Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Naamini Biblia? Mwanasayansi wa Nyuklia Aeleza

Kwa Nini Naamini Biblia? Mwanasayansi wa Nyuklia Aeleza

Kwa Nini Naamini Biblia? Mwanasayansi wa Nyuklia Aeleza

SIMULIZI LA ALTON WILLIAMS

MNAMO mwaka wa 1978, kulikuwa na matukio mawili muhimu maishani mwangu. Katika Septemba, nilipata shahada ya fizikia ya nyuklia, na katika Desemba nikawekwa rasmi kuwa mhudumu wa Mashahidi wa Yehova.

Watu wanaposikia kwamba mimi ni mwanasayansi na vilevile Shahidi, wao hushindwa kuelewa jinsi ambavyo mimi hupatanisha ujuzi wangu wa kisayansi na imani katika Biblia. Ni kweli kwamba kwa miaka mingi hata mimi sikuamini kwamba ujuzi wa kisayansi na imani katika Biblia zinaweza kupatana. Hata hivyo, baadaye nilisadiki kabisa kwamba Biblia inapatana na sayansi. Nilifikiaje uamuzi huo? Hebu kwanza nisimulie jinsi nilivyopata kuwa mwanasayansi.

Mradi wa Miaka 19

Nilizaliwa mwaka wa 1953 huko Jackson, Mississippi, Marekani, nikiwa mtoto wa tatu kati ya 11. Familia yetu ilikuwa maskini. Mara nyingi ilitubidi kuhamahama kwa sababu wazazi wangu hawangeweza kulipa kodi. Tulinunua chakula tukitumia pesa zilizotoka kwa mradi wa serikali wa kusaidia maskini, na tulipewa mavazi makuukuu na watu ambao mama yangu aliwasafishia nyumba na ofisi.

Mara nyingi wazazi wetu walitueleza kwamba tungeweza tu kuepuka umaskini kwa kupata elimu ya kutosha. Hivyo, nikiwa mdogo sana, niliamua kusomea shahada ya chuo kikuu. Nilianza shule nilipokuwa na umri wa miaka sita, nikaendelea kwa miaka 19 bila kuacha. Nilipenda sayansi na hesabu, kwa hiyo nilipoingia chuo kikuu nilianza kusomea sayansi.

Nilipokuwa huko, nilikutana na msichana anayeitwa Del. Alielekezwa kwangu na profesa wa sayansi ili nimsaidie katika somo la sayansi alilokuwa akisomea. Hata hivyo, hatukuzungumza tu kuhusu sayansi kwani baada ya muda tulianza kupendana. Tulioana Januari 10, 1974—katika kipindi cha saa mbili cha mapumziko kati ya masomo! Miaka minne baadaye, katika mwaka wa 1978, nilipata shahada ya tatu.

Nilitimiza kile ambacho nilidhani kingefanikisha maisha yangu. Nilikuwa mwanasayansi, na hasa mwanafizikia wa nyuklia! Nikiwa na shahada ya fizikia ya nyuklia, ningeanza kuchuma mazao ya jasho langu. Nilitaka sana kujifanyia jina katika nyanja ya sayansi. Isitoshe, sasa ningechagua kazi ya mshahara mnono katika mojawapo ya makampuni ya kibinafsi na ya serikali.

Hata hivyo, miezi michache baadaye, katika Desemba 30, 1978, nilichukua hatua ambayo baadaye ingebadili maisha yangu na wakati wangu ujao kuliko shahada yangu. Siku hiyo, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova Mungu kwa kubatizwa ndani ya maji, nikawa Shahidi wa Yehova. Nilifikiaje hatua hiyo?

Kitabu Kilichonipendeza

Mwishoni mwa mwaka wa 1977, nilipokuwa katika Chuo Kikuu cha Massachusetts huko Amherst, Mashahidi wawili walibisha mlango wa nyumba yetu. Hawakunikuta nyumbani, lakini walimkuta mke wangu na watoto wetu wawili, mmoja wa miaka mitatu na mwingine aliyezaliwa karibuni. Del aliwakaribisha Mashahidi hao. Baada ya mazungumzo mazuri pamoja nao, alikubali Mashahidi wamtembelee mara moja kwa juma ili wamfundishe Biblia.

Mke wangu aliponieleza jambo hilo, mara moja nilimpinga. Nilimruhusu ajiunge na dini nyingine yoyote, lakini si Mashahidi wa Yehova! Kwa kweli, sikujua mengi kuhusu Mashahidi, lakini niliwaelewa kimakosa kwamba wao ni kikundi cha ajabu ambacho kinatumia Biblia kuwadanganya watu. Hivyo, nilikusudia kutumia ujuzi wangu wa kisayansi kupinga mafundisho yao ili wasimnase mke wangu.

Nilichukua likizo kwa juma moja ili nihudhurie funzo la Biblia la mke wangu. Hata hivyo, nilichelewa kuwasili nyumbani na mwanamke aliyemfundisha alikuwa karibu kuondoka. Alinipa kitabu chenye kichwa Did Man Get Here by Evolution or by Creation? * Pia, alimwambia mke wangu kwamba kwenye funzo la Biblia juma linalofuata, wangechunguza unabii wa Biblia unaoonyesha kwamba mwaka wa 1914 ni muhimu. Hiyo ndiyo fursa niliyotaka! Nilimwambia Shahidi huyo kwamba ningekuwa nyumbani wakati wa mazungumzo hayo ya Biblia. Nilitaka kuhakikisha usahihi wa hesabu alizotumia kuzungumzia mwaka wa 1914.

Usiku huohuo, nilianza kukisoma kitabu nilichoachiwa na Shahidi huyo. Kusema kweli, nilipendezwa na mambo niliyosoma. Kiliandikwa kwa utaratibu mzuri, na kilikuwa na marejeo mengi ya kisayansi kuhusu mageuzi. Nilishangaa kujua kwamba Biblia ina habari sahihi kuhusu uumbaji kuliko nilivyofikiri. Siku chache baadaye, nilikimaliza na nililazimika kukubali kwamba yale ambayo Biblia inasema kuhusu uumbaji hayapingani na mambo yanayojulikana kuhusu uhai duniani.

Niliazimia Kupata Mafundisho Yanayopingana

Hata hivyo, bado nilishuku mafundisho ya Mashahidi, na nilitazamia kuchunguza hesabu ya unabii wa Biblia kuhusu mwaka wa 1914. Nilidhani kwamba kwa njia hiyo ningemtisha Shahidi huyo na huenda ningemsaidia mke wangu kuona kasoro katika mafundisho ya Mashahidi.

Juma lililofuata, Shahidi huyo alirudi na mwanamume mwingine aliyekuwa mzee katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova la eneo hilo. Mzee huyo aliongoza funzo hilo la Biblia. Alizungumzia unabii unaopatikana katika sura ya 4 na ya 9 ya kitabu cha Biblia cha Danieli kuhusu kutokea kwa Yesu akiwa Mesiya na Mfalme. Nilitaka tu kupata makosa ya hesabu katika mazungumzo hayo, lakini sikupata hata moja. Badala yake, nilivutiwa na utaratibu wa habari inayopatikana katika Biblia.

Kufikia wakati huo, nilidhani kwamba imani katika Mungu inategemea hisia wala si akili. Nilikosea sana! Niliwashukuru Mashahidi hao kwa habari hiyo yenye kuarifu na kusema kwamba ningependa kuendelea kuhudhuria funzo hilo kila juma. Hivyo, kuanzia wakati huo, niliendelea na masomo yangu chuoni na pia kufundishwa na Mashahidi Biblia pamoja na mke wangu. Isitoshe, mimi na mke wangu tulianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi kwenye Jumba la Ufalme.

Baada ya miezi michache tu, nilijifunza kweli nyingi za Biblia, na muda si muda nikajiunga na Mashahidi kuhubiri nyumba kwa nyumba. Nilifanya mambo hayo nilipokuwa bado kwenye hatua za mwisho-mwisho za kusomea shahada yangu ya tatu chuoni, ambayo ilimaliza muda wangu mwingi. Nilimaliza ripoti yangu ya mwisho katika majira ya kiangazi ya mwaka wa 1978 na kuhamia jimbo la Alabama, ambako nilianza kufunza fizikia katika Chuo Kikuu cha Alabama A. & M. huko Huntsville. Tuliwasiliana na Mashahidi wa huko upesi na mzee mmoja na mke wake wakaja kutufundisha Biblia. Miezi michache baadaye, mimi na mke wangu tukabatizwa siku ileile.

Kuwa Mwanasayansi na Mhudumu

Sijaona ugumu wa kuwa mwanasayansi na vilevile Shahidi wa Yehova. Katika mwaka wa 1983, niliajiriwa katika Kituo cha Angani cha George C. Marshall cha NASA (National Aeronautics and Space Administration), huko Huntsville. * Nilifanya majaribio na kuchunguza darubini ya eksirei. (Katika mwaka wa 1999, darubini hiyo, inayoitwa Darubini ya Chandra Eksirei, ilitumwa angani kwa kutumia chombo cha Columbia.) Nilifurahia mradi huo, ambao ulitia ndani kuchunguza eksirei zilizotokezwa na nyota na makundi ya nyota ili kuelewa anga vizuri zaidi.

Nilifurahia kazi hiyo ya kisayansi kwa sababu ilichangamsha akili na ilinisaidia nielewe zaidi nguvu na hekima ya Muumba. Nilielewa vizuri zaidi maneno ya Yehova aliyosema kupitia nabii wa kale Isaya. Muumba anasema: “Inueni macho yenu juu, mwone. Ni nani ameviumba vitu hivi? Ni Yeye anayelileta jeshi lake kulingana na hesabu, ambaye zote anaziita kwa jina. Kutokana na wingi wa nguvu zenye msukumo, yeye pia akiwa hodari katika nguvu, hakuna hata moja kati ya hizo inayokosekana.” (Isaya 40:26) Kadiri ‘nilivyoinua macho yangu juu’ na kuona anga kubwa lililo tata na maridadi, ndivyo nilivyothamini kazi ya Muumba mwenye akili ambaye aliviumba vitu hivyo vyote na kuweka sheria zinazoongoza vitu hivyo.

Wakati huo, niliendelea kuchapisha majarida ya kisayansi kuhusu uchunguzi wangu wa angani kwa kutumia eksirei. Hata hivyo, niliendelea kuwa mwenye bidii katika kutaniko la Kikristo. Nilitumikia nikiwa mzee na kutumia saa 20 kila mwezi kuhubiri. Naye mke wangu alianza kufanya kazi ya kufundisha Biblia wakati wote.

Baada ya kufanya kazi kwa miaka minne huko NASA, niliona uhitaji wa kujitolea zaidi kuwasaidia wengine wajifunze kweli za ajabu za Biblia. Ningewezaje kufanya hivyo? Baada ya kuzungumza jambo hilo na mke wangu na kusali kwa Yehova, niliona kwamba ninahitaji kufanya maamuzi fulani.

Maamuzi Mazito

Nilimwona mkubwa wangu huko NASA na kumwambia kwamba ninataka kufanya kazi kwa siku nne badala ya siku tano kwa juma. Bila shaka, mshahara wangu ungepungua. Nilimweleza kwamba nilitaka kutumia siku tatu zilizosalia katika utumishi wangu. Ingawa lilikuwa jambo jipya kwa wanasayansi wa NASA, mkubwa wangu alikubali ombi langu. Hata hivyo, aliniambia kwamba ninahitaji kuzungumza na mkubwa wake. Niliongea naye na nilifurahi alipokubali ombi langu. Hivyo, katika Septemba 1987, nilianza huduma ya wakati wote, nikaanza kutumia saa 90 kila mwezi kuhubiri nyumba kwa nyumba na kufanya utumishi mwingine.

Baadaye, msimamizi mmoja wa Chuo Kikuu cha Alabama A. & M. huko Huntsville alinipigia simu. Aliniuliza kama ningependa kufundisha katika idara ya fizikia katika chuo hicho. Nilimwambia kwamba ningefanya kazi hiyo iwapo ingeniruhusu niwe na wakati mwingi wa kuhubiri. Nilimhakikishia kwamba utumishi wangu haungeathiri kazi ya kufundisha. Alikubali. Bado ninafundisha katika chuo hicho na kuhubiri wakati wote. Hata nilipata wakati wa kujifunza Kihispania. Mimi na mke wangu tunashirikiana na kutaniko la Kihispania la Mashahidi wa Yehova la Huntsville.

Sayansi na Imani

Wakati wote ambao nimefanya utafiti wa kisayansi, sijaona kamwe kanuni za kweli za kisayansi zikipingana na mafundisho ya Biblia. Mara nyingi, Biblia huonekana kama inapingana na sayansi ikiwa mtu hana ujuzi wa kutosha kuhusu fundisho fulani la sayansi au yale ambayo Biblia inasema. Kwa mfano, wanasayansi fulani na watu wengine hufikiri kimakosa kwamba Biblia hufundisha kuwa mimea, wanyama, na wanadamu waliumbwa kwa siku sita za saa 24. Hiyo si kweli kulingana na sayansi. Hata Biblia haifundishi hivyo. Badala yake, inaonyesha kwamba “siku” za uumbaji zilikuwa maelfu ya miaka. *

Kutoelewana pia hutokea kwa sababu wengine wanafikiri kimakosa kwamba imani katika Mungu ni jambo la kihisia tu. Lakini kinyume cha hilo, imani katika Mungu na Biblia inategemea ukweli uliothibitishwa. Kama Biblia inavyosema, “imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, uthibitisho ulio wazi [au, uthibitisho wenye kusadikisha] wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Waebrania 11:1) Ndiyo, imani inategemea uthibitisho. Unabii mwingi ulitimia zamani na unatimia katika siku zetu. Hivyo, tukitumia mbinu ambayo wanasayansi wote hutumia kuthibitisha dhana za kisayansi, tunaweza kuwa na uhakika kamili kwamba unabii wa Biblia kuhusu wakati ujao utatimia.

Unabii mmoja unahusu ahadi ya kwamba tutafurahia hali nzuri katika Paradiso duniani wakati ujao ulio karibu. Madhara ya uzee, magonjwa, kifo, vita, na ukosefu wa haki hayatakuwepo. (Ufunuo 21:3, 4) Wakati huo tutapata wakati wa kuchunguza na kujifunza kinaganaga kuhusu uumbaji wa ajabu wa Yehova Mungu na sheria nyingi ambazo ameweka ili ziongoze ulimwengu wetu wa kustaajabisha.

Namshukuru Yehova Mungu kwa kunisaidia nipate njia inayoongoza kwenye furaha ya kweli, yaani, kweli za ajabu zinazopatikana katika Neno lake, Biblia. Natumaini kwamba wengi zaidi, kutia ndani wanasayansi, watapata njia hiyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini hakichapishwi tena.

^ fu. 22 NASA ni shirika la serikali ya Marekani ambalo halitegemei mashirika mengine ya serikali.

^ fu. 30 Ona sura ya 6, “Rekodi ya Kale ya Uumbaji—Je, Unaweza Kuitumaini?,” katika kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 20]

Nilidhani kwamba imani katika Mungu inategemea hisia wala si akili

[Blabu katika ukurasa wa 22]

Sijaona kamwe kanuni za kweli za kisayansi zikipingana na mafundisho ya Biblia

[Picha katika ukurasa wa 21]

Ninaruzuku familia yangu kwa kufundisha kwa siku kadhaa

[Picha katika ukurasa wa 23]

Darubini ya Chandra Eksirei ya NASA ikiwa angani na picha ya eksirei ya shimo jeusi

[Hisani]

NASA Photo

NASA/CfA/J. McClintock et al.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mimi na mke wangu tunafurahia utumishi wa wakati wote