Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jitihada za Kupinga Jina la Mungu

Jitihada za Kupinga Jina la Mungu

Jitihada za Kupinga Jina la Mungu

KULIKUWA na mtu anayeitwa Hananiah ben Teradion. Alikuwa msomi Myahudi wa karne ya pili W.K., naye alijulikana kwa kufanya mikutano ya hadhara ambapo alifundisha kutoka kwenye hati ya kukunja inayoitwa Sefer Torah, yenye vitabu vitano vya kwanza vya Biblia. Ben Teradion alijulikana pia kwa kutumia jina la Mungu na kuwafundisha wengine jina hilo. Kwa kuwa jina la Mungu linapatikana zaidi ya mara 1,800 katika vitabu vitano vya kwanza vya Biblia, angewezaje kufundisha Torah bila kufundisha jina la Mungu?

Hata hivyo, siku za Ben Teradion zilikuwa hatari kwa wasomi Wayahudi. Kulingana na wanahistoria Wayahudi, maliki Mroma alipiga marufuku kufundisha au kufuata dini ya Kiyahudi, na mtu ambaye angekiuka sheria hiyo angehukumiwa kifo. Mwishowe, Waroma walimkamata Ben Teradion. Alipokamatwa alikuwa ameshika nakala ya Sefer Torah. Alipokuwa akiwajibu washitaki wake, alikubali waziwazi kwamba kwa kufundisha Biblia, alikuwa akitii amri ya Mungu. Hata hivyo, alihukumiwa kifo.

Alipokuwa akiuawa, Ben Teradion alifungwa kwa hati ileile ya Biblia aliyokamatwa nayo. Kisha akachomwa juu ya mti. Kitabu Encyclopaedia Judaica kinasema kwamba “ili wamzidishie maumivu, waliweka sufu zilizotiwa ndani ya maji juu ya moyo wake ili asife haraka.” Pia, mke wake aliuawa na binti yake akauzwa kwenye nyumba ya makahaba.

Ingawa Waroma walihusika katika mauaji hayo ya unyama ya Ben Teradion, Talmud * inasema kwamba “alichomwa kwa sababu alitamka Jina la Mungu kwa ukamili.” Naam, Wayahudi waliona kutamka jina la Mungu kuwa dhambi nzito sana.

Amri ya Tatu

Inasemekana kwamba katika karne ya kwanza na ya pili W.K., Wayahudi walianza kuwa na maoni ya ushirikina kuhusu kutumia jina la Mungu. Mishnah (mkusanyo wa maandishi ya marabi ambayo baadaye yalikuwa msingi wa Talmud) inasema kwamba “mtu anayetamka jina la Mungu kama linavyoandikwa,” hataingia katika dunia Paradiso ya wakati ujao iliyoahidiwa na Mungu.

Sheria hiyo ilitoka wapi? Wengine wanasema kwamba Wayahudi waliona jina la Mungu kuwa takatifu sana hivi kwamba wanadamu wasiokamilika hawakupaswa kulitamka. Hatimaye, hata waliogopa kuliandika. Kulingana na kitabu kimoja, waliogopa kwamba jina la Mungu lingechafuliwa wakati ambapo kitabu chenye jina hilo kingetupwa kwenye pipa.

Kitabu Encyclopaedia Judaica kinasema kwamba “watu waliepuka kutamka jina YHWH . . . kwa sababu ya kutoelewa Amri ya Tatu.” Amri ya tatu kati ya zile Amri Kumi ambazo Waisraeli walipewa na Mungu inasema: “Usilitumie jina la Yehova Mungu wako kwa njia isiyofaa, kwa maana Yehova hatamwacha bila kuadhibiwa yule anayelitumia jina lake kwa njia isiyofaa.” (Kutoka 20:7) Hivyo, amri ya Mungu iliyokataza jina la Mungu lisitumiwe kwa njia isiyofaa, ilipotoshwa na ikawa ushirikina.

Ama kwa hakika, hakuna yeyote leo anayedai kwamba Mungu angependa watu wachomwe kwa sababu ya kutamka jina Lake! Hata hivyo, watu wangali wanafuata maoni ya Wayahudi ya ushirikina kuhusu jina la Mungu. Wengi bado wanasema kwamba Tetragramatoni ni “Jina Lisilotamkika.” Watu wengine hutamka vibaya majina yote yanayomwakilisha Mungu kimakusudi ili wasivunje desturi hiyo. Kwa mfano Yah, ufupisho wa jina la Mungu, hutamkwa Kah. Haleluya hutamkwa Haleluka. Hata wengine huepuka kuandika jina “Mungu,” na badala yake hutumia kistari kuwakilisha herufi moja au zaidi. Kwa mfano, wanapotaka kuandika neno la Kiswahili “Mungu,” wao huandika “M-ngu.”

Jitihada Zaidi za Kuficha Jina Hilo

Mbali na Dini ya Kiyahudi, dini nyingine pia zimeepuka kutumia jina la Mungu. Fikiria mfano wa Jerome, kasisi Mkatoliki na mwandishi wa Papa Damasus wa Kwanza. Katika mwaka wa 405 W.K., Jerome alikamilisha tafsiri yake ya Biblia nzima katika Kilatini, ambayo baadaye iliitwa Vulgate ya Kilatini. Jerome hakuweka jina la Mungu katika tafsiri yake. Badala yake, akifuata desturi ya wakati huo, alitumia maneno “Bwana” na “Mungu” badala ya jina la Mungu. Tafsiri ya Vulgate ya Kilatini ikawa Biblia ya kwanza ya Kikatoliki, na tafsiri nyingi za lugha nyingine zikatafsiriwa kutokana nayo.

Kwa mfano, Douay Version, ambayo ni Biblia ya Kikatoliki ya mwaka wa 1610, ilitafsiriwa katika Kiingereza kutokana na tafsiri ya Kilatini ya Vulgate. Basi haishangazi kwamba Biblia hiyo haina jina la Mungu hata kidogo. Hata hivyo, Douay Version ilionwa kuwa tafsiri muhimu ya Biblia. Ilikuwa tafsiri pekee iliyotumiwa na Wakatoliki wanaozungumza Kiingereza mpaka miaka ya 1940. Naam, kwa mamia ya miaka, mamilioni ya Wakatoliki walifichwa jina la Mungu.

Fikiria pia tafsiri ya King James Version. Katika mwaka wa 1604, mfalme wa Uingereza, James wa Kwanza, aliamuru kikundi cha wasomi watafsiri Biblia katika Kiingereza. Miaka saba hivi baadaye, walitoa tafsiri ya King James Version, ambayo pia huitwa Authorized Version.

Katika Biblia hiyo pia, watafsiri waliepuka kutumia jina la Mungu, isipokuwa katika mistari michache tu. Katika sehemu nyingi, walitumia neno “BWANA” au “MUNGU” kuwakilisha Tetragramatoni badala ya kutumia jina la Mungu. Tafsiri hiyo ilitumiwa na mamilioni ya watu. Kitabu World Book Encyclopedia kinasema kwamba “hakuna tafsiri nyingine muhimu za Biblia zilizotokezwa katika Kiingereza zaidi ya miaka 200 baada ya King James Version kuchapishwa. Wakati huo, King James Version ilikuwa tafsiri iliyotumiwa zaidi na watu wanaozungumza Kiingereza.”

Hiyo ni mifano mitatu tu ya tafsiri nyingi za Biblia zilizochapishwa katika karne zilizopita ambazo zimeliondoa au kuliepuka jina la Mungu. Basi si ajabu kwamba leo idadi kubwa ya watu wanaodai kuwa Wakristo hawalitumii jina la Mungu au hata hawalijui. Ni kweli kwamba baadaye watafsiri wa Biblia walitumia jina la Mungu katika tafsiri zao. Hata hivyo, tafsiri nyingi kati ya hizo zimechapishwa hivi majuzi na hazijabadili sana maoni ya watu wengi kuhusu jina la Mungu.

Zoea Linalopingana na Mapenzi ya Mungu

Watu wengi huepuka kutumia jina la Mungu kwa sababu ya desturi za wanadamu bali si mafundisho ya Biblia. Mtafiti Myahudi Tracey R. Rich, mwandishi wa kituo cha Judaism 101 cha Internet, anasema: “Hakuna chochote katika Torah kinachomkataza mtu kutamka Jina la Mungu. Maandiko yanaonyesha wazi kwamba Jina la Mungu lilitamkwa mara nyingi.” Naam, katika nyakati za Biblia waabudu wa Mungu walitumia jina lake.

Ama kweli, kujua jina la Mungu na kulitumia hutusaidia kupata njia inayokubalika ya kumwabudu kama ilivyokuwa katika nyakati za Biblia. Hiyo inaweza kuwa hatua yetu ya kwanza ya kusitawisha uhusiano wa kibinafsi pamoja naye, jambo ambalo ni muhimu zaidi ya kujua tu jina lake. Yehova Mungu anatualika tuwe na uhusiano kama huo pamoja naye. Aliongoza mwaliko huu mchangamfu uandikwe: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Hata hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Mtu awezaye kufa anawezaje kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu Mweza-Yote?’ Makala inayofuata inaeleza jinsi unavyoweza kusitawisha uhusiano pamoja na Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Talmud ni kitabu cha desturi za kale za Kiyahudi na huonwa kuwa mojawapo ya maandishi matakatifu zaidi na maarufu ya dini ya Kiyahudi.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Haleluya

Wewe hukumbuka nini unaposikia neno “Haleluya”? Labda linakukumbusha muziki wa kipekee wa Handel unaoitwa “Messiah,” wa miaka ya 1700 wenye korasi ya kuvutia ya Haleluya. Au huenda ukafikiria juu ya wimbo maarufu wa kizalendo wa Marekani unaoitwa “The Battle Hymn of the Republic,” au “Glory, Hallelujah.” Hapana shaka kwamba umesikia neno “Haleluya” wakati fulani au mahali fulani. Huenda hata wewe hulitumia mara kwa mara. Lakini je, unajua maana yake?

Haleluya—Hii ni tafsiri ya Kiswahili ya neno la Kiebrania ha·lelu-Yahʹ, linalomaanisha “msifu Yah,” au “msifuni Yah.”

Yah—Huu ni ufupisho wa kishairi wa jina la Mungu, Yehova. Jina hilo linapatikana zaidi ya mara 50 katika Biblia, hasa katika neno “Haleluya.”

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

Je, Jina Lako Linahusiana na Jina la Mungu?

Watu wengi leo wanaitwa majina ya Biblia. Katika Kiebrania cha awali, baadhi ya majina hayo yalitia ndani jina la Mungu. Ifuatayo ni mifano michache ya majina hayo na maana yake. Huenda jina lako ni mojawapo ya majina hayo.

Yoana—“Yehova Amekuwa Mwenye Neema”

Yoeli—“Yehova Ni Mungu”

Yohana—“Yehova Ameonyesha Kibali”

Yonathani—“Yehova Ametoa”

Yosefu—“Yah na Aongeze” *

Yoshua—“Yehova Ni Wokovu”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 34 “Yah” ni ufupisho wa jina “Yehova.”

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

Majina Yanayomwakilisha Mungu Katika Biblia

Maandishi ya Kiebrania ya Maandiko Matakatifu hutumia majina mengi kumwakilisha Mungu, kama vile Mweza-Yote, Muumba, Baba, na Bwana. Hata hivyo, jina lake linapatikana mara nyingi zaidi kuliko majina hayo yote yakijumlishwa. Basi ni wazi kwamba Mungu anataka tutumie jina lake. Fikiria orodha ifuatayo ya majina yanayomwakilisha ambayo yanapatikana katika Maandiko ya Kiebrania. *

Yehova—mara 6,973

Mungu—mara 2,605

Mweza-Yote—mara 48

Bwana—mara 40

Mfanyizaji—mara 12

Muumba—mara 8

Baba—mara 7

Mzee wa Siku—mara 3

Mfundishaji Mkuu—mara 2

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 40 Idadi iliyokadiriwa ya maneno hayo kama yanavyopatikana katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Mungu Anayetimiza Mambo

Wasomi hawakubaliani kuhusu maana ya jina la Mungu, Yehova. Hata hivyo, baada ya kufanya utafiti mwingi kuhusu jambo hilo, wengi wanaamini kwamba jina hilo ni namna ya kitenzi cha Kiebrania ha·wahʹ (kuwa), kinachomaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.”

Hivyo katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, * simulizi la Kutoka 3:14, ambapo Musa alimuuliza Mungu jina lake, limetafsiriwa hivi: “Ndipo Mungu akamwambia Musa: ‘Nitakuwa kile nitakachokuwa.’ Naye akaongeza kusema: ‘Hivi ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli, “Nitakuwa amenituma kwenu.”’”

Tafsiri hiyo inafaa kwa sababu Mungu anaweza kujifanya kuwa chochote anachotaka kuwa. Hakuna kitu kinachoweza kumzuia kufanya chochote ili atimize mapenzi yake. Makusudi yake na ahadi zake hutimia sikuzote. Kwa njia yenye kutokeza, Mungu akawa Muumba, aliye na uwezo usio na mipaka wa kutimiza mambo. Aliumba ulimwengu. Pia, aliumba makumi ya maelfu ya viumbe wa roho. Ama kweli, yeye ni Mungu anayetimiza mambo!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 55 Iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Mchongo unaoonyesha Hananiah ben Teradion akiuawa

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Sehemu Ambazo Jina la Mungu Limeonyeshwa Waziwazi

1. Kanisa moja huko Lomborg, Denmark, karne ya 17

2. Dirisha la kanisa la Bern, Uswisi

3. Kitabu cha Kukunjwa cha Bahari ya Chumvi katika maandishi ya kale ya Kiebrania, Israel, karibu mwaka wa 30-50 W.K.

[Hisani]

Shrine of the Book, Israel Museum, Jerusalem

4. Sarafu ya Sweden, mwaka wa 1600

[Hisani]

Kungl. Myntkabinettet, Sveriges Ekonomiska Museum

5. Kitabu cha sala cha Ujerumani, mwaka wa 1770

[Hisani]

From the book Die Lust der Heiligen an Jehova. Oder: Gebaet-Buch, 1770

6. Maandishi kwenye jiwe, Bavaria, Ujerumani

7. Jiwe la Moabu, Paris, Ufaransa, mwaka wa 830 K.W.K.

[Hisani]

Musée du Louvre, Paris

8. Mchoro kwenye kuba ya kanisa, Olten, Uswisi