Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maoni ya Biblia

Je, Amani ya Ulimwengu Itapatikana kwa Mapatano?

Je, Amani ya Ulimwengu Itapatikana kwa Mapatano?

JE, UNGEPENDA kuona vita vikikomeshwa? Ama kwa hakika, migogoro ya kitaifa na ya kimataifa inaweza kusuluhishwa kwa mapatano. Wengi wanaona kwamba ikiwa viongozi wa ulimwengu wangeshirikiana, vita vingekomeshwa. Hata hivyo, huenda umekatishwa tamaa na matokeo ya jitihada za kupatana. Kwa karne nyingi, mabalozi wametia sahihi mikataba, wameidhinisha maazimio, na kufanya makongamano, lakini matatizo mengi hayajasuluhishwa.

Biblia inazungumzia sana mapatano na amani. Inajibu maswali haya: Ni mambo gani kwa sasa yanayozuia mapatano yasilete amani? Je, Wakristo wanapaswa kujihusisha na shughuli za kibalozi? Amani ya kweli itapatikanaje hatimaye?

Ni Nini Kinachofanya Kusiwe na Amani?

Masimulizi kadhaa ya Biblia huonyesha jinsi mazungumzo ya ana kwa ana yanavyoweza kuleta amani. Kwa mfano, Abigaili alimsadikisha Daudi na jeshi lake kwa busara asilipize kisasi watu wa nyumba yake. (1 Samweli 25:18-35) Yesu alitoa mfano wa mfalme ambaye alilazimika kuwatuma mabalozi kutafuta amani. (Luka 14:31, 32) Naam, Biblia hukubali kwamba mapatano yanaweza kusuluhisha migogoro. Basi kwa nini mara nyingi mazungumzo ya amani hayafanikiwi?

Biblia ilitabiri kwa usahihi kwamba nyakati zetu zingekuwa ngumu. Wanadamu wangekuwa “wasiotaka makubaliano yoyote” na “wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi” kwa sababu ya kuchochewa na Shetani Ibilisi. (2 Timotheo 3:3, 4; Ufunuo 12:12) Isitoshe, Yesu alitabiri kwamba mwisho wa mfumo huu wa mambo ungekuwa na “vita na habari za vita.” (Marko 13:7, 8) Ni nani anayeweza kukana kwamba mambo hayo yameongezeka sana? Basi haishangazi kwamba jitihada za kutafuta amani kati ya mataifa hazifui dafu.

Pia, fikiria jambo hili: Ijapokuwa mabalozi hujitahidi sana kukomesha mapigano, wanahangaikia hasa faida za nchi zao. Hilo ndilo kusudi la mapatano ya kisiasa. Je, Wakristo wanapaswa kujihusisha na mambo hayo?

Licha ya jitihada zao, mabalozi wa ulimwengu hawana uwezo wala njia za kuleta suluhisho la kudumu

Wakristo na Mapatano

Biblia inashauri: “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote.” (Zaburi 146:3) Hiyo inamaanisha kwamba licha ya jitihada zao, mabalozi wa ulimwengu hawana uwezo wala njia za kuleta suluhisho la kudumu.

Yesu alipokuwa mbele ya Pontio Pilato, alisema: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangepigana ili nisitiwe mikononi mwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu hautoki katika chanzo hiki.” (Yohana 18:36) Mara nyingi jitihada za kutafuta amani huathiriwa na chuki ya kitaifa na ubinafsi. Hivyo, Wakristo wa kweli hujiepusha na mapambano ya ulimwengu na jitihada zake za kujaribu kupatana.

Je, hiyo inamaanisha kwamba Wakristo hawajali na hawapendezwi na hali za ulimwengu? Je, hawajali wanadamu wanapoteseka? Sivyo ilivyo. Biblia inasema kwamba waabudu wa kweli wa Mungu ‘wanaugua na kulia’ kwa sababu ya mambo mabaya yanayofanyika duniani. (Ezekieli 9:4) Wakristo wanamtegemea Mungu tu alete amani ambayo ameahidi. Je, unafikiri amani ni kutokuwepo tu kwa vita? Bila shaka Ufalme wa Mungu utatimiza hilo. (Zaburi 46:8, 9) Lakini pia utahakikisha kwamba wakazi wote wa dunia watakuwa na usalama na hali nzuri. (Mika 4:3, 4; Ufunuo 21:3, 4) Amani kama hiyo haiwezi kupatikana kwa mapatano au kwa jitihada za majeshi ya “kudumisha amani.”

Unabii wa Biblia na matukio mbalimbali yanaonyesha waziwazi kwamba jitihada za wanadamu za kuleta amani kupitia mapatano zinakatisha tamaa tu. Lakini wale wanaomtumaini Yesu Kristo alete amani na kuunga mkono Ufalme wa Mungu watapata amani ya kweli. Isitoshe, wataifurahia milele!—Zaburi 37:11, 29.