Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuishi na Ugonjwa wa Kihisia

Kuishi na Ugonjwa wa Kihisia

Kuishi na Ugonjwa wa Kihisia

WATU wengi sana wanaugua magonjwa ya kihisia. Kwa mfano, inakadiriwa kwamba zaidi ya watu milioni 330 ulimwenguni pote wameshuka moyo sana, hali inayowafanya wahuzunike sana na wasipendezwe na shughuli za kila siku. Inakadiriwa kwamba miaka 20 ijayo, idadi ya watu walioshuka moyo itazidi ile ya wagonjwa wengine isipokuwa tu wagonjwa wa moyo. Basi si ajabu kwamba watu wanasema ugonjwa huo umewakumba watu wengi kama mafua.

Katika miaka ya karibuni, watu wengi zaidi wameufahamu ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Dalili za ugonjwa huo zinatia ndani kushuka moyo na baadaye kusisimuka kupita kiasi. Kitabu kimoja kilichochapishwa hivi majuzi na Chama cha Kitiba cha Marekani kinasema kwamba “mtu anaposhuka moyo, anaweza kutaka kujiua. Wakati mtu amesisimuka sana, anaweza kushindwa kuamua mambo vizuri na kufanya mambo hatari bila kutambua.”

Inakadiriwa kwamba asilimia 2 ya watu nchini Marekani wanaugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika, hivyo kuna mamilioni ya watu wanaougua ugonjwa huo nchini humo pekee. Hata hivyo, takwimu hazionyeshi msononeko ambao wagonjwa hao hupata.

Mtu Hulemewa na Huzuni Anaposhuka Moyo

Wengi wetu tunajua jinsi mtu huhisi anapohuzunika. Baada ya muda mfupi, labda saa au siku kadhaa, huzuni hiyo huisha. Hata hivyo, ugonjwa wa kushuka moyo ni tofauti. Kwa njia gani? Dakt. Mitch Golant anasema kwamba ‘sisi ambao hatuna ugonjwa wa kushuka moyo tunajua kwamba hatimaye huzuni hutoweka, lakini kwa watu wenye ugonjwa huo huzuni hufuatwa na msisimuko, kisha hisia hizo hubadilika-badilika daima.’

Ugonjwa wa kushuka moyo huathiri watu kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, wengine huugua katika majira fulani, hasa majira ya baridi kali. Kitabu kilichochapishwa na Chama cha Kitiba cha Umma kinasema: “Watu wanaoshuka moyo katika majira fulani huathiriwa zaidi wakiwa katika maeneo ya kaskazini ya dunia na kukiwa na mawingu mengi. Ingawa inasemekana kwamba watu hao huathiriwa zaidi wakati wa baridi kali, wakati mwingine wao huathiriwa pia wanapofanya kazi mahali penye giza, wakati wowote ambapo kuna mawingu, na wasipoona vizuri.”

Ni nini kinachosababisha ugonjwa wa kushuka moyo? Haijulikani waziwazi. Ijapokuwa huenda mtu akarithi ugonjwa huo, mara nyingi watu huathiriwa na mambo yanayotukia maishani. Imeonekana kwamba wanawake huathiriwa mara mbili zaidi ya wanaume. * Lakini haimaanishi kwamba wanaume hawawezi kuugua. Inakadiriwa kwamba kati ya asilimia 5 na 12 ya wanaume wataugua ugonjwa wa kushuka moyo wakati fulani maishani mwao.

Mtu anapougua ugonjwa huo, karibu maisha yake yote huathiriwa. Sheila, anayeugua ugonjwa huo, anasema mgonjwa “huvurugika kabisa, hukosa kujiamini na kujiheshimu, hushindwa kufikiri vizuri na kufanya maamuzi vizuri, na huumia sana anapozidiwa.”

Wakati mwingine mgonjwa anaweza kufarijika kwa kumweleza mtu mwingine anayejali hisia zake. (Ayubu 10:1) Hata hivyo, tunapaswa kutambua kwamba kushuka moyo hakuwezi kumalizwa kwa kuwa na maoni yanayofaa tu wakati hali hiyo inaposababishwa na kemikali za mwili. Wakati huo, mgonjwa hawezi kudhibiti huzuni yake. Isitoshe, tayari huwa amefadhaishwa na hali hiyo kama tu watu wa familia na marafiki.

Mfikirie Paula, * Mkristo aliyehuzunika vibaya kabla ugonjwa wake haujatambuliwa. Anasema: “Wakati mwingine nilipokuwa kwenye mikutano ya Kikristo, nilirudi kwenye gari na kulia bila sababu yoyote. Nilijihisi mpweke sana na nilifadhaika sana. Ijapokuwa nilikuwa na marafiki wengi walionijali, bado nilihuzunika.”

Ellen pia alipatwa na jambo kama hilo, na alihitaji kulazwa hospitalini. Anasema: “Nina mume, wana wawili, na mabinti-wakwe wawili, na wote wananipenda sana.” Basi, Ellen anapaswa kuwa na furaha na kuhisi anathaminiwa na familia yake. Lakini mtu anaposhuka moyo, huwa na mawazo mabaya, hata ya kipumbavu, na anaweza kulemewa.

Pia ugonjwa huo unaweza kuathiri sana familia nzima. Dakt. Golant anaandika hivi: “Mtu unayempenda anaposhuka moyo, unaishi na wasiwasi kwa kuwa hujui kama atapata nafuu au atashuka moyo zaidi. Unaweza kuhisi mpweke na hata kuhuzunika na kukasirika kwa kuwa unaona maisha yamebadilika kabisa.”

Mara nyingi, watoto wanaweza kutambua kwamba mzazi ameshuka moyo. Dakt. Golant anaandika hivi: “Mtoto wa mama aliyeshuka moyo hutambua haraka hisia za mama yake, na huona mabadiliko yoyote yanayotokea.” Dakt. Carol Watkins anasema kwamba watoto wa mzazi aliyeshuka moyo “wanaweza kuwa na tabia zisizofaa, kushindwa kujifunza, na kutopatana na marafiki. Wanaweza kushuka moyo pia.”

Hisia Zinazobadilika-Badilika

Ugonjwa wa kushuka moyo hutatiza sana. Lakini iwapo pia mtu aliyeshuka moyo anasisimuka kupita kiasi, huwa anaugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. * Lucia anayeugua ugonjwa huo anasema: “Hisia za mtu anayeugua ugonjwa huo hubadilika-badilika daima.” Jarida The Harvard Mental Health Letter linasema kwamba katika kipindi cha kusisimuka kupita kiasi, mgonjwa “anaweza kuingilia mambo ya wengine na kuwatawala, na ghafula anaweza kushikwa na hasira.”

Lenore anakumbuka wakati aliposisimuka kupita kiasi. Anasema: “Nilikuwa na nguvu nyingi sana. Wengine waliniona kuwa mwanamke shujaa. Watu wengine waliniambia, ‘Laiti ningekuwa kama wewe.’ Mara nyingi nilijihisi nikiwa na nguvu nyingi sana, kana kwamba ningeweza kufanya jambo lolote. Nilifanya mazoezi kupita kiasi. Nilifanya kazi kila siku ijapokuwa nililala kwa muda mfupi sana—kwa saa mbili au tatu tu. Lakini, bado niliamka nikiwa na nguvu nyingi.”

Hata hivyo, baada ya muda Lenore akaanza kushuka moyo. Anasema: “Kipindi cha msisimuko kilipofikia upeo, nilihisi hasira kutoka ndani kama mashine iliyokuwa ikiendeshwa bila kuzimwa. Kwa ghafula, hisia zangu nzuri zikabadilika, nikawa mkali na mjeuri. Niliwafokea washiriki wa familia bila sababu. Nilikuwa mwenye hasira, mwenye chuki, na singejizuia hata kidogo. Baada ya hisia hizo zenye kutisha, nilichoka ghafula, nikalia, na kushuka moyo sana. Nilihisi kuwa mwovu na asiyefaa kitu. Wakati mwingine, ningebadilika na kuwa mchangamfu kama zamani kana kwamba hakuna kitu kilichokuwa kimetukia.”

Hisia zinazobadilika-badilika za mgonjwa huwavuruga washiriki wa familia. Mary, ambaye mume wake ana ugonjwa huo anasema hivi: “Mimi huvurugika ninapomwona mume wangu akiwa mwenye furaha na akiongea sana halafu ghafula anabadilika na kushuka moyo na kunyamaza. Ni vigumu sana kwetu kuamini kwamba hawezi kujizuia.”

Ni kweli kwamba mgonjwa hutaabishwa zaidi na ugonjwa huo. Mgonjwa mmoja anayeitwa Gloria anasema hivi: “Mimi hutamani niwe kama watu wanaoweza kudhibiti maisha yao. Ni mara chache tu ambapo wagonjwa wenye hisia zinazobadilika-badilika huishi maisha ya kawaida.”

Ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika husababishwa na nini? Ni rahisi zaidi mtu arithi ugonjwa huo kuliko ule wa kushuka moyo. Chama cha Kitiba cha Marekani kinasema: “Kulingana na uchunguzi wa kisayansi, watu wa karibu zaidi wa familia, yaani wazazi, ndugu, dada, au watoto wa watu wenye ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika wako katika hatari ya kupatwa na ugonjwa huo mara 8 mpaka 18 zaidi ya watu wanaotoka katika familia zisizo na ugonjwa huo. Isitoshe, kuna uwezekano mkubwa wa kushuka moyo sana ikiwa mtu wa familia ana ugonjwa huo.”

Tofauti na kushuka moyo, inaonekana ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika huwapata wanaume na wanawake kwa kiwango kilekile. Ijapokuwa mara nyingi ugonjwa huo huanza mtu anapokuwa mtu mzima, vijana na watoto wamepatikana na ugonjwa huo. Hata hivyo, kuchunguza dalili na kuutambua ugonjwa huo ni jambo gumu sana hata kwa wataalamu wa tiba. Dakt. Francis Mark Mondimore wa Chuo cha Tiba katika Chuo Kikuu cha Johns Hopkins, anaandika hivi: “Ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika ni ugonjwa wa akili unaobadilika kama kinyonga kwani dalili za wagonjwa hutofautiana na hata kipindi kimoja cha ugonjwa hutofautiana na kingine kwa mgonjwa yuleyule. Ugonjwa huo ni kama zimwi linalosababisha hofu nyingi na kutoweka, kisha hutokea tena kwa kishindo baada ya miaka mingi na kumfanya mgonjwa asisimuke kupita kiasi.”

Ni wazi kwamba si rahisi kugundua magonjwa ya kihisia na ni vigumu hata zaidi kukabiliana nayo. Lakini wagonjwa wana matumaini.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Sababu moja ni kwamba wanawake wanaweza kushuka moyo baada ya kujifungua na kuathiriwa na mabadiliko ya homoni wakati wa kukoma kwa hedhi. Pia, wanawake huenda hospitalini mara nyingi na hivyo wengi huchunguzwa.

^ fu. 11 Baadhi ya majina katika makala hizi yamebadilishwa.

^ fu. 16 Madaktari wanasema kwamba mara nyingi kila hisia huendelea kwa miezi mingi. Hata hivyo, wanasema kwamba hisia za wagonjwa fulani hubadilika haraka-haraka mara kadhaa kwa mwaka. Hisia za wagonjwa wachache hubadilika-badilika katika kipindi cha saa 24.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Ni mara chache tu ambapo wagonjwa wenye hisia zinazobadilika-badilika huishi maisha ya kawaida.”—GLORIA

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

Dalili za Kushuka Moyo Sana *

Kushuka moyo siku nzima, karibu kila siku kwa angalau majuma mawili

Kutopendezwa na shughuli zilizopendeza hapo awali

Kupunguza au kuongeza uzito sana

Kulala sana au kukosa usingizi kwa ukawaida

Kufanya mambo haraka-haraka au polepole sana

Kuchoka sana bila sababu

Kuhisi hufai au mwenye hatia, au yote mawili

Kushindwa kukaza fikira

Kufikiria kujiua mara nyingi

Baadhi ya dalili hizi huenda pia zikawa dalili za dysthymia—ugonjwa wa kushuka moyo kidogo lakini kwa muda mrefu

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 31 Orodha hii inaonyesha tu baadhi ya dalili za kushuka moyo na haipasi kutumiwa kubainisha ugonjwa wa kushuka moyo. Nyingine huenda zikawa dalili za matatizo mengine mbali na ugonjwa wa kushuka moyo.