Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Utu Wako Unategemea Damu Yako?

Je, Utu Wako Unategemea Damu Yako?

Maoni ya Biblia

Je, Utu Wako Unategemea Damu Yako?

KATIKA nchi fulani, watu wengi wanapenda kuamua utu wa mtu kulingana na aina yake ya damu. Kwa mfano, nchini Japan, ni kawaida kuanzisha mazungumzo kwa kuuliza hivi: “Damu yako ni aina gani?” Wale wanaoshikilia maoni hayo hudai kwamba watu wenye damu aina ya A ni watulivu, wanachukua mambo kwa uzito, na ni wenye kutia shaka; na wale wenye damu aina ya B ni wakarimu, wanapenda kukasirika, wanaweza kudanganywa kwa urahisi; na kadhalika. Pia inasemwa kwamba watu wenye aina tofauti za damu hushindwa kupatana au hupatana kwa urahisi.

Kwa kutegemea dhana hiyo, watu fulani huona damu kuwa muhimu wanapochagua wanafunzi ambao watakuwa katika darasa moja, wanapoteua wasimamizi katika makampuni, au hata kuchagua mwenzi wa ndoa. Je, kuna jambo lolote linalothibitisha kwamba damu yetu huathiri utu wetu? Je, kuna mafundisho yoyote ya Biblia yanayozungumzia jambo hilo?

Aina za Damu

Kitabu The World Book Multimedia Encyclopedia kinasema hivi: “Chembe nyekundu za damu zina protini zinazoitwa antijeni. Zaidi ya antijeni 300 za chembe nyekundu zimegunduliwa.” Ingawa watu fulani wana antijeni nyingine, wengine hawana, na antijeni nyingine haziwezi kuwa pamoja. Hivyo kitabu hicho kinaongezea kwamba “wanasayansi wamegawanya damu ya wanadamu katika aina mbalimbali kwa kutegemea kuwapo au kutokuwapo kwa antijeni fulani.”

Mfumo wa kugawanya damu unaotumiwa zaidi ni mfumo wa ABO, ambao hugawanya damu ya wanadamu katika aina nne—A, B, AB, na O. Mfumo wa Rh pia hutumiwa sana. Ama kwa hakika kuna mifumo 20 hivi ya kugawanya damu. Basi, ni wazi kwamba damu ni tata sana. Kitabu Encyclopædia Britannica kinasema hivi: “Kwa kuwa kuna antijeni nyingi tofauti za chembe nyekundu, ni vigumu sana kwa watu kuwa na damu inayofanana kabisa isipokuwa wawe mapacha wanaofanana.”

Maelezo hayo yanaonyesha kwamba kila mtu ana ‘aina tofauti ya damu.’ Basi ni kosa kudai kwamba watu wenye aina fulani ya damu wana utu unaofanana. Ni wazi kwamba utu wetu unategemea mambo mbalimbali.

Utu Wetu Unategemea Nini?

Utu ni tabia zilizorithiwa na ambazo mtu amejifunza, nazo humtofautisha na watu wengine. Naam, mbali na tabia tulizorithi, kuna mambo mengine yanayoathiri utu wetu kama vile malezi, elimu, marafiki, na hali nyingine mbaya au nzuri. Kwa hiyo, utu wetu hautegemei tu mambo tuliyorithi. Mara nyingi, hata mapacha wanaofanana, wenye chembe zilezile za urithi, wana nyutu tofauti.

Jambo jingine la maana ni kwamba utu wa mtu unaweza kubadilika au kubadilishwa. Mtume Paulo alikazia jinsi mafundisho ya Kikristo yalivyo na nguvu za kubadili watu. Aliandika hivi: “Uvueni utu wa zamani pamoja na mazoea yake, na mjivike utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba.” (Wakolosai 3:9, 10) Wakristo hutambua kwamba wao ni watenda-dhambi na wamerithi mielekeo ya kutenda dhambi. Ili wakubaliwe na Mungu, iliwabidi wabadili utu wao.

Ni nini huwawezesha kubadilika? Ni nguvu ya neno la Mungu, au ujumbe wake. Paulo aliandika hivi kuhusu nguvu za neno la Mungu linalopatikana katika Biblia: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na urojorojo wake, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” (Waebrania 4:12) Mtu anapokubali roho takatifu ya Mungu imwongoze na kujaribu kujipatanisha na viwango vya maadili vya Biblia, utu wake unaweza kubadilika hatua kwa hatua. Utu wa Kikristo unaofanyizwa kwa njia hiyo unatia ndani “upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu.”—Wakolosai 3:12.

Usawaziko wa Kikristo

Ni kweli kwamba hakuna kanuni ya Biblia inayowakataza watu kuchunguza aina za damu. Lakini hiyo ni tofauti ikiwa uchunguzi huo unatumiwa kuamua utu wa wanadamu. Kama ilivyo na mambo yote maishani, ni lazima tuache Neno la Mungu liongoze hatua zetu. (Zaburi 119:105) Usawaziko ni muhimu pia.—Wafilipi 4:5.

Bila shaka mtu hapaswi kuona aina yake ya damu kuwa kisingizio cha kutorekebisha utu wake. Licha ya tabia walizorithi, ni lazima Wakristo waendelee kurekebisha utu wao ili ufanane na ule wa Yehova na Yesu kwa kadiri inavyowezekana.—Waefeso 5:1.

Isitoshe, Wakristo hujitahidi kuwaona wengine jinsi Yehova anavyowaona. “Mungu hana ubaguzi.” (Matendo 10:34, 35) Yehova huwakubali watu wa namna zote. Hivyo haifai wala si Ukristo kuwaepuka wengine kwa sababu ya aina yao ya damu. Pia haifai kushirikiana tu na watu walio na aina yako ya damu. Biblia inaonya hivi: “Mkiendelea kuonyesha upendeleo, mnafanya dhambi.”—Yakobo 2:9.

Kadiri sayansi na teknolojia inavyozidi kupiga hatua, mavumbuzi na dhana nyingi kuhusu mwili wa mwanadamu zinabuniwa. Ni kawaida kusisimuliwa na mambo hayo. Hata hivyo, Wakristo wanapaswa kuacha mawazo yao yaongozwe na Biblia wala si dhana za wanadamu. Katika maisha yao yote, Wakristo wanahitaji ‘kuhakikisha mambo yote’ na ‘kushika sana yaliyo mazuri.’—1 Wathesalonike 5:21.