hata sasa. Isitoshe, Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba pambano hilo halitaendelea milele. Hivi karibuni, wale wanaotumia misaada ya kiroho kutoka kwa Mungu wataponywa kabisa kimwili na kiroho. (Ufunuo 21:3-5; 22:1, 2) Watawekwa huru kutokana na dhambi na kifo. (Waroma 6:23) Kwa upande mwingine, watu wanaoendelea kuongozwa na tamaa mbaya zinazodhuru hawatapata baraka hizo.—Ufunuo 22:15.

Inafariji sana kujua kwamba pambano letu dhidi ya tamaa mbaya halitaendelea milele. Tamaa hizo zitakomeshwa kabisa. Kitulizo kilichoje!