Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukabiliana na Magumu ya Eneo la Pekee

Kukabiliana na Magumu ya Eneo la Pekee

Kukabiliana na Magumu ya Eneo la Pekee

KWA makumi ya miaka, Mashahidi wa Yehova wamehubiri katika maeneo ya Wanavajo yaliyoko katika sehemu fulani za Arizona, New Mexico, na Utah, Marekani. Katika Kinavajo, maeneo hayo yanaitwa Diné Bikéyah (nchi ya Wanavajo). Kuna Wahindi-Wamarekani zaidi ya 220,000 huko, wanaoitwa Diné (watu) katika lugha hiyo. Hivyo, hilo ni mojawapo ya makabila makubwa ya Wahindi wa Amerika Kaskazini.

Katika miaka hiyo, makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yenye wanaume na wanawake Wanavajo ambao wanapendezwa na Biblia yalianzishwa. Kwa sasa, kuna makutaniko manne katika eneo hilo—Tuba City, Kayenta, Keams Canyon, na Chinle. (Ona ramani chini.) Mpaka hivi majuzi, makutaniko yote yalikuwa na Jumba la Ufalme isipokuwa tu kutaniko la Chinle, ambalo lilikuwa linakutana kwenye shule. Lakini sasa mambo yamebadilika.

Jumba la Ufalme Katika Eneo la Pekee

Mnamo Jumamosi, Juni 7, 2003, Jumba la Ufalme la Chinle liliwekwa wakfu. Hotuba ya wakfu ilitolewa na Gerrit Lösch, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Alizungumza juu ya ongezeko kubwa la Majumba ya Ufalme ulimwenguni pote na kusema kwamba bado maelfu ya majumba mengine yanahitajiwa kwa ajili ya yale makutaniko zaidi ya 94,600. Pia aliwaeleza wahudhuriaji 165 waliokuwapo sababu 15 za kuthamini jumba lao jipya na faida za kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. Alimalizia kwa sala ya wakfu, akimwomba Yehova abariki matumizi ya jumba hilo maridadi.

Zamani, kabla kutaniko hilo halijaanzishwa, lilikuwa kikundi cha Kutaniko la Keams Canyon, lililo umbali wa kilometa 100 hivi kusini-magharibi. Sasa Kutaniko la Chinle lina jukumu la kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu katika eneo lenye ukubwa wa zaidi ya kilometa 11,000 za mraba! Wanavajo wengi huishi katika nyumba zinazoweza kuhamishwa zenye umbo la pembe sita au pembe nane. Gari linalokwenda kwa magurudumu yote manne linahitajiwa ili kuyafikia maeneo ya mbali, kama korongo la kupendeza la Canyon de Chelly (linatamkwa d’Shay).

Eneo la Canyon de Chelly Ni Takatifu kwa Wanavajo

Nyanda za juu za Arizona zina mandhari za kupendeza na barabara ndefu zilizo tambarare. Korongo la Canyon de Chelly liko kilometa chache kutoka kwenye barabara ya Jumba la Ufalme. Korongo hilo hujipinda-pinda kwa kilometa 40 kupitia majabali ya mawe mekundu ambayo yanaanza kwenye urefu wa meta 9 na kufikia meta 300. Eneo hilo ni ishara ya kitaifa na maelfu ya wageni hulitembelea kila mwaka. Korongo hilo, na lile linaloitwa Canyon del Muerto, ni takatifu kwa Wanavajo. Familia kadhaa huishi huko katika nyumba zilizoundwa kwa magogo na udongo. Lakini, Mashahidi wa Yehova hufika huko pia na kuwapelekea vitabu vya Biblia katika lugha yao.

Ili kuingia katika korongo hilo, ni lazima mtu aandamane na Mnavajo aliyepewa ruhusa ya kuwatembeza watu. Wageni fulani hutembea, wengine hupanda farasi, lakini wengi hutumia magari yanayokwenda kwa magurudumu yote manne. Magari ya aina hiyo yanahitajiwa kwa sababu yanapitia bonde la Chinle Wash. Wanavajo wanaowatembeza watu wanajua jinsi ya kuepuka mchanga wenye maji kwani farasi au gari dogo linaweza kuzama ndani. Ni nini kinachofanya korongo la Canyon de Chelly lipendeze sana?

Mtu anaweza kufahamu historia ya korongo hilo kwa kuchunguza maandishi na michoro iliyo kwenye kuta ndefu za majabali. Wachimbaji wa vitu vya kale wanaamini kwamba makao hayo maarufu yalijengwa katika mapango ya majabali kati ya mwaka wa 350 W.K. na 1300 W.K. Huenda Magofu ya Nyumba Nyeupe ndiyo makao maarufu zaidi, na yaliitwa hivyo kwa sababu jengo moja lilikuwa na ukuta mweupe. Makao hayo yaliachwa na Anasazi (jina la Kinavajo linalomaanisha “adui wa kale”) karibu na mwaka wa 1300 W.K. Inasemekana kwamba Wanavajo waliingia katika eneo hilo katika karne ya 18.

Ukitembelea eneo la Canyon de Chelly, utapitia barabara ya Navajo Route 7. Kwenye kona iliyo karibu na Ishara ya Kitaifa, tafuta ishara inayosema “Jiihōvah Yádahalne’í bi Kingdom Hall” na “Kingdom Hall of Jehovah’s Witnesses.” Unakaribishwa kwenye jumba hilo.

[Ramani katika ukurasa wa 22]

(Ukitaka kuona picha zote, tazama gazeti lenyewe)

COLORADO

TAIFA LA WANAVAJO

ARIZONA

ISHARA YA KITAIFA YA CANYON DE CHELLY

Chinle

Kayenta

Tuba City

TAIFA LA WAHOPI

Keams Canyon

NEW MEXICO

UTAH

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wachimbaji wa vitu vya kale wanasema kwamba huenda familia kumi na mbili za Anasazi ziliishi pamoja katika majabali haya

[Picha katika ukurasa wa 24]

Nyumba ya Wanavajo

[Picha katika ukurasa wa 24]

Canyon del Muerto

[Picha katika ukurasa wa 24]

Jabali la Spider huko Canyon de Chelly