Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nawezaje Kupata Wakati wa Kufanya Kazi za Shule?

Nawezaje Kupata Wakati wa Kufanya Kazi za Shule?

Vijana Huuliza . . .

Nawezaje Kupata Wakati wa Kufanya Kazi za Shule?

‘Niko karibu kumaliza shule ya sekondari, na nina mfadhaiko mwingi sana. . . . Nina kazi nyingi za shule, na si mchezo. Sina wakati wa kufanya kazi hizo.’—Msichana mwenye umri wa miaka 18.

JE, WEWE huhisi umelemewa na kazi ya shule kila jioni? Ikiwa ndivyo, si wewe peke yako. Ripoti moja ya habari kutoka Marekani inasema: “Shule zote nchini zinapojitahidi kuboresha viwango vya elimu na maksi, wanafunzi wanapewa kazi nyingi. Katika sehemu fulani, wanafunzi wa shule za sekondari wanasema kwamba wanafanya kazi za shule kwa zaidi ya saa tatu kila jioni. Uchunguzi mmoja uliofanywa na Chuo Kikuu cha Michigan unaonyesha kwamba watoto wanapewa kazi za shule mara tatu zaidi kuliko ilivyokuwa miaka 20 iliyopita.”

Si nchini Marekani tu ambapo wanafunzi wana kazi nyingi za shule. Kwa mfano, ingawa asilimia 30 hivi ya wanafunzi wenye umri wa miaka 13 nchini humo walisema kwamba walifanya kazi za shule kwa zaidi ya saa mbili kila siku, idadi hiyo ilikuwa asilimia 40 huko Taiwan na Korea, na asilimia 50 nchini Ufaransa. Katie, mwanafunzi wa chuo kikuu nchini Marekani, anasema: “Nyakati nyingine mimi hufadhaika sana kazi ya shule inaporundamana.” Marilyn na Belinda, wanaosomea Marseilles, Ufaransa, wanaona hivyo pia. Marilyn anasema: “Sisi hutumia saa mbili au zaidi kila jioni kufanya kazi ya shule. Ukiwa na kazi nyingine, ni vigumu kupata wakati wa kutosha.”

Nitapataje Wakati?

Si ungefurahi ikiwa ungeweza kupata saa za ziada kila siku ili umalize kazi ya shule na kufanya mambo mengine ya lazima? Kwa kweli, unaweza kupata saa zaidi kwa kutumia kanuni ya Biblia kwenye Waefeso 5:15, 16: “Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa.” Ingawa mwandikaji huyo wa Biblia hakuwa akizungumzia kazi za shule alipoandika maneno hayo, tunaweza kutumia kanuni hiyo katika shughuli za kila siku. Unaponunua kitu, ni lazima ujinyime kitu fulani. Wazo kuu hapa ni kwamba ili upate wakati wa kujifunza, utahitaji kujinyima kitu fulani. Nini?

Kijana anayeitwa Jillian anashauri hivi: “Orodhesha mambo unayopaswa kufanya kwanza.” Hiyo inamaanisha kwamba unapaswa kujua mambo ya kutangulizwa. Mikutano ya Kikristo na mambo ya kiroho ndiyo mambo yanayopaswa kutangulizwa. Usisahau madaraka yako katika familia, kazi za nyumbani, na kazi za shule.

Halafu, jaribu kuandika jinsi unavyotumia wakati wako katika muda wa juma moja hivi. Huenda ukashangaa kuona jinsi unavyotumia wakati wako. Unatumia muda gani kutazama televisheni? kuchunguza Internet? kwenda sinema? kuzungumza kwenye simu? kutembelea marafiki? Sasa, maandishi yako yanaonyesha unatanguliza mambo gani? Labda unahitaji tu kupunguza wakati unaotumia kutazama televisheni, kupiga simu, au kuchunguza Internet ili ununue wakati mwingi!

Tanguliza Mambo Muhimu

Hiyo haimaanishi kwamba hutatazama televisheni au kujiburudisha hata kidogo. Huenda ukahitaji kutumia kanuni hii, “Tanguliza mambo muhimu.” Andiko unaloweza kutumia ni: “Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:10) Kwa mfano, kwa kuwa kazi ya shule ni muhimu, unaweza kuamua kwamba hutafungua televisheni mpaka utakapomaliza kazi za nyumbani, kutayarisha mikutano ya Kikristo, na kazi ya shule. Ni kweli kwamba huenda ukajihisi vibaya unapokosa kutazama kipindi unachopenda. Lakini, kusema kweli, ni mara ngapi ambapo umekusudia kutazama kipindi unachopenda tu lakini ukajipata unatumia jioni nzima bila kufanya jambo lingine lolote?

Kwa upande mwingine, unapaswa kuona kuhudhuria mikutano kuwa jambo muhimu. Kwa mfano, ikiwa kuna mtihani unaokuja au mgawo wa shule, unaweza kuufanya mapema ili usikuzuie kuhudhuria mikutano. Hata unaweza kuzungumzia jambo hilo na walimu wako, uwaombe wakujulishe mapema kama watatoa mgawo fulani siku ya mkutano. Huenda walimu wengine wakakubali.

Kanuni nyingine muhimu inapatikana kwenye simulizi la Biblia kuhusu rafiki ya Yesu aliyeitwa Martha. Alikuwa mwenye shughuli nyingi na bidii sana, lakini hakujua mambo ya kutanguliza. Inaonekana wakati fulani, alijichosha kwa kumtayarishia Yesu mlo mkubwa huku dada yake Maria akimsikiliza Yesu badala ya kumsaidia Martha. Martha alipolalamika kuhusu jambo hilo, Yesu alimwambia: “Martha, Martha, wewe unahangaika na kusumbuka juu ya mambo mengi. Ingawa hivyo, mambo machache ndiyo yanayohitajiwa, au moja tu. Yeye, Maria alichagua fungu jema, nalo halitaondolewa kwake.”—Luka 10:41, 42.

Tunajifunza nini? Usijishughulishe na mambo mengi. Unawezaje kutumia kanuni hiyo? Je, “unahangaika na kusumbuka juu ya mambo mengi,” ukijaribu kusawazisha kazi za shule na kazi ya muda? Je, kweli familia yenu inahitaji pesa unazopata kwa kufanya kazi hiyo? Ama unataka tu kupata pesa za ziada ili ununue vitu ambavyo huvihitaji sana?

Kwa mfano, katika nchi fulani vijana hutamani kununua magari. Mshauri wa shule ya sekondari, Karen Turner, anasema kwamba “inawabidi vijana wafanye kazi kwa sababu kudumisha gari kunagharimu pesa nyingi.” Hata hivyo, Turner anakata kauli hii: “Ni vigumu kufanya mambo mengi pamoja kama vile shughuli za baada ya shule, kazi ya kuajiriwa, na kazi nyingi za shule. Hilo humlemea mwanafunzi.” Mbona ujitaabishe bure? Ikiwa hupati wakati wa kufanya kazi zako za shule, labda inafaa upunguze saa unazotumia kufanya kazi au uiache.

‘Nunua’ Wakati Shuleni

Mbali na kutafuta wakati wa ziada baada ya shule, fikiria jinsi unavyoweza kununua wakati unapokuwa shuleni. Josue anasema: “Mimi hujaribu kufanya kazi za shule kadiri niwezavyo nikiwa shuleni. Wakati huo mimi hupata nafasi ya kumuuliza mwalimu mambo ambayo sikuelewa darasani.”

Pia unaweza kufikiria kupunguza idadi ya masomo ya ziada unayosomea. Pia, unaweza kuacha baadhi ya shughuli za baada ya shule unazofanya. Unaweza kupata wakati zaidi wa kujifunza ukifikiria mambo hayo.

Kutumia Wakati Vizuri

Haya, baada ya kujinyima na kufanya mabadiliko fulani, una wakati zaidi wa kufanya kazi za shule. Unawezaje kutumia wakati huo vizuri? Ikiwa unaweza kufanya asilimia 50 ya kazi za shule katika wakati uleule inamaanisha una asilimia 50 ya wakati wa ziada. Yafuatayo ni madokezo ya kutumia wakati wako vizuri.

Uwe na ratiba. Kabla hujaanza kufanya kazi za shule, fikiria mambo kama vile: Ni somo gani linalohitaji kutangulizwa? Somo hilo litachukua muda gani? Je, utahitaji kutumia vitabu, karatasi, kalamu, na kifaa cha kupiga hesabu?

Tafuta mahali pa kujifunzia. Panapaswa kuwa mahali ambapo huwezi kukengeushwa. Kijana anayeitwa Elyse anasema: ‘Ikiwa una dawati, litumie. Utakaza fikira vizuri zaidi ukiketi badala ya kulala kitandani.’ Ikiwa huna chumba chako binafsi, waombe ndugu na dada zako wanyamaze au wasikusumbue wakati unapojifunza ama uende kwenye maktaba ya umma au bustani. Ikiwa una chumba chako binafsi, usifungue televisheni au kucheza muziki wakati unaposoma.

Pumzika kidogo. Ukishindwa kukaza fikira baada ya muda, pumzika kidogo.

Usiahirishe mambo! Katie, aliyenukuliwa mapema anasema hivi: “Mimi huahirisha mambo kila wakati. Mimi huanza kufanya kazi ya shule dakika ya mwisho.” Panga ratiba kwa ajili ya kazi ya shule na uifuate ili uepuke kuahirisha mambo.

Ingawa kazi ya shule ni muhimu, kama Yesu alivyomwambia Martha, mambo muhimu zaidi—‘mafungu mema’—ni yale ya kiroho. Hakikisha kwamba kazi ya shule haikuzuii kufanya mambo muhimu kama vile kusoma Biblia, kushiriki katika huduma, na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Mambo hayo yataboresha maisha yako milele!—Zaburi 1:1, 2; Waebrania 10:24, 25.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ni vigumu kufanya kazi za shule ukijaribu kufanya mambo mengi sana kwa wakati uleule

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ukipanga mambo vizuri, utakuwa na wakati wa kufanya kazi za shule