Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Je, Watoto Wanakua Haraka Mno? Mfululizo wa makala “Je, Watoto Wanakua Haraka Mno?” (Aprili 22, 2003) uliandikwa vizuri sana. Ulinisaidia kuelewa sababu ya matatizo yangu. Nilikuwa na maisha magumu ya utotoni, na ninakubali kwamba ni jambo la hekima kumruhusu mtoto afurahie maisha ya utotoni.

S. M., Japan

Makala hizo zilinigusa moyo sana. Nililelewa katika familia ya mzazi mmoja. Mara nyingi sikulala kwa kuwa nilimsikia mama yangu akilia kwa sababu ya matatizo. Sijui maisha yangu yangekuwaje kama kutaniko la Kikristo halingenisaidia. Asanteni kwa jitihada zenu zenye upendo za kutulisha kiroho.

D. B., Marekani

Nina umri wa miaka 11 na sikuzote nimetamani kukua haraka. Makala hizo zilinionyesha umuhimu wa kuthamini maisha yangu ya utotoni.

G. M., Marekani

Maisha yangu yanafanana na yale ya Carmen na dadake waliotajwa katika makala hiyo. Ijapokuwa sikutoroka nyumbani kama walivyofanya, baba zangu wa kambo walinitesa na mamangu akanipuuza. Kwa kuwa wazazi wangu walitumia dawa za kulevya, nililazimika kuwalea ndugu zangu wadogo nilipokuwa mwenye umri wa miaka kumi tu! Bila shaka jambo hilo liliniletea matatizo zaidi. Namshukuru Yehova daima kwa msaada ambao amenipa kwa miaka mingi.

D. S., Marekani

Nungunungu Mimi ni msimamizi wa Chama cha Uingereza cha Kuhifadhi Nungunungu, na nilifurahia kusoma makala nzuri yenye kichwa “Mnyama Mdogo Mwenye Miiba wa Mashambani.” (Aprili 22, 2003) Tofauti na magazeti mengine, iliandikwa vizuri na habari zake ni sahihi.

F. V., Uingereza

Asanteni sana kwa gazeti la Amkeni! Sikuzote mama yangu huniambia nisome Amkeni! Ninapoanza kulisoma, mimi huendelea kwa saa moja au zaidi. Mimi hufurahia makala nyingi, kama vile “Mnyama Mdogo Mwenye Miiba wa Mashambani.” Nina umri wa miaka 15 sasa. Endeleeni kufanya kazi hiyo nzuri.

K. G., Marekani

Wazazi Walezi Asanteni kwa makala nzuri “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Nina Wazazi Walezi?” (Aprili 22, 2003) Binti yangu alilazimika kumkabidhi mtoto wake kwa wazazi walezi kwa sababu ya hali zake, na jambo hilo lilinisumbua sana. Habari hiyo ilikuja kwa wakati unaofaa. Nilimtumia binti yangu makala hiyo.

E. D., Guyana

Ninaandika ili niwashukuru sana kwa ajili ya makala za wakati unaofaa kuhusu wazazi walezi katika matoleo ya Aprili 22 na Mei 22. Hivi majuzi mimi na mume wangu tumeanza kumlea mvulana mchanga. Baadaye tutatumia makala hizo kumsaidia mwana wetu atambue na kuelewa jinsi anavyopendwa na Yehova Mungu, Baba yake, na mimi.

S. R., Marekani

Asanteni sana kwa makala zinazohusu wazazi walezi. Nina umri wa miaka 47 na bado nasumbuka kwa sababu ya jambo hilo. Wazazi wangu—ambao nawaheshimu na kuwapenda sana—hawakuweza kunionyesha upendo niliohitaji. Hawakunikumbatia wala kunibusu, hata nilipowaomba. Jambo hilo lilinilemea. Hata hivyo, makala hiyo ilinifariji sana na kunichangamsha moyo sana.

D. H., Marekani