Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dumisha Maoni Yanayofaa Kuhusu Wanyama- Vipenzi

Dumisha Maoni Yanayofaa Kuhusu Wanyama- Vipenzi

Dumisha Maoni Yanayofaa Kuhusu Wanyama- Vipenzi

KAMA ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, wanadamu walipewa daraka la kutunza dunia na wanyama wote. Biblia inasema hivi: “Kila kitu [Mungu amekiweka] chini ya miguu yake: kondoo na mbuzi na ng’ombe, wote hao, na pia wanyama wa porini, ndege wa mbinguni na samaki wa baharini.”—Zaburi 8:6-8; 115:16.

Ni muhimu wanadamu wazingatie jinsi wanavyowatendea wanyama. Neno la Mungu linasema hivi: “Mwadilifu anatunza nafsi ya mnyama wake wa kufugwa.” (Methali 12:10) Kwa kweli, sheria ambazo Mungu aliwapa Waisraeli zilikazia uhitaji wa kuwajali wanyama. (Kumbukumbu la Torati 22:4, 10; 25:4) Kadiri wanadamu wanavyoendelea kutekeleza daraka lao, wamekuwa na uhusiano wa karibu na wanyama wa kufugwa na hata wamewafuga wanyama wa mwituni.—Mwanzo 1:24.

Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba Biblia huonyesha kuna tofauti kati ya wanadamu na wanyama. Wanadamu ndio walioumbwa ‘kwa mfano na sura ya Mungu’ wala si wanyama. (Mwanzo 1:26) Isitoshe, ingawa wanadamu waliumbwa waishi milele duniani, haikuwa hivyo kwa wanyama. (Mwanzo 3:22, 23; Zaburi 37:29) Yesu Kristo alisema kwamba ili tufurahie “uzima wa milele,” ni lazima tumwamini Mungu na tujifunze kumhusu—mambo ambayo wanyama hawawezi kuyafanya. (Yohana 3:36; 17:3) Isitoshe, Biblia inawalinganisha wale ambao hawastahili kufufuliwa na “wanyama wasiofikiri waliozaliwa kiasili ili kukamatwa na kuangamizwa.”—2 Petro 2:9-12.

Waliumbwa Kuwafaidi Wanadamu

Mungu aliwaumba wanyama kwa ajili ya wanadamu. Wanyama wanaweza kuwasaidia wanadamu kufanya kazi zao na wanaweza kuwa marafiki au wanyama-vipenzi. Pia wanaonyesha upendo na hekima ya Mungu. Ama kweli, inapendeza kuona uzuri wa wanyama na kujifunza mengi kumhusu Muumba kwa kuchunguza hekima yao ya kisilika yenye kustaajabisha. (Zaburi 104:24; Methali 30:24-28; Waroma 1:20) Wadudu ni mfano mmoja wa hekima hiyo. Inastaajabisha jinsi nyuki huwasiliana na kufuata harufu zinazoongoza kwenye chakula na kujenga mizinga iliyo tata sana.

Wanadamu wanaweza kula wanyama. Mwanzoni Mungu aliwaruhusu wanadamu wale mimea tu. Lakini zaidi ya miaka 1,600 baadaye—kufuatia Furiko la siku ya Noa—Mungu alisema hivi: “Kila mnyama anayetembea ambaye yuko hai anaweza kuwa chakula chenu. Kama nilivyowapa mimea ya majani, nawapeni hao wote.” (Mwanzo 1:29; 9:3) Hivyo, Mungu aliwaruhusu wanadamu kula wanyama. Inaonekana Mungu aliwaruhusu wanadamu wale nyama kwa faida yao ijapokuwa hakuwa ameruhusu jambo hilo mwanzoni.

Matatizo Kati ya Wanyama-Vipenzi na Wanadamu

Inaonekana kwamba katika historia yote, wanyama-vipenzi hawakufugwa ndani ya nyumba na ndivyo ilivyo katika sehemu nyingi duniani. Hata hivyo, siku hizi watu wamehamia mijini na wamekuwa matajiri, hivyo wanafuga wanyama-vipenzi ndani ya nyumba. Jambo hilo limeleta matatizo katika nchi zilizoendelea.

Inakadiriwa kwamba kuna wanyama-vipenzi milioni 500 duniani, na asilimia 40 hivi wanapatikana Marekani. Mbwa milioni 59 hivi na paka milioni 75 hufugwa huko. Lakini idadi ya wanyama wanaofugwa katika kila nyumba huko London na Paris ni kubwa kuliko ya New York City!

Miaka michache iliyopita huko Paris, pikipiki ndogo 70 zilikodishwa kusafisha kinyesi cha mbwa barabarani. Ilikadiriwa kwamba mbwa 250,000 wanaopatikana Paris walikunya tani 25 za kinyesi kila siku, na ni kiasi kidogo sana kilichoondolewa na pikipiki. Inasemekana kwamba kila mwaka, mamia ya watu walijeruhiwa na kulazwa hospitalini baada ya kuteleza juu ya kinyesi.

Isitoshe kuna tatizo la kelele. Watu fulani wenye mbwa huvumilia tabia za wanyama hao kuliko wanavyoweza kuvumilia za wanadamu. Kulingana na kituo cha Internet kinachoitwa Utunzaji wa Wanyama-Vipenzi, “inaonekana watu wenye mbwa wanaobweka sana wamezoea kelele hizo.” Kwa mfano, wengine hawawazuii mbwa wao kubweka hata kama kelele hiyo inazuia mazungumzo muhimu.

Kwa upande mwingine, mbwa anaweza kuwa mtulivu na mwenye furaha akiwa pamoja na bwana wake, lakini mwenye kusumbua majirani sana wakati bwana wake hayuko. Ni kweli kwamba watu wanaofuga wanyama huenda wakawapenda licha ya kasoro hizo, lakini jirani anayefanya kazi kwa zamu au mama anayejaribu kumbembeleza mtoto alale huenda asielewe jambo hilo. Isitoshe, wanyama wanaweza kusitawisha tabia mbaya na hata kuwa wakali wanapohuzunika.

Tatizo lingine la wanyama-vipenzi jijini ni kwamba wanazaana haraka. Inakadiriwa kwamba mbwa milioni 17 na paka milioni 30 huzaliwa kila mwaka huko Marekani. Mamilioni ya wanyama hao huishi kwenye vituo vya kutunza wanyama ambako inakadiriwa kwamba kila mwaka wanyama milioni nne hadi sita huuawa.

Kwa nini wanyama wengi hupelekwa kwenye vituo hivyo? Mara nyingi ni kwa sababu watu humpenda mnyama kwa muda mfupi tu. Kitoto maridadi cha mbwa au cha paka hukua na kuhitaji utunzaji. Lakini hakuna yeyote nyumbani mwenye wakati na subira ya kucheza au kumzoeza mnyama huyo. Dakt. Jonica Newby, ambaye ni mwandishi na mtaalamu wa wanyama, anasema hivi: “Tofauti na wengi wanavyodhani, uchunguzi uliofanywa ulimwenguni pote unaonyesha kwamba nusu ya mbwa wanaopelekwa katika vituo vya utunzaji hawajatupwa, bali wamepelekwa huko na wenyewe ambao hawawezi kuvumilia tena kelele, uharibifu, na usumbufu wao.”

Habari moja kuhusu idadi kubwa ya wanyama-vipenzi inasema hivi kuhusu hali hiyo: “Wanyama wamekuwa kama takataka, wanakumbatiwa wanapokuwa wachanga na kutupwa wanaposumbua. Kutowajali wanyama jinsi hiyo kumeongezeka na kunaharibu utamaduni wetu.”

Mambo Muhimu Tunayopaswa Kufikiria

Tunapaswa kufikiria sana kabla ya kufuga wanyama, hasa mjini. Wanyama wenye afya wanahitaji mazoezi kila siku. “Uchunguzi wa Kitaifa Kuhusu Wanyama-Vipenzi na Wanadamu” nchini Australia ulisema hivi: “Mbwa anahitaji kutembea na kufanya mazoezi mengine ili awe na afya na kuchochea ubongo wake. Inaweza kuwa vigumu kushughulika na mbwa wasiopata mazoezi ya kutosha.” Lakini wengi wanaofuga mbwa huwa wamechoka sana baada ya kufanya kazi ngumu mchana hivi kwamba hawawezi kuwatembeza ili watumie nguvu zao.

Hivyo wale wanaotaka kufuga wanyama-vipenzi wanapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, nitaweza kumtunza vizuri mnyama huyo? Je, maisha yangu ya kila siku yatamfanya awe peke yake kwa muda mrefu? Je, nitapata wakati wa kumtembeza au kucheza naye? Iwapo mbwa wangu anahitaji mazoezi, niko tayari kumzoeza au kumpeleka katika shule ya kuwazoeza mbwa? Je, kuwa na mnyama kutanizuia kufanya mambo muhimu zaidi?’

Jambo lingine la kuzingatia ni kwamba kuwa na mnyama kunaweza kugharimu sana. Uchunguzi uliofanywa kuhusu watu wanaofuga wanyama ulionyesha kwamba gharama za kumtibu mbwa mmoja kila mwaka huko Marekani zilikuwa dola 196 na za paka dola 104. Hiyo haitii ndani gharama za chakula na mahitaji ya kila siku. Isitoshe katika maeneo fulani kuna gharama za kuwasajili wanyama.

Ni Vigumu Kuwa na Maoni Yanayofaa

Muumba wetu hufurahi tunapopendezwa na kuwatunza wanyama aliowaumba. Basi je, hukubali kwamba ni vibaya kuwatesa wanyama? Lakini watu wengine hufurahi kuwaona wanyama kama vile fahali, mbwa, na kuku wakiteseka na kuuana wanapopigana. Inasikitisha kwamba wanadamu hawawatendei wanyama kwa huruma kama vile Mungu alivyokusudia.

Kwa upande mwingine, watu wengine huwahangaikia wanyama sana na kupuuza mambo muhimu zaidi. Kwa kweli, wanyama wanapopendwa kupita kiasi, huenda uhai wao ukaonwa kuwa muhimu kuliko wa wanadamu. Kwa mfano, moto ulipotokea katika hospitali moja ya wanyama, wenyewe walikusanyika nje na inasemekana wengine “walijaribu kuwapita wazimamoto wakisema kwamba eti wanataka kufa na wapenzi wao.”

Bila shaka ni jambo la kuhuzunisha sana kumwona mnyama-kipenzi akifa. Lakini hata katika hali hiyo, tunapaswa kuwa na maoni yanayofaa. Kama tulivyoona mapema, wanyama hawakuumbwa kwa mfano wa Mungu wala hawakukusudiwa waishi milele kama wanadamu. Biblia inasema hivi kuhusu jinsi Mungu alivyowaumba wanadamu: “Tena ameiweka hiyo milele ndani ya mioyo yao.” Lakini haisemi hivyo kuhusu wanyama.—Mhubiri 3:11, Union Version.

Hivyo, Biblia haisemi kwamba ni kosa kuwaua wanyama. Ama kweli, wao huliwa na mamilioni ya watu. Lakini vipi kumwua mnyama-kipenzi anayeugua na kuteseka? Huo ni uamuzi mgumu na wenye kuhuzunisha! Mwenyewe anaweza kuamua kwamba kufanya hivyo haraka bila kumuumiza ni bora kuliko kurefusha maisha ya mnyama-kipenzi kwa matibabu yanayogharimu sana na kumfanya ateseke zaidi. Na huenda kurefusha maisha yake kukasababisha hali ngumu ya kifedha katika familia.

Kwa kuwa Mungu anawapenda wanadamu sana, je, hatupaswi kuwapenda na kuwajali wanyama ambao ametupatia tuwatunze? Wale walio na upendo kama huo wamevutiwa na tumaini la kufurahia wanyama kama vile Muumba wetu alivyokusudia mwanzoni. Makala ya kumalizia katika mfululizo huu itazungumzia jambo hilo.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kwa nini mamilioni ya wanyama katika vituo vya utunzaji huuawa kila mwaka?

[Hisani]

© Hulton-Deutsch Collection/CORBIS

[Picha katika ukurasa wa 8]

Mambo mengi sana yanahitajiwa ili kumfuga mnyama-kipenzi hasa mjini

[Picha katika ukurasa wa 9]

Muumba wetu hufurahi tunapowatendea wanyama kwa fadhili