Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kujua Jina la Mungu

Jinsi ya Kujua Jina la Mungu

Jinsi ya Kujua Jina la Mungu

MWANDISHI mmoja wa gazeti alipokea barua hii kutoka kwa msomaji: “Swali hili limenisumbua katika maisha yangu yote, na ningependa unijibu. Mungu anaitwa nani? Wayahudi wanasema kwamba jina lake halisi limesahaulika. Wakristo wanamwita Yesu. Waislamu wanamwita Allah. . . . Basi, anaitwa nani?” Gazeti hilo lilichapisha swali hilo pamoja na jibu hili: “Kulingana na mafundisho ya kale ya Kiebrania, Mungu anaweza kufanya mambo yote, hivyo hakuna jina lolote linaloweza kumfafanua. Hata hivyo, ninakuhakikishia kwamba atakujibu ukimwomba kwa heshima ukitumia jina lolote lile.”

Maoni kama hayo ya kutojali kuhusu jina la Mungu ni ya kawaida leo. Ijapokuwa wanafuata dini, watu wengi wanaoamini Biblia hawalifikirii sana jina la Mungu. Lakini Mungu huhisije kuhusu jambo hilo? Je, analiona kuwa jambo dogo?

Si Jambo Dogo

Kumbuka kwamba Biblia inataja jina la Mungu, Yehova, mara elfu kadhaa. Katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, jina la Mungu linapatikana mara 7,210! * Mungu mwenyewe ndiye aliyewaongoza waandikaji wa Biblia watumie jina lake mara nyingi hivyo. Mmoja wa waandikaji hao, mtunga-zaburi Asafu, aliandika: “Wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” (Zaburi 83:18) Daudi pia aliandika hivi katika zaburi: “Tutataja kuhusu jina la Yehova Mungu wetu.”—Zaburi 20:7.

Biblia inaonyesha kwamba Yehova Mungu huchunguza mioyo yetu ili kutambua jinsi tunavyohisi kuhusu jina lake. Mtunga-zaburi alisema: “Ikiwa tumelisahau jina la Mungu wetu, . . . je, Mungu mwenyewe hatachunguza hilo? Kwa maana yeye anajua siri za moyo.” (Zaburi 44:20, 21) Nabii Isaya aliandika: “Mpeni Yehova shukrani! Liitieni jina lake. Tangazeni matendo yake kati ya vikundi vya watu. Semeni kwamba jina lake limeinuliwa juu.”—Isaya 12:4.

Mungu mwenyewe alisema: “Watajua kwamba jina langu ni Yehova.” (Yeremia 16:21) Alisema hivi pia: “Nami hakika nitalitakasa jina langu kuu, ambalo lilikuwa likitiwa unajisi katikati ya mataifa, . . . nayo mataifa yatalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.” (Ezekieli 36:23) Baadhi ya taarifa hizo zinaonyesha wakati ambapo Yehova atakasirika na kuchukua hatua dhidi ya wale wasioliheshimu jina lake. Mungu haoni suala la jina lake kuwa jambo dogo.

Yehova Mungu Hayuko Mbali Nasi

Unawezaje kujua jina la Mungu? Inamaanisha nini kujua jina la Mungu? Biblia inajibu: “Wale wanaolijua jina lako watakutegemea.” (Zaburi 9:10) Ni wazi kwamba kujua jina la Mungu kunatia ndani mengi zaidi. Unapaswa kumtegemea. Hiyo inamaanisha kujua yeye ni Mungu wa aina gani na kujifunza kuhusu sifa zake na mawazo yake. Hilo litakuchochea umtegemee.

Kwa kusoma na kujifunza Biblia kwa bidii, utafahamu Yehova ni Mungu wa aina gani. Anaahidi kuwalinda wale wanaompenda na wanaolipenda jina lake. Mungu anasema hivi kuhusu mtu anayefanya hivyo: “Kwa sababu ameweka upendo wake juu yangu, mimi nitamwokoa pia. Nitamlinda kwa sababu amelijua jina langu. Ataniitia, nami nitamjibu. Nitakuwa pamoja naye katika taabu. Nitamwokoa na kumtukuza. Nitamshibisha kwa wingi wa siku, nami nitamfanya aone wokovu wangu.”—Zaburi 91:14-16.

Yehova Mungu ana uhusiano mzuri kama nini na wale wanaojua jina lake! Wewe pia unaweza kuwa na uhusiano kama huo. Usisite kutumia jina lake unaposali kutoka moyoni. Atakujibu kwa sababu, kama Biblia inavyosema, “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.”—Matendo 17:27.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova, inatumia lugha ya kisasa badala ya maneno ya kikale yanayotumiwa na tafsiri za kale. Jambo la pekee zaidi kuhusu tafsiri hiyo ni kurudishwa kwa jina la Mungu mahali linapopatikana katika maandishi ya Biblia. Kufikia sasa, nakala zaidi ya milioni 122 zimechapishwa katika lugha 45 zikiwa nzima au sehemu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

Mungu Anajua Jina Lako

Mungu alimwambia Musa hivi: “Ninakujua wewe kwa jina.” (Kutoka 33:12) Simulizi linalojulikana vizuri la mti unaowaka moto linathibitisha jambo hilo. Biblia inasema kwamba Mungu ‘alimwita mara moja toka katikati ya ule mti wa miiba na kusema: “Musa! Musa!”’ (Kutoka 3:4) Hiyo ni pindi moja tu kati ya pindi nyingi ambazo Mungu aliwaita watu kwa majina yao. Ni wazi kwamba Muumba wa ulimwengu anapendezwa nasi kibinafsi.

Biblia inasema kwamba Mungu anajua jina la kila moja ya mabilioni ya nyota. (Isaya 40:26) Basi, si ni zaidi kwamba anawajali wanadamu wanaomwabudu! Mtume Paulo aliandika kwamba “Yehova anawajua walio wake.” (2 Timotheo 2:19) Hilo linatia ndani mengi zaidi ya kukumbuka majina. Mungu anawajua waabudu wake vizuri sana. Sisi pia tunapaswa kujua jina la Mungu na kujifunza sifa zake kwa undani.

Kitabu cha mwisho cha Biblia kinasema kuhusu kitabu cha mfano ambacho Mungu anatumia kuandika majina ya wote ambao wamemwabudu tangu jadi. Kinaitwa “kitabu cha kukunjwa cha uzima” kwa kuwa Yehova Mungu atawapa uzima wa milele wale ambao wameandikwa humo. (Ufunuo 17:8) Hilo ni tarajio zuri kama nini kwa wale wanaojua jina la Mungu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12]

Walilitangaza Jina la Mungu

Wimbo wa Musa kabla Waisraeli hawajaingia Nchi ya Ahadi: “Nitatangaza jina la Yehova.”—Kumbukumbu la Torati 32:3.

● Maneno ambayo Daudi aliliambia lile jitu Goliathi: “Mimi naja kwako nikiwa na jina la Yehova wa majeshi.”—1 Samweli 17:45.

● Maneno ya Ayubu baada ya kupoteza mali zake zote na kufiwa ghafula na watoto wake wote: “Jina la Yehova na liendelee kubarikiwa.”—Ayubu 1:21.

● Mtume Petro akinukuu Maandiko ya Kiebrania katika hotuba: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.”—Matendo 2:21.

● Nabii Isaya: “Mpeni Yehova shukrani! Liitieni jina lake. . . . Semeni kwamba jina lake limeinuliwa juu.”—Isaya 12:4.

● Yesu Kristo akiwafundisha wanafunzi wake kusali: “Basi, ninyi msali hivi: ‘Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.’”—Mathayo 6:9, 10.

● Yesu Kristo akisali kwa Mungu: “Nimelifunua jina lako.”—Yohana 17:6.

● Mungu akizungumza na watu wake: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu; nami sitampa mwingine yeyote utukufu wangu mwenyewe.”—Isaya 42:8.