Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Ana Jina!

Mungu Ana Jina!

Mungu Ana Jina!

Mungu anaitwa nani? Wanadamu wote wana majina. Hata wengine huwapa wanyama wao majina! Je, haifai Mungu awe na jina pia? Kwa kawaida wanadamu huwa na majina na huyatumia. Hiyo ni sehemu muhimu ya mahusiano yao. Ndivyo ilivyo pia na uhusiano wetu pamoja na Mungu. Lakini inashangaza kwamba mamilioni ya watu wanaodai kumwamini Mungu wa Biblia hawatumii jina lake. Hata hivyo, jina la Mungu limejulikana kwa karne nyingi! Unaposoma makala hizi, utaona kwamba jina la Mungu lilitumiwa sana zamani. Pia, utajifunza yale ambayo Biblia inasema kuhusu umuhimu wa kujua jina la Mungu.

KUFIKIA karne ya 17, nchi kadhaa za Ulaya zilikuwa zikitengeneza sarafu zenye jina la Mungu. Kwa mfano, sarafu ya Ujerumani iliyotengenezwa katika mwaka wa 1634 ilionyesha jina Yehova waziwazi. Sarafu hizo ziliitwa sarafu za Yehova, na zilitumiwa kwa makumi ya miaka.

Yehova * ni tafsiri ya jina la Mungu ambayo imetambuliwa kwa karne nyingi. Katika Kiebrania, ambacho husomwa kutoka kulia hadi kushoto, jina hilo huandikwa kwa konsonanti nne, יהוה. Herufi hizo nne za Kiebrania—zinazotafsiriwa kuwa YHWH—huitwa Tetragramatoni. Herufi hizo za jina la Mungu ziliandikwa pia kwenye sarafu za Ulaya kwa makumi ya miaka.

Jina la Mungu hupatikana pia kwenye majengo, sanamu za ukumbusho, sanaa, na vilevile nyimbo nyingi za kanisa. Kulingana na ensaiklopidia ya Ujerumani inayoitwa Brockhaus, wakati mmoja watawala Waprotestanti walikuwa na desturi ya kuvaa beji iliyokuwa na mchoro wa jua na Tetragramatoni. Ishara hiyo, ambayo pia ilitumiwa kwenye bendera na sarafu, iliitwa beji ya Jua-Yehova. Ni wazi kwamba wanadini wa Ulaya wa karne ya 17 na 18 walijua kwamba Mungu Mweza-Yote ana jina. Na jambo la pekee zaidi ni kwamba hawakuogopa kulitumia.

Jina la Mungu lilijulikana pia huko Amerika wakati wa ukoloni. Mfano mmoja ni wa askari aliyehusika katika Mageuzi ya Amerika, Ethan Allen. Kulingana na maandishi yake, katika mwaka wa 1775, aliwataka maadui wake wasalimu amri “kwa jina la Yehova Mkuu.” Baadaye, wakati wa utawala wa Abraham Lincoln, washauri kadhaa walitaja jina Yehova mara nyingi katika barua walizomwandikia Lincoln. Maandishi mengine ya kale ya Marekani yenye jina la Mungu yanapatikana katika maktaba nyingi za umma. Hiyo ni mifano michache inayoonyesha jinsi jina la Mungu lilivyotumiwa kwa karne nyingi.

Vipi leo? Je, jina la Mungu limesahaulika? La. Tafsiri mbalimbali za Biblia zinatumia jina la Mungu katika mistari mingi. Ukitembelea maktaba au ukichunguza kamusi utaona kwamba jina Yehova ndiyo tafsiri ya Tetragramatoni inayokubaliwa zaidi. Kwa mfano, kitabu Encyclopedia International, kinafafanua jina Yehova kuwa “tafsiri ya kisasa ya jina takatifu la Kiebrania la Mungu.” Toleo jipya la The New Encyclopædia Britannica linaeleza kwamba Yehova ni “jina la Mungu lililotokana na dini ya Kiyahudi na Ukristo.”

Huenda ukajiuliza, ‘Je, watu huona jina la Mungu kuwa muhimu leo?’ Tafsiri mbalimbali za jina la Mungu, zinapatikana katika sehemu nyingi za umma. Kwa mfano, jina Yehova limeandikwa kwenye jiwe kuu la jengo moja huko New York City. Katika jiji hilohilo, kuna mchoro maridadi wenye jina hilo katika Kiebrania kwenye stesheni ya gari-moshi la chini ya ardhi. Hata hivyo, tunaweza kusema kwamba kati ya maelfu ya watu ambao wametembelea sehemu hizo, si wengi ambao wameona umuhimu wa maandishi hayo.

Je, watu katika eneo lenu wanaona jina la Mungu kuwa muhimu? Au je, wengi wanasema kwamba jina la Muumba ni “Mungu,” kana kwamba jina hilo la cheo ndilo jina lake halisi? Huenda unaona kwamba watu wengi hawafikiri kuwa Mungu ana jina. Vipi wewe? Je, wewe huona ni sawa kumwita Mungu kwa jina lake, Yehova?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Makala hizi zimeonyesha namna 39 ambavyo jina Yehova huandikwa katika lugha zaidi ya 95.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]

Mfalme Aliyewafundisha Wengine Jina la Yehova

Mnamo mwaka wa 1852, mishonari kadhaa walisafiri kutoka Hawaii mpaka visiwa vya Micronesia. Mishonari hao walikuwa na barua ya kuwatambulisha yenye muhuri wa Mfalme Kamehameha wa Tatu, aliyetawala Visiwa vya Hawaii wakati huo. Barua hiyo, ambayo iliandikwa katika Kihawaii kwa watawala kadhaa wa Visiwa vya Pasifiki, ilisema hivi: “Kuna walimu wa Mungu Aliye Juu Zaidi, Yehova, wanaotaka kusafiri kwenye visiwa vyenu kuwatangazia Neno Lake ili mpate wokovu wa milele. . . . Nawaomba mwapokee walimu hawa wazuri na ninawasihi msikilize maagizo yao. . . . Nawashauri mtupilie mbali sanamu zenu, mmpokee Bwana Yehova awe Mungu wenu, mmwabudu na kumpenda na atawabariki na kuwaokoa.”

[Picha]

Mfalme Kamehameha wa Tatu

[Hisani]

Hawaii State Archives

[Picha katika ukurasa wa 3]

Neno Tetragramatoni linamaanisha “herufi nne,” ambazo huonyesha jina la Mungu katika Kiebrania