Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wengine Wanaweza Kusaidiaje?

Wengine Wanaweza Kusaidiaje?

Wengine Wanaweza Kusaidiaje?

LABDA unamjua mtu anayeugua ugonjwa wa kushuka moyo au wa hisia zinazobadilika-badilika. Ikiwa ndivyo, unawezaje kumtegemeza? D. J. Jaffe wa Shirika la Kitaifa la Wagonjwa wa Akili anashauri hivi: “Tofautisha ugonjwa na mgonjwa; chukia ugonjwa lakini umpende mgonjwa.”

Kwa sababu ya kuwa na subira na upendo, mwanamke anayeitwa Susanna alifaulu kufanya hivyo. Rafiki yake aliugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Susanna anasema: “Nyakati nyingine hata hakutaka kuniona.” Badala ya kukata tamaa, Susanna alifanya utafiti ili aufahamu ugonjwa huo. Anasema: “Sasa natambua jinsi rafiki yangu alivyoathiriwa na ugonjwa wake.” Susanna anasema kwamba kuna faida kubwa kumwelewa mgonjwa. Anasema: “Jambo hilo linaweza kukusaidia kupenda na kuthamini zaidi sifa nzuri za mgonjwa.”

Ikiwa anayeugua ni mshiriki wa familia, anahitaji kutiwa moyo sana. Mario, aliyetajwa katika makala zilizotangulia, alijifunza jambo hilo mapema. Mke wake, Lucia, ambaye pia alitajwa mapema, anaugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Mario anasema: “Mwanzoni, nilifaidika kwa kuandamana na mke wangu alipoenda kumwona daktari na kujifunza kuhusu ugonjwa huo wa ajabu ili nifahamu jambo ambalo tunakabili. Mimi na Lucia tulizungumza sana na tukashughulikia hali yoyote iliyotokea.”

Utegemezo wa Kutaniko la Kikristo

Biblia huwashauri Wakristo wote ‘waseme kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika’ na ‘kuwa wenye ustahimilivu kuelekea wote.’ (1 Wathesalonike 5:14) Unawezaje kufanya hivyo? Kwanza, ni muhimu kuelewa tofauti kati ya ugonjwa wa akili na wa kiroho. Kwa mfano, mwandikaji wa Biblia Yakobo alisema kwamba sala inaweza kumsaidia mtu mwenye ugonjwa wa kiroho apone. (Yakobo 5:14, 15) Hata hivyo, Yesu alisema kwamba wale wenye matatizo ya kimwili wanahitaji daktari. (Mathayo 9:12) Bila shaka, inafaa sikuzote kusali kwa Yehova kuhusu matatizo yoyote, kutia ndani ya afya. (Zaburi 55:22; Wafilipi 4:6, 7) Lakini, Biblia haisemi kwamba matatizo ya kiafya yanaweza kusuluhishwa tu kwa kuongeza utendaji wa kiroho.

Hivyo, Wakristo wenye utambuzi huepuka kudokeza kwamba watu walioshuka moyo wamejiletea matatizo. Matamshi kama hayo ni kama yale ya watu waliodai kumfariji Ayubu lakini hawakumsaidia. (Ayubu 8:1-6) Ukweli ni kwamba mara nyingi ugonjwa wa kushuka moyo hauwezi kupona bila matibabu, hasa ikiwa mgonjwa ameshuka moyo sana na hata anataka kujiua. Katika hali kama hizo, daktari anahitajika.

Isitoshe, kuna mambo ambayo Wakristo wenzetu wanaweza kufanya ili kusaidia. Bila shaka, subira inahitajiwa. Kwa mfano, shughuli fulani za Kikristo zinaweza kuwashinda watu wenye magonjwa ya kihisia. Diane, mwenye hisia zinazobadilika-badilika, anasema: “Ni vigumu kwangu kuhubiri. Ni vigumu kuwapelekea wengine habari njema zenye furaha kutoka kwa Biblia nikiwa sijisikii vizuri na sina furaha.”

Ili uwasaidie wagonjwa hao, jitahidi kuwa mwenye huruma. (1 Wakorintho 10:24; Wafilipi 2:4) Jaribu kuona mambo kama mgonjwa anavyoyaona. Usimlemee mgonjwa kwa kumtarajia afanye mengi. Carl, ambaye ameshuka moyo, anasema: “Watu wasipotarajia mengi kutoka kwangu, pole kwa pole mimi huanza kujiheshimu. Kwa msaada wa marafiki wenye umri mkubwa nimeweza kujenga uhusiano wa karibu na Mungu na nimepata furaha nyingi sana kwa kuwasaidia wengine wafanye hivyo.”

Wagonjwa wanaweza kupata kitulizo kikubwa wakisaidiwa. Fikiria mfano wa mwanamke Mkristo anayeitwa Brenda ambaye pia ana ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Anasema: “Marafiki wangu kutanikoni wamenisaidia na kunijali ninaposhuka moyo badala ya kunishutumu kuwa dhaifu kiroho. Mara nyingi wameniruhusu tuandamane kwenye utumishi na kuacha nisikilize tu au kunihifadhia kiti kwenye Jumba la Ufalme ili niingie wakati ambapo watu wote wameketi.”

Cherie, ambaye ameshuka moyo na alitajwa katika makala iliyotangulia, pia amesaidiwa sana na wazee wa kutaniko wenye upendo na wanaojali. Anasema: “Wazee hunihakikishia kwamba Yehova ananipenda na hunisomea Neno la Mungu, Biblia, na kunieleza juu ya kusudi la Yehova la kuleta paradiso yenye amani na afya bora. Wanaposali nami hata kwenye simu, mimi hujihisi vizuri. Ninajua kwamba Yehova na ndugu zangu hawajanitupa na hilo huniimarisha.”

Hakuna shaka kwamba watu wa familia na marafiki wanaweza kumsaidia sana mgonjwa ajihisi vizuri. Lucia anasema: “Sasa naona ninaweza kudhibiti maisha yangu. Mimi na mume wangu tumejitahidi kukabiliana na hali hiyo, na sasa hali ni afadhali sana.”

Wengi ambao wamepambana na magonjwa ya akili wametambua kwamba hilo ni pambano la muda mrefu. Hata hivyo, Biblia inaahidi kwamba katika ulimwengu mpya wa Mungu, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) Hakutakuwa na magonjwa yenye kutaabisha ambayo yanawakumba watu wengi leo. Inachangamsha moyo sana kufikiria ahadi ya Mungu ya ulimwengu mpya ambapo magonjwa yote, kutia ndani ya kihisia, yatatokomea kabisa. Biblia inasema kwamba wakati huo hakutakuwa maombolezo wala kilio wala maumivu.—Ufunuo 21:4.

[Blabu katika ukurasa wa 12]

Yesu alisema kwamba wagonjwa wanahitaji daktari.—MATHAYO 9:12

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Biblia inaahidi kwamba katika ulimwengu mpya wa Mungu, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—ISAYA 33:24